Story
azazi wake
walibaki wakimwangalia jinsi anavyozunguka pale chumbani wakijua wazi. “Jipe muda wa kufikiria zaidi Elvin.
Ndoa sio kitu cha kukimbilia.” Mwasha
alijaribu kutupia neno. “Bella ni mke wangu baba. Nilishakueleza kila kitu.
Na kuwa mjamzito hakubadilishi chochote. Ila ni kweli namuhurumia sana. Alikuwa
amefurahia sana kuachana na Mzee Masha. Leo akija kujua amebeba mtoto wake!
Nahisi atachanganyikiwa.” “Sasa
nashauri mpe muda wa kupumzika, usimwambie kitu chochote kwanza. Amehangaika
sana kuniuguza huyu mtoto. Alikuwa halali, mpaka nilikuwa nikimuhurumia. Ngoja
apate muda wakupumzika, akili yake ikishatulia ndio umwambie swala la ujauzito.
Ukishaona jinsi alivyolipokea, ndipo uendelee na maswala ya uchumba. Lakini
naomba upate muda wakufikiria Elvin. Ujue mtaanza maisha ya ndoa na Bella,
akiwa na mtoto ambaye sio wako!” “Nampenda Bella, mama. Hayo ni matokeo ya
maisha aliyoishi zamani. Nilazima mimi ndio niwe mume wa Bella.
Nitachanganyikiwa nikija kuona anaolewa na mtu mwingine.” Mama Mwasha alicheka kidogo. “Haya Elvin, sisi tunakuombea.
Tunaamini mawazo yako.” Elvin
alifikiria kidogo. “Asanteni
kwa ushauri wenu na kumpokea Bella na Eric. Asanteni sana. Na nitafanya kama
mlivyonishauri.” “Na mimi
itabidi nimtafute Mzee Masha nizungumze naye, kabla hamjarudi, nijue ni jinsi
gani atamsaidia Bella na huyo mtoto. Asibaki akilea mwenyewe.” “Ni kweli baba.
Na kwa kuwa Mzee Masha anakuheshimu sana, najua mtaelewana tu.” Elvin alitoka lakini akiwa amechanganyikiwa.
atagairi
baada ya kusikia Bella ni mjamzito
My Past - Sehemu ya 11
|
W
|
azazi wake
walibaki wakimwangalia jinsi anavyozunguka pale chumbani wakijua wazi. “Jipe muda wa kufikiria zaidi Elvin.
Ndoa sio kitu cha kukimbilia.” Mwasha
alijaribu kutupia neno. “Bella ni mke wangu baba. Nilishakueleza kila kitu.
Na kuwa mjamzito hakubadilishi chochote. Ila ni kweli namuhurumia sana. Alikuwa
amefurahia sana kuachana na Mzee Masha. Leo akija kujua amebeba mtoto wake!
Nahisi atachanganyikiwa.” “Sasa
nashauri mpe muda wa kupumzika, usimwambie kitu chochote kwanza. Amehangaika
sana kuniuguza huyu mtoto. Alikuwa halali, mpaka nilikuwa nikimuhurumia. Ngoja
apate muda wakupumzika, akili yake ikishatulia ndio umwambie swala la ujauzito.
Ukishaona jinsi alivyolipokea, ndipo uendelee na maswala ya uchumba. Lakini
naomba upate muda wakufikiria Elvin. Ujue mtaanza maisha ya ndoa na Bella,
akiwa na mtoto ambaye sio wako!” “Nampenda Bella, mama. Hayo ni matokeo ya
maisha aliyoishi zamani. Nilazima mimi ndio niwe mume wa Bella.
Nitachanganyikiwa nikija kuona anaolewa na mtu mwingine.” Mama Mwasha alicheka kidogo. “Haya Elvin, sisi tunakuombea.
Tunaamini mawazo yako.” Elvin
alifikiria kidogo. “Asanteni
kwa ushauri wenu na kumpokea Bella na Eric. Asanteni sana. Na nitafanya kama
mlivyonishauri.” “Na mimi
itabidi nimtafute Mzee Masha nizungumze naye, kabla hamjarudi, nijue ni jinsi
gani atamsaidia Bella na huyo mtoto. Asibaki akilea mwenyewe.” “Ni kweli baba.
Na kwa kuwa Mzee Masha anakuheshimu sana, najua mtaelewana tu.” Elvin alitoka lakini akiwa amechanganyikiwa.
********************************************
Ni kweli Bella alikuwa akiendelea kunenepa. Kwa kuwa akili
zake zilikuwa kwa Mama Mwasha hakupata muda wakujifikiria hata kidogo. Alilala,
akaamka ilishakuwa jioni. Aliingia bafuni kuoga, akarudi kwenye sanduku lake
alilokuwa ameliacha hapo nyumbani, akaanza kutafuta nguo ya kuvaa kwenye
tafrija. “Elvin! Elvin!” Walimsikia akimwita Elvin akiwa
chumbani kwake, wakajua ameamka. Elvin akagonga na kuingia. Alimkuta amejifunga
kitenge cha Mama Mwasha na amekasirika sana. “Vipi?”
“Nguo zote hazinienei, nitavaa nini?” “Umejaribu zote.” “Ndiyo. Hazinienei,
zinabana na sitaki kubanwa hata kidogo leo.” “Pole. Unataka niende kule kwako
nikakuletee nguo zingine?” “Nitashukuru sana. Basi nalala tena kidogo wakati
nakusubiria. Najisikia mwili unachoka. Tokea nipo India. Nilimwambia mama, akasema
labda kwa kuwa silali vizuri usiku.” “Labda. Basi lala, nikirudi nitakuamsha.”
“Lakini njaa pia inauma sana, Elvin.” “Ngoja nikakuletee chakula. JJ
ameshaivisha.” Bella
alitabasamu. “Asante Vin.” Elvin alirudisha tabasamu na kutoka.
Baada ya muda mfupi akarudi na sahani ya chakula. Bella
alikivamia kile chakula, akaanza kukila bila kupumzika, Elvin alibaki
akimshangaa. “Nenda basi
ukaniletee nguo. Ujue sina nguo kabisa.” “Haya. Sitachelewa. Nitarudi sasa
hivi.” Elvin alimtoa
headphone Eric masikioni. “Twende unisindikize.” “Subiri kidogo Elvin,
namalizia.” “Hapana Ric. Nenda bwana na Elvin sasa hivi mkaniletee nguo.”
“Namalizia kidogo Bella.” “Eric wewe!” “Basi Bella. Ngoja niende.” Bella aliinamia sahani yake na
kuendelea kula bila kuongeza neno.
Elvin na Eric walirudi na nguo zote za Bella. Wakamkuta
amelala kama aliyekufa. “Bella!
Bella! Amka wageni wameshaanza kufika.” “Nataka kulala kidogo Elvin. Nipe kama
dakika kumi nitaamka.” “Nakupa dakika 20 nyingine Bella, nikirudi nilazima
utoke hapo kitandani.” Kabla
hajamaliza kuongea, alimsikia Bella akihema kuashiria alishapotelea usingizini.
Elvin alisimama pale akimwangalia kwa muda. Akamfunika shuka vizuri, akabaki
amekaa pembeni yake akimtazama. Bella alikuwa mzuri sana. Alijaliwa sura nzuri,
ya kuvutia kuangalia. Elvin alicheka kidogo, kila akikumbuka visa vya Bella
aliendelea kucheka. Alikuwa akimsubiri kwa hamu sana, ili waongee na wataniane
lakini Bella alirudi mchovu na mtulivu sana. Alikaa pale akifikiria zaidi ya
nusu saa.
“Bella! Bella!” Bella alishtuka. “Nilikuwa
na hamu na wewe kweli!” “Hata mimi Elvin.” “Sasa mbona huamki tukaongea?”
“Pole. Nilikuwa nimechoka. Basi navaa sasa hivi nakuja. Umesikia?” “Usichelewe
basi.” Kabla Elvin hajasimama
ili atoke, mlango ulifunguliwa. “Nyinyi
mbona hamtoki?” Eno akauliza. “Nilipitiwa na usingizi. Nakuja
sasa hivi.” Bella alijibu,
akasimama na kuanza kutafuta nguo. Eno alitoka na kuwaacha pale chumbani, Eric
akiwa amepotelea kwenye michezo yake. “Hivi
huyu alikuwa anafanya kitu kingine au ni hizi game tu?” “Nilikuwa nikienda nae
kazini kuanzia asubuhi mpaka usiku. Alikuwa anachoka mpaka namuhurumia.”
“Afadhali.” Bella alianza
kutafuta nguo.
“Mbona umeleta nguo zote?” “Si tunaishi wote
hapa?” “Elvin wewe! Natakiwa turudi nyumbani kwetu, maisha mengine yaendelee.
Hatuwezi kuhamia hapa moja kwa moja.” “Kwa nini?” “Elvin jamani!” “Niambie
Bella, kwa nini hutaki tuishi hapa pamoja?” “Unajua hatuwezi Elvin. Hapa ni
nyumbani kwa wazazi wako. Mimi nipo na Ric, hatuwezi kuhamia tu hapa. Si sawa.”
“Kwa hiyo kama hapa ingekuwa ni nyumbani kwangu, je?” “Halafu ukanitaka tuishi
wote?” Bella na yeye akauliza. “Ndiyo. Ungekubali?” “Haraka sana
tena bila hata kufikiria mara mbili. Ningehamisha vitu vyangu vyote mpaka
vijiko.” Elvin akacheka.
“Basi utanifanya niharakishe kumalizia ile nyumba kwa
haraka sana.” “Kwa hiyo ikiisha utatuchukua mimi na Ric?” “Haraka sana.” Bella alianza kucheka. “Usije
kumaliza kujenga ukatukimbia sisi halafu ukahamia na watu wengine!” “Nishawahi
kukuahidi kitu halafu sijatimiza Bella?” Bella akacheka tena. “Hujawahi Elvin.” “Basi tuwe wavumilivu. Nikimaliza
tu kujenga, tunahamia wote. Tutakuwa tukiishi wote Bella. Si hauta nikimbia?” Bella alifurahi sana. “Nikikimbia, tunakimbia wote. Mimi,
wewe na Eric. Ric akioa tunabaki mimi na wewe tu, Vin. Ni sawa?” Elvin alikuwa akicheka kwa furaha. “Kabisa. Lakini tukae wote hapa
kidogo, usikimbilie kurudi kule kwako. Kwanza naona Ric ameshapazoea hapa.”
“Ameniambia, na kila nikimwambia itabidi tuondoke turudi kwetu ananizungusha na
maneno mengii. Mara nisubirie mpaka shule zifungue, mara hiki. Anaonekana
amepafurahia sana hapa. Ric anapenda watu. Anatamani kuishi kwenye nyumba ya
watu wengi sio sisi wenyewe wawili tu.” Mlango
ulifunguliwa tena. “Bella njoo
nikutambulishe kwa Mchungaji wetu.” Mama
Mwasha aliingia. “Natafuta
nguo mama. Nguo zote zinabana. Sijui ni sababu ya kula sana? Kila saa nasikia
njaa. Hapa sina nguo ya kuvaa hata moja, mama yangu!” Bella aliendelea kulalamika.
“Ngoja nikusaidie kutafuta nguo, Bella. Mpe muda mfupi tu
mama. Atakuja kusalimia wageni.” Elvin
aliingilia maongezi yao na kuinama kwenye sanduku la Bella na kuanza kumtolea
nguo za kujaribisha. “Inabidi
kwenda kununua nguo nyingine kesho.” “Kweli Elvin, kuliko hii shida
tunayopata.” Mwishowe alipata
gauni kubwa kidogo, lilikuwa limechanua kuanzia chini ya kifua. Lilimkaa vizuri
sana. “Umependeza sana.” Bella akacheka. “Asante. Na nimelipenda
hili gauni halijanibana hata kidogo. Lakini njaa inauma tena, Elvin.” “Ndio
tutoke ukale.”
Elvin na Bella walitoka pale chumbani na kuelekea jikoni
kula. Baada ya kula tena, Bella alitoka kusalimiana na wageni. Hakuna
aliyemuona Bella akatosheka kumwangalia binti huyo. Cheko ilimtawala usoni
wakati wote nakumfanya kila anaye ongea naye asichoke wala kujisikia vibaya. Na
usiku ule waliufanya ukawa ni usiku maalumu kwa Bella. Watoto wa Mama Mwasha
walikuwa wamemwandalia zawadi nzuri sana, kama kumshukuru lakini walijua usiku
huo ndio mdogo wao angemvalisha pete ya uchumba pia. Bella alikuwa akitoa
machozi ya furaha. “Na
tumekuandalia sehemu maalumu ya kwenda kupumzika kabla yakurudi kazini. Elvin
na Eric watakusindikiza.” JJ
alitangaza mbele za wageni wote waliokuwa wamefika mahali pale. “Asanteni
sana jamani. Lakini sijui niseme nini? Sikuwa nimejiandaa. Na wala msinge
hangaika kwa kiasi hiki jamani! Mama Mwasha ni mama yangu.” Watu walikunywa na kula, lakini Irene na wenzake hawakuacha
kunong’ona, huku rafiki wa Mama Mwasha na wao wakiongea kivyao.
Hakikumsumbua sana Mama Mwasha juu ya minong’ono na jicho
la husuda kwa Bella. Kwanza alijua ni wivu ndio unaowasumbua. Uzuri wa Bella,
ulikuwa sio wakufichika, na wema wake haukuwa wakinafika. Hata alipocheka,
alionekana ni mwanadamu mwenye moyo mzuri kutokea moyoni. Hakuwa ameficha hila
ndani yake. Tafrija iliisha, kila mtu akaondoka, wakabaki wao kama familia
wakiongea na kucheka.
********************************************
“Sasa jamani, Bella akishatoka mapumzikoni na Elvin na sisi
tunaenda mapumzikoni mwezi mzima. Njoo kwanza hapa kwenye meza ya chakula
tuongee mambo yetu ya familia yetu.” Eli alianza kumchokoza tena. “Wewe na nani?” Bella alimuuliza. Eli akaenda kumshika
mkono pale alipokuwa amekaa sebleni na kumvutia mezani. “Si wewe na mimi!” Bella alianza kucheka bila kunyamaza
mpaka machozi na kufanya wengine waanze kucheka pia. “Sasa unacheka nini wewe Bella?” “Nacheka mambo mengi sana.” “Nini?”
“Ujue wewe Eli una utani mbaya sana? Kwanza sitaki mwenyewe!” “Kwa nini?”
“Namtaka Vin.” “Sasa safari hii si unakwenda na Vini, halafu ukirudi ndio
tunaenda sisi!” “Kwanza
haitwi hivyo. Unaharibu jina lake mwenyewe. Mimi naenda kulala, nimechoka.
Twende Vin unisindikize.” “Ngoja
mimi nikusindikize Bella wangu.” “Akuuu! Naenda zangu na Vin. Wewe mchokozi
sana Eli.” Bella alipandisha
mabega yake yote kukataa.
“Mimi na wewe Bella?” “Mmmh!” Bella aliguna, kisha akaanza kucheka tena. “Ila ujue Eli mimi nakupenda sana?
Nilikuwa nakukumbuka nacheka mwenyewe.” “Najua kama unanipenda Bella. Huwezi
kuishi bila mimi.” “Sasa usianze kujisifia. Kama ndio hivyo nafuta urafiki na
wewe, siongei na wewe tena.” “Nina uhakika huwezi Bella.” Bella alisimama akaanza kuondoka kimya
kimya kumfuata Elvin. “Aaaah!
Ndio umeanza kuninunia? Njoo Bella wangu bwana.” “Sitaki tena. Twende Vin.” Alienda kumfuata Elvin alipokuwa
amekaa, akamshika mkono. “Usiku
mwema Bella. Uniote mimi eeh!” Eli
alimchokoza tena. Akarudi na kumbusu shavuni kimya kimya akaondoka. “Bwana Bella ananipenda jamani!
Hawezi kulala bila kunibusu!” Bella
akarudi akamfuta pale alipombusu. “Nimechukua
busu langu.” Kila mtu alianza
kucheka. “Mjinga wewe!” Bella akarudi kumshika Elvin mkono
wakaondoka.
“Elvin aweka ahadi ya Maisha kwa
ndugu hao wawili”
Elvin, Bella na Eric waliondoka asubuhi na mapema
wakielekea mapumzikoni. Elvin aliwapitisha kwenye nyumba yake. Wakapata muda
wakuzunguka eneo zima, huku Elvin akimtaka Bella ushauri. Nini kiongezwe, nini
kiwekwe wapi. Bella naye alimpa ramani nzuri sana ya bustani, na kumpongeza
Elvin kwa ujenzi wa hiyo nyumba. “Ric!
Unajua kuwa hapa ndio patakuwa kwetu?” Elvin
alimgeukia Eric. “Unamaanisha
nyumbani kwetu pamoja na mimi na Bella?” “Ndiyo.” Elvin alijibu. “Kweli Elvin?” Eric aliuliza akionyesha mashaka. “Huniamini?” “Nakuamini, lakini
nilidhani unanitania.” Eric
aliongeza. “Sikutanii Ric.
Hapa ndipo patakuwa nyumbani kwetu.” Eric
alitulia kidogo. Bella hakuwa ameelewa. Alitegemea mdogo wake afurahie. “Vip Ric?” Bella alimshika begani. “Hujapapenda?” “Naogopa Bella. Huwa wanabadilika.”
“Sio Elvin. Elvin hajawahi kutuahidi kitu halafu akashindwa kutimiza.” Bella alimuhurumia mdogo wake. “Siwezi kuwageuka Eric. Na sina
sababu yakufanya hivyo. Tuombe Mungu ili iishe haraka, tuhamie. Kwanza tutakuwa
tukija wote huku wakati wanamalizia kujenga, ili na wewe utoe mawazo yako.” Eric alicheka bila ya kujibu kitu. “Asante Vin.” Bella aliamua kushukuru kwa ahadi
aliyokuwa amepewa. “Mimi ndio
nitakuwa na furaha zaidi, mkija kuishi na mimi hapa. Mmeniongezea shauku ya
kumaliza mapema.” Walizunguka
pale kwa muda, kisha wakaamua waendelee na safari yao.
********************************************
Wote walitoka pale wakiwa na furaha sana. Eric na Bella
walikuwa wakiimba njia nzima, Elvin dereva akiwa anawasikiliza ndugu hao.
Walifika Bagamoyo, mazingira ya hoteli yalimfurahisha sana Bella kitu
kilichomfanya na Elvin afurahi. Kwa Eric yeye hakuwa na neno, ilimradi yupo na
dada yake, hakujali alipo. “Nataka
kuogelea kabla jua halijaisha, Bella.” Eric
alipenda sana kuogelea. “Subiri
tutaenda kuogelea wote.” Walipopata
chakula cha mchana, wote walielekea kuogelea kwenye pool sio baharini.
Walishinda huko wakila na kunywa mpaka ilipofika jioni. “Nimechoka nataka nikalale kidogo,
Elvin.” “Basi nitakuletea chakula cha usiku chumbani.” Bella aliondoka akaenda kulala
akawaacha Elvin na Eric pale pale.
Usiku Elvin na Ric walienda kumgongea Bella chumbani kwake.
Bella alikuwa na chumba chake, Elvin na Eric na wao walikuwa na chumba chao. “Naomba hata nusu saa nyingine,
Elvin. Nitaamka kula hicho chakula.” Bella
hakutaka kutoka kitandani. “Hapana
Bella. Amka ule, ukishiba ndio utalala vizuri.” Bella alikaa na kuanza kula. “Bella!” Eric aliita. “Kesho naomba tukaogelee baharini.”
“Wewe huchoki kuogelea!? Leo tumeshinda kwenye maji siku nzima!” “Bella please!”
“Sawa, samaki. Kesho tukiamka tunahamia baharini.” Eric akacheka. “Unaniita samaki?” “Kwa kuwa
huchoki kukaa majini.” Eric
alipanda kwenye kitanda cha dada yake, akaanza kuruka ruka. “Shuka bwana Ric, utanifanya
nitapike.” “Miss you Bella. Unalala tu, hujapata muda na mimi hata kidogo!” Eric aliacha kuruka ruka, akabaki
akiendelea kuongea naye huku bado akiwa kitandani kwake amepiga magoni, amemuegemea
mabegani huku akimchungulia usoni.
“Na mimi pia ninahamu na wewe, Ric. Najua nimerudi na
uchovu mwingi. Nikiamka kesho nitakuwa na nguvu, tutapata muda wakutosha.
Umenisikia?” “Hope so.” Eric alionyesha kutokuridhika. “Promise Ric. Tutapata muda kesho. Tutacheza mpaka unikimbie.” “Wewe
ndio huwa unakimbia ukishindwa, Bella. Sio mimi.” “Riccc!!!” “Muulize Elvin.
Hukukimbia siku ile?” “I was tired.” Bella
alijibu. “Hicho ndio
kisingizio chako kila siku, Bella.” Elvin
alikuwa akicheka tu. “FINE. Tutaona kesho.” Bella alijibu kwa ujasiri. “Si umemsikia mwenyewe Elvin? Kesho
akisema amechoka, hakuna kumruhusu kurudi kulala. Mpaka nimfunge magoli
yakueleweka ndia ataruhusiwa kuja kulala.” “Usije kulia tu, hiyo kesho.” “Sawa
Bella.” “Basi narudi kulala, ili kesho niamke na nguvu.” Bella alijirudisha kitandani. Alikuwa
na uchovu usioisha.
“Wakati wewe unalala sisi tutakuwa tukiangalia tv hapahapa
chumbani kwako.” Elvin
alijirusha na yeye kwenye kochi. “Tucheze
game Elvin.” “Umeanza Ric. Kwani huwezi kuwa kama watu wengine? Unacheza game
kila wakati!” Bella
aliwaingilia. “Leo sijacheza
hata kidogo Bella.” “Sitaki kuwaingilia. Mimi naenda kupiga mswaki nilale.
Nyinyi endeleeni kufanya chochote mnachotaka.” “Ila umeniahidi kuogelea bahari
kesho.” “Nakumbuka Ric. Na
tutaenda kuanzia asubuhi mpaka usiku. Mimi nikiamka tu, nitaelekea baharini,
mnifuate huko.” Eric alienda
akambusu dada yake. Bella akaenda kupiga mswaki, akarudi kujitupa kitandani
kulala.
********************************************
Aliamka ilishakuwa asubuhi, kumepambazuka. Hakuamini kama
alilala kwa kiasi kile. Akaangaza macho yake kulia na kushoto hakumkuta Eric
wala Elvin. Alijisikia ameamka na nguvu mpya. Akakumbuka ahadi aliyomuahidi Eric. Alivaa
nguo za kuogelea, akachukua taulo lake akatoka kuelekea chumbani kwa kina
Elvin. Alipoona wamelala. Alirudi chumbani kwake, akaandika ujumbe mfupi kwenye
kikaratasi akaenda kukitumbukiza chini ya mlango wao, yeye akaelekea baharini
asubuhi hiyo kuogelea ili mdogo wake amkute huko baharini, aridhike.
“Mkasa Mwingine Mkubwa wa
Bella"
Kwa kuwa Elvin na Eric walichelewa sana kulala, waliamka
mida ya saa nne. Wakati anaelekea bafuni, Elvin aliona kile kikaratasi.
Nimetangulia
baharini kuogelea.
EnaBella!
Elvin alifanya haraka akabadili nguo, akaamua kumuacha Eric
aendelee kulala, yeye akamfuata Bella ili wapate muda wa peke yao kabla Eric
hajaamka. Alipofika baharini akakuta malapa ya Bella na taulo lake mchangani,
lakini Bella hakuwepo. Alirudi sehemu wanapouzia chakula kumuangalia kama yupo,
kwa kuwa alihisi labda alisikia njaa akaamua kwenda kula kwanza ndipo arudi
kuogelea, lakini Bella hakuwepo. Elvin alizunguka ile hoteli kama mara tatu,
vyooni na mabafuni bila kumuona Bella. Hofu ikaanza kumuingia.
Akarudi baharini kumtizama tena, lakini hakuwepo. Mwishowe
akaamua kujitosa majini na kuanza kumsaka. Aliogelea zaidi ya nusu saa, tena
chini sana ya bahari akimsaka Bella bila mafanikio. “Mungu wangu Bella wangu!” Elvin alianza kuongea peke yake.
Mwishowe akaanza kukimbia kila mahali akimwita mpaka wahudumu na wageni wengine
walipojua kuna tatizo. Elvin aliwaambia Bella amepotea, labda amezama. Uongozi
wa hoteli uliwatuma waokoji humo baharini kumsaka Bella, huku wengine
wakitembea pembeni ya ufukwe kumtafuta. Elvin alikuwa kama amechanganyikiwa.
Aliamua kumpigia baba yake simu. “Vipi mbona unalia?” “Bella
amepotea baba. Nitafanya nini?” “Amepotelea wapi?” Elvin
alisimulia huku akilia sana. “Nampigia simu JJ, tunakuja sasa hivi
kusaidia kumtafuta.” “Msichelewe
baba, nahisi nachanganyikiwa.” “Naomba
utulie Elvin. Eric yuko wapi?” “Mungu
wangu Eric!” Elvin akakata simu na kukimbilia chumbani alipomuacha Eric
amelala. Alimkuta Eric bado amelala kama aliyekufa kwa uchovu wakucheza game
usiku kucha. Elvin alipumua, akafunga tena mlango nakutoka.
Akaamua kupiga tena simu. “Baba mbona hamjafika bado?” “Elvin,
unajua ndio tumetoka kuzungumza sasa hivi, na wewe upo Bagamoyo?” “Kwa hiyo
unakuja au? Mbona kama hamjali?” Elvin alianza
kulalamika huku akigomba sana. “Tunajali Elvin. Hapa wote tupo njiani
tunakuja.” “Samahani baba, nahisi nimepaniki.” “Pole sana. Tunakuja.” “Asante
baba. Naomba msichelewe.” Akakata tena simu.
Baada ya muda alifika Mwasha na familia yake. Kabla
hajamaliza kuelezea ndugu zake kilichotokea, walishangaa kuona Masha na yeye
anaingia na magari ya polisi na mbwa wa polisi kumsaka Bella. Hoteli ilijaa
polisi na waokoaji wa majini. Walirudi tena baharini, huku wakiwa wamegawana
kumsaka Bella. Pesa ya Masha ilikuwa ikiongea kwa nguvu sana siku hiyo.
Aliahidi kwa kutoa hundi pale pale ya pesa nyingi sana, tena kwa kuwaonyesha,
kwa atakayefanikiwa kumpata Bella siku hiyo. “Ukiniletea
Bella hapa, hii pesa ni yako bila maswali.” Masha
aliongeza. Walijitosa watu baharini bila kufikiria. Bella alisakwa baharini na
nchi kavu.
Kelele za mahali pale zilimuamsha Eric aliyekuwa amelala.
Kwani alisikia jina la dada yake likiitwa kwa kipaza sauti. Alishtuka sana na
kukimbilia nje, ndipo alipokuta Hoteli hiyo imefurika watu. Raia kwa Polisi.
Alipoambiwa dada yake amepotea, na yeye alijitupa majini kumsaka. Eric alikuwa
akilia kama amekatwa kidole. Mpaka kufika usiku huo alikuwa amekaukiwa sana. “Isingekuwa
mimi kumlazimisha Bella kwenda kuogelea jana, labda asingepotea.” Eric aliendelea kujilaumu. “Sio kosa lako Eric.” Mzee Mwasha alijaribu kumfariji.
Usiku huo, wote walilala pale pale hotelini. Watu walipiga
kambi ufukweni. Masha alinunua vyakula kwa kila aliyekuwepo pale akisaidia
kumtafuta Bella. Walijaa vijana wengi sana pale hotelini, wakubwa kwa wadogo
waliitana kutoka mtaani wakihangaika baharini kumpata Bella ili wapate pesa ya
Masha na kula chakula cha bure kilichokuwa kikigawiwa usiku kucha. Walikuwa
wakipishana baharini usiku kucha huku jina la Bella likiitwa bila kupumzika.
Wote walilala, lakini sio Masha, kitu kilichomshangaza kila
mtu. Alikuwa kwenye simu usiku kucha akiongea na watu mbali mbali. Polisi
kutoka Dar, walizidi kumiminika hotelini hapo na wote waliletwa na Masha.
Yaliletwa maboti ya uokoaji, yakaanza kuzunguka humo baharini usiku kucha.
Elvin na yeye aliamka asubuhi sana na kurudi baharini. Aliogelea kwa masaa
mengi, juu na chini sana ya maji akimtafuta Bella. Alitoka akiwa amechoka.
Akaanza kuita Bella, mpaka watu wangine waliamka. Walikuta amepiga magoti
ufukweni akiita huku akilia sana. Elvin alikuwa kama amechanganyikiwa.
“Nahisi Bella hayupo huko majini, wamemteka nyara!” Mzee Masha alifikiria kwa nguvu na kufanya kila mtu
afikirie. “Nani atamteka nyara
Bella jamani?” Elvin
aliuliza. “Kama angekuwa
amepotelea majini, mpaka sasa hivi tungekuwa tumeshauona mwili wake.” Masha alikuwa akiongea huku
akifikiria. “Bella hana
maadui. Na alienda kuogelea asubuhi sana. Huyo aliyemteka nyara angekuwa
amefika huku saa ngapi?” Elvin
aliendelea kuhoji. “Ngoja na
mimi niwapigie simu watu baadhi kujua kama ameonekana mahali.” Masha akasogea pembeni kuwasiliana
na watu wake.
“Jinsi
Masha alivyopokea taarifa za ujauzito wa Bella.”
Mzee Masha alipoambiwa habari za ujauzito wa Bella,
alimshangaza mpaka Mzee Mwasha kwa furaha aliyokuwa nayo. Alizipokea zile
habari vizuri sana na kumuahidi Mzee Mwasha kumtunza Bella na mtoto. Hapo hapo
alimpigia simu wakili wake kuwa nyumba ya Kunduchi beach ibadilishwe jina
kutoka kwa mwanae Junior iandikwe jina la Enabella. Na kuahidi kumpa Mzee
Mwasha kiwango fulani cha pesa kila mwisho wa mwezi ili kuhakikisha Bella
anatunzwa vizuri. Mzee Mwasha alihisi Mzee Masha hakuwa amefikiria vizuri,
kwani alizipokea zile taarifa kwa urahisi sana tofauti na alivyotegemea. Mzee
Mwasha alimuomba Masha yeye aondoke pale kwake ili ampe muda wakufikiria kabla
hajaendelea kuahidi mambo mengi zaidi. Lakini Masha alimwambia, zile ni habari
ambazo hakutegemea kuzikia mpaka anaingia kaburini. Akamwambia yeye ni kama
malaika Gabrieli aliyekuwa ametumwa na Mungu, kumwambia
Mariamu atazaa wakati alikuwa bikira. Mzee Mwasha hakumuelewa, kwani Masha
tayari alikuwa na watoto wawili.
********************************************
Ndoa ya Mzee Masha ni kama ilishafikia ukingoni. Kwani
habari za Bella, Irene alihakikisha anamfikishia Junior mpenzi wake wa
siri na Zera, hukohuko waliko. Baada ya watoto wake kujua walikasirika sana,
hawakutaka hata kuongea na baba yao tena. Alipokuwa akienda kuwatembelea
Uholanzi, wale watoto waliondoka nyumbani kwa muda wote waliokuwa wakijua baba
yao yupo nyumbani. Heshima iliwaishia kabisa kwa baba yao. Kile kitendo
kilimkera sana Masha akawaahidi kuwa watamrudia kwa magoti, kwani ile jeuri
waliyokuwa nayo na heshima waliyoweka mtaani, na kwenye mabaa ni pesa yake. Na
kwa kuwa alikuwa na hasira na mama yao zaidi, aliahidi kuwakomoa vibaya sana.
********************************************
Upweke ulishamuandama Masha. Uholanzi akawa haendi tena, na
Bella alishamkimbia. Akabakia na maisha yakutafuta pesa tu. Na kwa kuwa hakuwa
na asili ya kupenda wanawake, hata hivyo alianza kusumbuliwa na pressure sababu
ya matatizo ya familia yake, hakutaka kutafuta mwanamke mwingine tena. Akabaki
akibuni miradi kila leo ili kupoteza mawazo huko. Akawa akiingiza pesa kila
mahali lakini bila furaha. Sasa kuja kupata taarifa kuwa Bella amebeba mtoto
wake, kwake ilikuwa faraja kubwa sana.
********************************************
Kwa kuwa uchunguzi wa siri kubwa sana aliyokuwa akifuatilia
kwa muda mrefu juu ya mkewe na watoto wake ulikuwa umekamilika, Masha akaamua
ahamishe urithi aliokuwa amempa mwanae Junior kwa huyo mtoto wa Bella, ambaye
hata hakuwa amezaliwa. Siku ile ile alipopata taarifa ya ujauzito wa Bella,
akampigia simu huyo wakili wake, akamtajia vitu vya kubadilisha kutoka kwa
Junior kwenda kwa mtoto wa Bella, kisha akaondoka pale nyumbani kwake kwenda
kuweka saini kwa huyo wakili, kuhakikisha hakuna atakayebadilisha tena. Na
hakutaka kufanya siri, mbele ya familia yake waliokuwa na wao wamerudi Tanzania
kwa likizo, aliongea na wakili wake pale pale sebleni, akijua popote walipo
huko vyumbani watamsikia tu.
“Na kuanzia leo, haparuhusiwi sherehe ya namna yeyote
humu ndani. Kwanza hii nyumba ni ya kwangu, nimejenga kwa jasho langu, wote
mmenikuta na mali zangu, hakuna wakunizuia kuongea nitakavyo na kupanga mipango
yangu nitakavyo.” Mzee Masha
alizidi kuongea kwa hasira. “Hamna
shukurani kabisa nyinyi watoto kama mama yenu. Na nitawaonyesha kama mimi ndiye
mwenye mali. Nitamgawia huyo mwanangu anayekuja mali zangu zote. Mbaki mmenuna
nyinyi na mama yenu. Nione mwisho wenu ni nini. Na magari yangu yote nitayauza,
muone jinsi wenzenu wanaotembea na miguu vile wanavyofaida. Na nikitoka hapa,
napitia benki kufunga akaunti zenu nyinyi wote mpaka ya mama yenu, nichukue
pesa yangu. Niwabakishie mshahara wa mama yenu, ili muonje maisha kama ya
watoto wenzenu wanaoishi na mishahara ya wazazi wao tu. Hamna adabu kabisa.” Mzee Masha alitoka na kuwaacha wanae
na mama yao wakiwa wamesogea karibu na alipokuwa amekaa hapo sebleni
wakisikiliza sheria mpya.
********************************************
Bella alitafutwa kwa zaidi ya mwezi mchana na usiku bila
mafanikio. Kwa mara ya kwanza Mzee Mwasha na Mzee Masha waliweza kufanya kazi
kwa karibu na makubaliano makubwa wakati wakutafutwa kwa Bella. Baada ya muda
mrefu sana kupita, walikubaliana kuwa Bella alichukuliwa na mawimbi makali
sana, na labda mwili wake uliliwa na smaki au ulitupwa nchi za jirani kwani
hata vijana wa Masha, walisema hawakusikia tetesi zozote mtaani kama alitekwa
nyara. Na huko pia Masha alimwaga pesa akitaka Bella atafutwe na yeyote
atakayeleta habari kuwa anawajua waliomteka, napo pia aliahidi pesa nyingi
sana. Kwa hiyo sio polisi tu walioingia kazini kumsaka Bella, hata vijana wa
mtaani walipeleleza angalau kupata fununu. Wale wote aliowahisi Masha, aliweka
ulinzi mkali sana wafuatiliwe, bila mafanikio yeyote yale. Walipojiridhisha
kuwa ni kweli Bella hatapatikana tena, walifanya ibada ndogo kama kumbukumbu
yake, watu wakaomboleza na kutawanyika.
********************************************
Eric alikuwa na hali mbaya sana. Hakuacha kutoka pale
nyumbani na kwenda kumtafuta dada yake. “Bella hawezi kuwa amekufa. Namjua Bella, hawezi
kuniacha. Mama aliniambia nitabaki na Bella.” Eric alikuwa akiongea hivyo kila wakati huku akilia na
kumtangazia kila mtu kuwa dada yake yupo hai mahali, wasikate tamaa
yakumtafuta. Hakukubaliana kabisa na wazo lakumfanyia Bella ibada na watu
kukubali amefariki. Alipinga kwa machozi. “Msimkatie tamaa Bella jamani! Atakuwa yupo sehemu
anahitaji msaada wetu. Lazima tuendelee kumtafuta.” Wakati mwingine alitoroka pale nyumbani akiwa peke yake na
kwenda baharini kumtafuta dada yake mpaka usiku.
Ikawa hivyo hivyo hata shule zilipofunguliwa. Alikuwa
akitoroka shuleni na kwenda baharini kumsaka dada yake. Matokeo yake shuleni
yakawa mabovu sana. Mara kwa mara Mzee Mwasha aliitwa shuleni kuzungumzia
maendeleo yake, kwani Mzee Mwasha ndio alibaki kuwa kama baba wa Eric, kwani
hali ya Elvin ilikuwa mbaya zaidi. Hakuacha kumuombolezea Bella. Ilikuwa ngumu
kuamini kama kweli Bella ndio amefariki. Alishinda kazini akifanya kazi,
kuanzia asubuhi mpaka usiku sana bila kula, ila siku za weekend alirudi
Bagamoyo kwenda kumtafuta Bella. Siku zilizidi kwenda lakini wao wawili maisha
yalishindwa kuendelea kabisa. Waliendelea kumsaka Bella kana kwamba ndio
ameondoka jana yake.
“Eric!”
Siku moja Eric alishushwa shuleni na Elvin asubuhi hiyo,
alipoona tu Elvin ameondoka, hakuingia hata ndani ya geti la shule, akageuza
hapo hapo na kuelekea baharini kumtafuta Bella. Mzee Mwasha alifika shuleni
hapo jioni yake kumchukua Eric, lakini akaambiwa hakufika shuleni siku hiyo.
Eric naye alianza kutafutwa mchana na usiku, baada ya siku tatu mwili wake
uliokotwa ufukweni akiwa amevimba sana, huku macho yake yakiwa yameliwa
na samaki, hatizamiki. Ni habari iliyokuwa imeenea sana kwenye vyombo vya
habari. Iliwasikitisha watu wengi. Kisa chake kuwa alikufa akiwa anamtafuta
dada yake baharini ndicho kilichowaumiza wengi. Watu kutoka sehemu mbali mbali
walifurika kanisani siku ya kuaga mwili wake, Eric alizikwa nyuma ya nyumba ya
Mzee Mwasha. Ulikuwa ni wakati wa majonzi sana kwa familia hiyo.
********************************************
Elvin alikuwa kwenye wakati mgumu sana kuliko mtu yeyote
kati yao. Hakuwa akilala usiku wala mchana. Ilikuwa ni miezi 19 iliyojaa
hekaheka na simanzi kubwa sana kwa Elvin, hali yake haikuwa nzuri hata kidogo.
Mwishowe kaka zake wakaamua ahame kabisa pale Dar na kwenda kuishi na kaka yake
Eno nchini Dubai. Eno alimpeleka Elvin kwa washauri mbalimbali kuongea naye.
Baada ya kama miezi mitano ya matibabu na kuongea na wataalamu yaani kufanyiwa ‘counseling’, ndipo angalau Elvin alirudi kwenye hali yake ya kawaida.
Akarudi nchini akionekana angalau anaweza kufanya kitu kingine kikaeleweka.
Hapo ilikuwa ni baada ya kama miaka miwili tokea kupotea kwa Bella. Elvin
alirudi kazini kama kawaida. Mambo mengi yalikuwa yamebadilika lakini alifurahi
kukuta baadhi ya sura alizokuwa akizifahamu.
“Revange/Kisasi.”
Elvin alirudia maisha yake ya kawaida, asijue mkasa mkubwa
uliokuwa ukimsubiri. Bila wao wawili kujua, mahusiano yao, na mahusiano
waliyokuwa nayo kabla ya wao wawili, yalitengeneza adui wasiojua kusamehe. Na
wote waliapa kutopumzika mpaka walipe kisasi. Swali la kifo cha Bella kilikuwa
kipi, kama alitekwa au kufia majini likiwa halijajibiwa, njama kubwa sana za
kuangamiza familia ya Mwasha wakihesabiwa kama wasaliti katika jamii zilikuwa
zikiwasubiria pia. Zilipangwa njama nyingi sana kuumiza familia hiyo waliyosema
wanajidai wacha Mungu na wenye umoja kumbe ni wasaliti wakubwa. Kila mmoja
kwenye familia ya Mwasha alikuwa na kosa lake lililowapa sababu tosha
yakulipizwa kisasi. Kuanzia Mwasha mwenyewe mpaka Elvin walikuwa na makosa
walioona ni lazima waangamize familia hiyo kabisa.
Walitafuta kila njia jinsi yakuwatesa kwanza ndipo
kuwamaliza, lakini walianza kukata tamaa. Kwanza walianza na Eli waliedhani ni
cha pombe wakidhani itakuwa rahisi sana kumwingilia yeye ili kumaliza familia
hiyo lakini walishindwa. JJ aliyekuwa ametengana na mkewe na yeye alibaki kulea
wanae, mama yake na kazi tu. Hakuonekana mahali popote na yeyote. Eno ndiye
alikuwa mbali sana na jamii tokea zamani. Kwanza hata kuongea kwa Eno ilikuwa
shida zaidi ya salamu au kucheka basi. Wengine walisema anadharau sana, lakini
alikuwa na haiba ya ukimya kupita hata Mwasha baba yao. Hakujulikana kama
anamsichana au ana matatizo. Aliporudi Elvin kutoka nchini Dubai, walifurahi
sana. Mipango ikaanza upyaa.
********************************************
Walimtafuta binti wa kazi za ndani waliyejua ametulia na
mwenye dhiki sana. Wakamuuliza kama anashida na pesa na anataka pesa ya haraka.
Yule binti alieleza matatizo ya kwao yote. Akaanza kupewa ahadi nyingi sana kwa
kuambiwa anapewa kazi. “Tutakupa
sehemu ya kuishi wewe na familia yako hapa mjini. Yaani tutaenda kuwachukua
wazazi wako kutoka kijijini na kuwaleta hapa mjini. Huna haja yakufanya kazi za
ndani tena, tutakuwa tunakulipa mshahara kila mwezi, kwa mwaka mzima. Lakini
ndani ya huo mwaka uwe umefanya kazi tutakayokuwa tumekupa.” “Kazi gani?” Yule binti akauliza. “Kwanza wewe ni bikra?” Yule binti alishtuka kidogo. “Sijawahi kuwa na mwanaume.”
Alijibu kwa aibu kidogo kwani walikuwa wamemzunguka na wote walionekana
wanataka matokeo mazuri na pesa sio tatizo. “Wewe
utatufaa.” Waliangaliana na kucheka.
“Jina lake nani tena?” Mwingine akauliza. “Happiness.” Akajibu. “Unakwenda kanisani?” “Ndiyo.”
“Sasa sisi tunataka mlokole.” “Mmmh! Sisi kwetu hatuamini hayo mambo, tena baba
yangu ndio kabisaa.” Yule
binti alisita. “Sasa mnataka
pesa au hamtaki?” “Tunataka. Tena mama anasumbuliwa na mgongo kweli! Alikujaga
hapa mjini akaambiwa anatakiwa upasuaji, lakini tulishindwa pesa.” “Basi atatibiwa buree. Kaongee nao,
waambie atatibiwa na watu wakanisani kama watakubali kubadili dini na tutawapa
nyumba yakuishi huku mjini.” “Sasa mbona kazi yenyewe hamniambii!” “Kwanza
tunataka kujua kama watakubali kuingia kwenye kanisa la walokole. Na wala sio
kwa muda mrefu. Ukijitahidi kufanya kazi yako kwa haraka, utakuwa huru kuishi
vile utakavyo, lakini wakati huo utakuwa umeshakuwa tajiri.” Yule binti alikunja uso na tabasamu
usoni.
“Ni kazi gani hiyo?” Happiness akauliza kwa shauku huku na wasiwasi kidogo. “Maana kama ni madawa ya kulevya,
hiyo sitaki.” “Nani amekwambia madawa ya kulevya wanafanya mabikra?” Walimuuliza kwa ukali kidogo
nakumfanya Happy atulie na kufikiria. Wakamtolea picha, Happiness akabaki
amekodolea macho ile picha. “Huyu ndio nani?” Aliuliza Happiness kwa sauti yake
nzuri ya upole. “Anaitwa
Elvin. Huyo ndiye atakupa utajiri wote.” Happiness
hakuwa ameelewa. “Sasa ni hivi
Happiness, kazi yako kubwa nikuhakikisha huyu kaka anakuoa.” Happiness alishtuka sana.
“Kaka mwenyewe yupo hivi, atanikubali mimi!?” “Huo
nimuonekano tu, usiogope. Sisi tutakuwa tunakufundisha kila kitu kutokana na
tabia zake, mpaka akuoe. Hiyo sauti yako, na ukiingia kwenye dini yao, utampata
tu. Tutakupa udhaifu wake, na nguvu yake ilipo ili isiwe shida kumwingia. Cha
kwanza rudi kijijini, ongea na familia yako. Waambie umepata watu ni walokole,
wapo tayari kuwasaidia. Kwanza kumtibu mama yako na kuwapa makazi hapa mjini,
lakini sharti lao, nikuwa wanaenda kanisani jumapili na katikati ya wiki.”
“Kwani huko kijijini wanafanya kazi gani?” Mwingine akamuuliza Happiness. “Wakulima.” “Basi waambie hapa
mjini kazi yao itakuwa ni kwenda kanisani tu, sisi tutawatunza kwa mwaka
mzima.” “Sasa na huo mwaka ukiisha?” Happiness
akauliza. “Ndipo inapokuja
jukumu lako la pili.” Happiness
alijiweka sawa, maana mpaka hapo hakuwa ametajiwa kitu kigumu sana
kitakachopingana na utajiri unao mjia.
“Huyo kijana tunayekuonyesha, kwao wanapesa. Tunataka zote
ziwe zako. Kikubwa na chamuhimu, ukazane uolewe naye, mengine yote, tuachie
sisi tutakutajirisha. Ila kwa masharti haya, uingie kwenye ndoa ukijua upo
kazini, sio mapenzi na utusikilize sisi kila tutakachokwambia. Usiwahi
kumwambia mtu yeyote juu ya huu mkutano wa leo, wala hutakiwi kutujua zaidi ya
hivi. Tutakupa simu na pesa za kuanza kujikimu. Ukirudi tu nyumbani leo,
ukaache kazi, urudi kwenu ukaanze kazi yakuwashawishi wazazi wako kuingia
kwenye ulokole.” Alitolewa
simu nzuri ya kisasa na kukabidhiwa pesa zilizomtoa macho Happiness.
“Unafikiri utaweza?” Akiwa amechanganyikiwa kwa kulala masikini na kuamka
tajiri, Happiness alikubali kila kitu. Hakuwahi kushika milioni moja tokea
anazaliwa tena hasa kipindi hiki kila mtanzania analia shida! Hata bosi wake
alishaacha kumlipa mshahara, akabaki akiishi pale akihofia kurudi
kijijini kwa ugumu wa maisha. Hata hivyo bosi mwenyewe alikuwa akimvumilia sana
Happiness. Alikuwa mchafu na mvivu sana. Alibaki amekodoa macho akiwa ameshika
simu yake na kitita cha pesa. “Hii
ndio namba utakayopiga siku mtakayokuwa mnahamia mjini na familia yako.” Happiness alifurahi sana, akarudi kwa
bosi wake, akaaga kuwa mama yake amezidiwa kijijini amepigiwa simu na baba
yake, nilazima aondoke asubuhi yake.
Happiness na wazazi wake waanza kazi rasmi
kwa ajili ya kuangamiza familia ya Mwasha.
Tofauti na alivyotarajia, hakutumia nguvu nyingi sana
kushawishi familia yake. Baada yakusikia mkewe atatibiwa bure, na wanahamia
mjini kuishi na binti yao aliyepata ajira itakayoweza kufanya waweze kuishi
bila kazi ila kwenda kanisani tu, walifungasha mizigo yao haraka sana, na
kurudi na Happiness mjini siku inayofuata. Walipewa nyumba ndogo ya uwani
katika nyumba hiyo ya wapangaji wengi, nakuambiwa matibabu ya mama yake
yataanza mara watakapoona wamechukua hatua ya pili. Kuanza kwenda kanisani na
kuaminisha kuwa wameokoka.
Hilo nalo halikuwa tatizo. Familia hiyo ilihamia kwenye
kanisa alilokuwa akiabudu Mzee Mwasha na familia yake. Nakuanza kuwa washirika
wa kweli pale. Happiness alikuwa binti wa kuigwa. Aljitoa kwa hali ya juu pale
kanisani. Alianza kufahamika na kila mtu huku akisifiwa ni binti mwenye juhudi.
Hakukosa kwenye usafi wa pale kanisani, siku za maombi hakukosekana, kwenye
mkesha pia alikuwepo yeye na mama yake kuanzia mkesha unaanza mpaka asubuhi.
Mama yake aliingia kwenye kundi la kina mama, na yeye kwenye kundi la vijana.
Happiness alijaliwa sauti ya upole na ndogo sana. Hakuna jinsi angeongea
ukachoka kumsikiliza.
Kwa kuwa Mama Mwasha alikuwa ndiye mwenyekiti wa kundi la
kina mama, alishazipata sifa za Happiness. Urafiki kati ya mama yake Happiness
na Mama Mwasha haukuchelewa. Happiness alimwambia mama yake ajitahidi sana kuwa
karibu na yule mama. Na kweli, alijisogeza mpaka mama Mwasha akamuweka karibu.
Waliongozana kwenye kutembelea wagonjwa mahospitalini na kuona watoto yatima.
Ukaribu ukazidi, hata alipokuwa akifanyiwa upasuaji katika kitengo cha MOI
katika hospitali ya Taifa Muhimbili, akidhaminiwa na adui za Mwasha, Mama
Mwasha ndiye aliyekuwa akimuuguza mama huyo kwa karibu sana. Alipika kila
chakula akimsaidia Happiness kumuuguza mama yake mpaka alipopona.
“Sasa umeona jinsi tulivyomsaidia mama
yako mpaka akapona? Kinachofuata ni kuhakikisha unaajiriwa kwenye kampuni yao
kina Mwasha.” Walimpigia simu Happiness usiku huo akiwa anajiandaa kwenda
kulala. “Kweli ni rahisi. Hawana shida. Sasa nitafanyaje mpaka niajiriwe?” Happiness akahoji. “Kwa kuwa umefanikiwa kumsogeza mama yako karibu sana na Mama Mwasha,
na hiyo familia wanamsikiliza sana mama yao, mwambie mama yako akuombee kazi.” Nalo hilo halikusumbua hata kidogo. Mama yake Happiness
alipomwambia Mama Mwasha uhitaji wa kazi, Happiness akaanza kazi mara moja
kwenye Kampuni ya Mwasha na ndipo sasa akaanza kuwa karibu na Elvin.
********************************************
Baada ya Mzee Mwasha kujiridhisha kuwa Elvin yupo sawa na
akili ipo kazini, alimwachia tena majukumu ya pale ofisini na yeye kubaki
mshauri tu. Ulikuwa wakati ambao maadui zao hawakutaka kuulazia damu. Walimfundisha
Happiness kufanya kila awezalo kuwa karibu na Elvin. Walimfundisha kumjali yeye
kama Elvin kwanza. Happiness akaingia kazini. Kumjali Elvin kwa karibu. Alihakikisa
Elvin anakula milo yote kila awapo kazini. Taratibu Mama Mwasha akaanza
kumkaribisha na nyumbani kwake, kufanya ukaribu zaidi. Urafiki kati ya familia
ya mama yake Happiness na Happiness ukanoga kwa mama Mwasha. Salamu za hapa na
pale kila siku, Happiness akiulizia ni aina gani ya vyakula vidogo vidogo
anapenda Elvin ili awe anampelekea kazini. Hilo likampendeza na kumvutia zaidi
mama Mwasha. Kwa kiziwanda wake tena! Mungu ampe nini kama sio Happiness? Hata
hivyo Happiness hakuwa na mapungufu makubwa yakumfanya mtu aliyekusudia kuoa
ashindwe kumuoa. Ubora uliongezeka kwa kuwa alikuwa mcha Mungu sana, mpole na
mnyenyekevu.
Ugumu aliokumbana nao na kuwambia adui za Mwasha anakaribia
kukata tamaa, ni Elvin mwenyewe. Alishakubalika kwa Mama Mwasha. Alimpenda sana
Happiness. Na Happiness akaanza kujiuza kwa upande wa Elvin. Kila alipokuwa
akiongea na mama Mwasha, hakuacha kumsifia Elvin kwa hili au lile. Utendaji
kazi wake ofisini, utulivu na nidhamu. Alionyesha wazi kuwa anampenda na
kumuheshimu Elvin. Kujalia ndio kulizi. Kila mama Mwasha alipotaka kujua
maendeleo ya mwanae hapo kazini, basi Happiness ndiye akawa mtu sahihi. Kwa
muda mfupi sana, Happiness akaweza kujaa kwenye maisha na upande mzuri wa mama
Mwasha. Katika vipimo vyake, Happiness alishampitisha.
Swala la elimu yake haikumsumbua kabisa Mama Mwasha,
alijiambia anachotaka ni mke mwema kama Happiness kwa mwanae Elvin. Akaanza
kusambaza kwa juhudi zote sifa za Happiness mpaka kwa Mzee Mwasha ili
kutengeneza njia rahisi pale kwake ili Happiness akubalike. Kanisani ndipo
walipoimba sifa zake zaidi mpaka wazee wakanisa walikuwa wakimtolea mfano
Happiness. Kuanzia mchungaji mpaka washirika wengine walimpenda na kumsifia,
lakini Elvin ndio alikuwa tatizo ni kama hakuwa akiona kitu. Japokuwa
alimuheshimu sana lakini hakuwahi kumfikiria upande wa mapenzi hata kidogo.
Kila alipojaribu kumsogelea, alimsimulia habari za marehemu Enabella na Eric.
Jinsi alivyokuwa mcheshi na mwingi wa upendo.
********************************************
Siku zilizidi kwenda lakini maongezi yao makubwa yalikuwa
ni Enabella tu. “Hata wewe
ungempenda tu Bella. Alikuwa ni binti mzuri sana. Mungu alimpendelea kila kitu
kizuri. Huwezi kuchoka kumtizama Bella. Iwe usiku au mchana, awe macho au
amelala, Bella alivutia kumwangalia. Alinifanya nicheke kila wakati. Hakuwa na
sifa za upole hata kidogo, alikuwa muongeaji sana, lakini wakati wote Bella
alipoongea mtu yeyote aliyekuwa karibu yake alijisikia vizuri. Hachoshi
kuangalia. Akicheka utatamani asiache. Sitakaa
nimsahau Bella.” “Pole sana Elvin.” “Na kinachoniumiza zaidi, amekufa nikiwa
nataka kumchumbia. Nilikuonyesha pete yake?” “Zaidi ya mara kumi.” Elvin alicheka kidogo.
“Ninatembea nayo hapa.” Akaitoa tena ile pete nakuivaa kwenye kidole chake kidogo.
“Tulikuwa tumekwenda mapumzikoni, hukohuko ndipo alipopotea Bella wangu.
Natamani ningeendelea na mipango yangu ya mwanzoni. Nilipanga siku aliyokuwa
amerudi kutoka nchini India ndiyo siku nilitaka nimuombe awe mke wangu, lakini
mama alinishauri nisubiri kwani alikuwa ni mjamzito na yeye mwenyewe hakuwa
akijua.” “Mimba ilikuwa ni yako!?” Happy
alishtuka kidogo. “Hapana.
Hapana kabisa. Ni habari ndefu. Lakini ilikuwa sio yangu.” “Kwa hiyo ulikuwa
tayari kumuoa hivyo hivyo?” “Bella alikuwa ni mke wangu, hilo halikuwa na
ubishi. Umeshawahi kujua moyoni na kujua, halafu ukaelewa kwamba huyu mtu ni
wako? Hata kama mazingira yote yanakataa, lakini wewe unajua huyu ni mtu wangu
tu!” “Ndiyo.” Happy akajibu. “Basi ndivyo ilivyokuwa kwa Bella.
Nilijua na ninajua Bella angekuwa mke wangu hata iweje.” Elvin aliuliza bila kutarajia jibu la ‘ndiyo’ kutoka kwa Happiness.
Alitulia kidogo na kukumbuka jibu la Happiness. “Hivi ulijibu ndiyo?” Happy akacheka. “Na mimi nimepitia huko.” “Sasa
iweje mpaka leo hujaolewa naye?” Elvin
aliuliza kwa mshangao mkubwa sana. “Kwa
kuwa mwenzangu hakuwahi kuniangalia mimi kama mke. Hakuwahi kunipenda
kimapenzi.” “Lazima huyo
mtu anatatizo. Wewe ni msichana mzuri sana Happiness, umetulia na unaweza
kumfanya mwanaume yeyote awe na furaha.” Happy
alicheka kwa huzuni kidogo. “Sio
kwake. Nimejitahidi kwa kila njia lakini hakuwahi kunipenda.” “Unajua
Happiness, wapo watu wengine wanahitaji kufunguliwa macho. Kwa nini
usimwambie?” “Unafikiri ni sawa kwa mwanamke kumfuata mwanaume?” “Mimi sioni
tatizo, lakini sijui wengine.” “Kuna hofu ya kukataliwa pia.” “Mimi nakushauri
uende tu Happiness. Hakuna jibu latofauti utakalopewa mbali ya ndiyo au hapana.
Na itakurahisishia kuendelea na maisha yako mengine, kuliko kuendelea kumsubiri
mtu ambaye pengine na yeye anakupenda sana, ila ameshindwa au anachelewa
kuchukua hatua, au hana mpango kabisa na wewe. Nakushauri chukua hatua Happiness.
Wewe ni dada mzuri sana, una haki zote zakuwa kwenye nyumba yako, na mume na
watoto wenu wakifaidi upendo wako. Nakushauri usichelewe.” Happiness alitabasamu kisha
akanyamaza.
Ilikuwa ni siku ya jumapili baada ya ibada, Mama Mwasha
alimkaribisha Happiness kwa ajili ya chakula cha mchana pale nyumbani kwao. Na
baada ya kula, Mama Mwasha alitoka na mumewe, kama kuwapa nafasi ya mazungumzo
pale pale nyumbani kwao. Nia yake ni kuhakikisha Elvin anafunguka macho na
kuweza kumpenda Happiness. Na kwa kuwa alishajua jinsi Happiness anavyompenda
mwanae, akamshauri asipoteze muda. Atumie muda huo kumwambia Elvin ukweli.
Lakini ni kama alimuachia nafasi Elvin yakumtangaza Enabella. Alimsimulia kwa
kurudia rudia mpaka Happiness akaishiwa nguvu.
Ilipofika jioni Mzee Mwasha na mkewe walirudi nyumbani na
Mama Mwasha akaomba yeye ndio amrudishe Happiness nyumbani kwao. Lakini lengo
ilikuwa ni kupata naye muda wa maongezi wakiwa njiani. “Vipi umeweza
kumwambia chochote?” “Sijui kama nimuoji wa leo wala kesho mama. Bado
anakumbukumbu za Enabella, hawezi kuongea chochote isipokuwa Bella. Sio kazini,
si nyumbani. Anarudia habari za Bella tu. Nimejaribu mama, lakini nimeshindwa.” Mama Mwasha alifikiria kidogo. “Ngoja nikwambie ukweli Happiness.
Enabella ni msichana aliyeacha pengo ambalo hakuna mwanadamu anayeweza kuliziba
mioyoni mwetu wote, hata wewe usijaribu kuziba pengo la Bella. Hutaweza. Kuwa
wewe kama wewe. Bella ameshaondoka, na Elvin ni lazima aoe, na jinsi
ninavyokuona, wewe ndiye msichana utakaye mfaa Elvin.” “Sidhani mama. Naona
sina nafasi kwenye moyo wa Elvin kabisa.” Happiness
alishafika mwisho.
“Labda kama uliyoniambia tokea mwanzoni hayakuwa na ukweli.
Upendo una nguvu sana Happiness.” “Sasa nitafanyaje mama?” “Kama uliweza
kunifuata mimi na kuniambia, kwa nini usimwambie na Elvin mwenyewe? Hapatakuwa
na jibu la tofauti zaidi ya ndiyo au hapana. Na itakusaidia wewe kuendelea na
maisha mengine Mungu aliyokukusudia. Ni kweli Bella na Elvin walipendana sana,
lakini haitamzuia Elvin kuendelea na maisha mengine. Sijui umeelewa?” “Nimeelewa mama.” Bila kujijua, Mama
Mwasha aliendelea kumpa moyo Happiness adui mkubwa sana katika maisha yao, na
alimpa mbinu nyingi za kuweza kufanikisha lengo la kuolewa na mwanae. Njia
nzima aliongea naye kwa hekima sana akimtia moyo nakumuomba asikate tamaa mpaka
alipomfikisha nyumbani kwa wazazi wake, akaongea habari za kawaida sana na
wazazi wa Happiness ambao walikuwa wameshakuwa karibu sana, mwishowe akaaga na
kuondoka.
********************************************
Kama kawaida yake, ilikuwa lazima kutoa ripoti ya maendeleo
ya kazi aliyopewa, lasivyo aliambiwa akishindwa watafukuzwa pale kwenye ile
nyumba na kurudishwa kijijini. Happiness alitoka nje ili kupiga simu baada
yakuhakikisha ndugu zake na wapangaji wote wamelala. Hakuwa akijua jina hata la
mmoja wao lakini alipewa namba ambayo aliambiwa huyo mtu ndiye atakayeendelea
kuwa akimpa maelekezo. Alieleza kila kitu na ushauri alioshauriwa na mama
Mwasha na Elvin mwenyewe. “Lakini labda mnipe njia nyingine jamani.
Nimeshindwa kwa Elvin.” Happiness
alijitetea. “Labda kama useme umeshindwa kuishi mjini,
na unataka kurudia hali yako ya umasikini. Na itabidi utulipe pesa yetu ya kodi
tuliyolipia hiyo nyumba mnayoishi sasa hivi na uturudishie pesa zetu zote. Na
itabidi uiche ile kazi kwa Mwasha.” “Hee! Si ni kazi aliyonitafutia mama
yangu!?” “Usijisahau kabisa Happiness. Sisi ndio tunakupa ramani ya kipi
ufanye. Unatembea juu ya ramani yetu. Mbona hukutoka kule ulikokuwa ukifanya
kazi za ndani na kwenda kuajiriwa ofisini?” Happiness
alipooza gafla. “Usijisahau na kuweka kiburi. Tutayafanya
maisha yako yawe magumu sana hapa mjini. Kina Mwasha wataujua ukweli wote juu
yenu na mtafukuzwa kila mahali. Si kanisani, si hapo kwenye hiyo kazi. Wale
watu wanaroho mbaya sana na hawataki wasaliti. Wakijua kuwa ulikuwa na hila
tokea mwanzo, na si kweli upo kama hivyo ulivyojionyesha kwao, utajuta. Utakuwa
umejitengenezea adui wawili. Wao na sisi. Na kundi letu huwa hatukubali
kushindwa.” Wakaendelea kumtisha.
“Nasisitiza, ili usisahau, upo kwenye
maisha yao sasa hivi kwa sababu sisi tumekuvalisha hilo vazi la utakatifu na
tumekuwezesha kifedha. Wale watu sio wakukaribisha watu kwenye maisha yao
hovyohovyo. Na ninakuahakikishia Happiness, tukikuacha wewe hata siku moja tu,
watakugundua kuwa sio mlokole na wewe ni mjinga mjinga tu wa kijijini.” Happiness kimya. “Na tunakupunguzia muda. Naona unaanza kulewa pesa yetu. Tumekuvalisha
na kukulisha vizuri wewe na familia yako hapa mjini, unaanza kujifananisha na
watu wa hadhi hiyo. Sasa ndani ya miezi 6, uwe umeolewa na Elvin. Kitakachopata
familia yako, usimlaumu mtu.” Simu ikakatwa
na kumuacha Happiness akishangaa. Hapakuwa na kubembelezwa tena, ni vitisho.
********************************************
Lilikuwa ni jaribu na mtihani mkubwa sana aliokuwa amepewa Happiness
na hao Waajiri wake,
kwani Elvin hakuacha kurudia habari za Bella bila kuchoka. Kila wakati kazi
zilipokuwa zikisuasua, watu wakiwa hawafanyi kazi vizuri, alimkumbuka Bella. “Bwana Bella alikuwa mchapakazi
yule mtoto sio mchezo! Alikuwa analala hapa ofisini, kuhakikisha kazi
zimekamilika. Halafu umeona hii biashara ndogo inayotuingizia sana faida kuliko
hata hii kubwa?” Elvin
aliuliza. “Ni wazo la Bella.
Alikuwa na akili yakufikiria, sijawahi ona. Na nijasiri kama simba. Haogopi
kujaribu kitu chochote. Na yeye ndiye aliyenifundisha msemo wa ‘Hakuna haja yakuogopa kusogelea mlango wowote ule. Kwani
matokeo yake ni mawili tu, Kufunguka au kutokufunguka’.Bella sio mchezo.” Happy alisikiliza na kuamua kuondoka ofisini kwa Elvin
kwani alikuwa amemletea chai ya saa kumi. “Asante
sana Happy.” Happy
alitabasamu. “Karibu.” Akatoka.
Siku zilizidi kwenda Happiness akitafuta jinsi yakumwambia
Elvin lakini alishindwa. Waajiri
wake walimwambia Happiness, kadiri anavyochelewa ndivyo anavyompa nafasi Elvin
yakumfikiria msichana mwingine mbali na yeye. Walimwambia anaweza kushuhudia
Elvin akioa mwanamke mwingine, kama yeye akishindwa kumwambia ukweli na hapo
ndipo atakapoona hasira zao kwa kukubali kazi ambayo anashindwa kufanya. “Nimefanya kila mlichotaka. Kama Elvin mwenyewe hataki mimi nifanyaje?
Kwanza nimechoka kumbembeleza na mimi nina mpenzi wangu nataka nimlete mjini
tufunge ndoa. Msinibabaishe. Kama ni nyumba yenu na pesa mnayonipa, sina shida
navyo tena. Hamkunikuta nalala njaa au nalala nje.” Happiness na yeye akakata simu.
Onyo
kwa Happiness.
Happiness akaamua aachane kabisa na wale watu. Akaacha
kupokea simu zao kabisa. Zilipita siku mbili tu, siku ya tatu akiwa anatoka
kazini alipigiwa simu na wazazi wake kuwa kaka yake amekimbizwa hospitalini
kwani amekamatwa na vibaka wamempiga sana na ameumia. Kaka huyo alikuwa anatoka
kwenye shuguli zake wakati anakaribia na nyumbani kwao, lilimsogelea gari,
wakashuka vijana asiowafahamu, wakiwa wameficha nyuso zao, walimpiga sana, na
kumuacha akiwa anavuja damu. Waliondoka na gari yao, lakini alishindwa hata
kusoma namba za gari kwa maumivu na giza lilikuwa limeanza kuingia.
Happiness alikuwa dada mkubwa nyumbani kwao, baada ya kaka
yake waliyekuwa wamepishana kama mwaka tu, na yeye hakuwa amesoma kabisa,
aliishi kijijini na wazazi wake pamoja na wadogo zao wawili wakike na wakiume,
mpaka walipokuja mjini, huyo kaka mtu alianza shuguli ndogo ndogo kama kuongeza
kipato pale nyumbani.
Akiwa amepigwa sana bila hata kupokonywa kitu chochote,
ndipo alipowapigia simu nyumbani kwao wamfuate hapo alipokuwa kwani alisema
hawezi hata kutembea. Wazazi wake walimfuata na kumkimbiza hospitalini. Mtaa
mzima ulijua juu ya sakata hilo na kuwaogopesha sana. Cha ajabu ni kule
kutoibiwa kitu chochote. Walijua wazi ni mambo ya vijana, kulipizana kisasi.
Labda alitembea na mwanamke wa mtu.
Ilibidi Happiness abadilishe daladala. Kutoka ile aliyokuwa
amepanda wanzoni yakumfikisha nyumbani, akashuka na kupanda yakumpeleka
hospitalini. Kabla hajaonana na ndugu zake hospitalini hapo, simu yake ikaingia
ujumbe.
“Hayo ni matokeo ya kusahau fadhila. Ulikubali
kazi, lazima ulete matokeo yatakayo turidhisha. Ukitoka hospitalini upige simu
lasivyo kitakachotokea tena, hutakaa ukasahau.”
Macho yalimtoka Happiness akaamua kupiga simu pale pale na
kuomba msamaha. “Sasa
kinachofuata ni wewe kuongea na Elvin kama mama yake alivyokushauri. Na tumia
mbinu zote za kike kuhakikisha mnafunga ndoa. Unasikia Happiness?” “Ndiyo.” “Kumbuka
na simu uliyoshika sasa hivi au unayotumia, pia ni ya kwetu. Usisahau matumizi
yake, ukaishia kuonyesha ufahari tu. Tunauwezo wakufika popote na kwa yeyote.
Huna utakapotushitaki tusijue na kukufuata wewe na familia yako.” Simu ikakatwa.
Happiness alibaki akifuta machozi huku hofu imemjaa.
Pale pale akaamua kumtumia ujumbe Elvin siku hiyo ya ijumaa
akiwa hata bado hajaonana na kaka yake aliyeambiwa ni mgonjwa sana. ‘Kama utapata nafasi, naomba tuonane kesho
tafadhali sana Elvin.’ Ule ujumbe
ulionekana umefika lakini haukujibiwa usiku kucha. Happiness alishindwa hata
kuongea na mtu yeyote pale hospitalini, tumbo lilikuwa likimuuma sana kwa
wasiwasi.
‘Nilijua tu hawezi kukubali. Nitafanyaje?’ Happiness aliendelea kuwaza. Baada ya kaka yake kuangaliwa
na kuonekana ni madonda tu ya nje tu na hakuna popote kwenye madhara zaidi,
aliruhusiwa usiku huo, wakarudi nyumbani. Wengine walilala lakini Happiness
alibaki akisubiria majibu kutoka kwa Elvin. Alijuta na kuendelea kujuta.
Palipambazuka, ikawa asubuhi mpaka ilipofika mchana hapakuwa na jibu lolote.
Happiness alijifungia chumbani kwake akilia sana. Mama yake na ndugu zake
walimuhurumia sana Happiness, lakini hawakuwa na jinsi ya kumsaidia kwani wao
walijua upande mmoja tu wa stori, wakidhani ni mapenzi pekee yanayomliza, kumbe
alishaanza kutishiwa maisha. Aliona madonda ya kaka yake, akajua hao watu
hawatashindwa kuua.
‘Labda kwa kuwa mimi sio mweupe. Hata umbile lenyewe
halivutii. Elvin amenidharau sana. Ameshindwa hata kunipenda hata kidogo
jamani! Nimejitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu. Basi hata angerudisha ujumbe
wakuniambia hataweza kukutana kuliko dharau aliyonifanyia! Hakika atakuja
kulipa matatizo aliyomsababishia kaka yangu.’ Happiness alianza kujenga chuki kwa Elvin. Alikuwa akiwaza
huku akilia kwa hofu.
Kila wakati alihakikisha simu yake ipo na chaji yakutosha
na haijazimika ili Waajiri wake wakimtafuta wampate na Elvin pia
asimkose kama ataamua kumtafuta. Alisubiri simu hiyo ya Elvin huku akijaribu
kuwatuliza Waajiri wake, kuwa lazima atafanikisha swala
la Elvin, wasiwe na wasiwasi, anaomba muda zaidi. ‘Umebakisha siku chache sana Happiness ili tufikie muafaka na wewe.
Mnaonekana mkiendelea kunufaika na maisha tunayowapa bila sisi wenyewe kupata
tunachogaramia. Baada ya muda mfupi kuanzia sasa, kama hakutakuwa na matokeo
tunayotarajia, tutakuja kuwatoa hapo kama mbwa, na kumrudisha mama yako kuwa
kiwete kabisa. Tutafungua huo mshono wa upasuaji aliofanyiwa kwa garama zetu,
tutatoa hivyo vyuma mgongoni bila hata ganzi, na wewe utapewa adhabu yako.’ Ujumbe huo ulizidi kumtisha Happiness.
Hata maji yalishindwa kupita kooni kwa Happiness. Alishinda chumbani kwake
akilia tu.
********************************************
Mpaka ilipofika jioni ndipo alipoona Elvin anampigia simu.
Happy aliruka kutoka pale alipokuwa amelala akainyakuwa simu yake. “Hallow!” Happy alianza. “Samahani sana Happiness, niliacha simu kazini tokea jana. Yaani hapa
ndio nimeifuata na kukuta ujumbe wako. Sijui nimechelewa au bado tunaweza
kukutana tu? Najua muda umekwenda sana, naweza kukufuata hata hapo nyumbani.” Happiness hakuamini masikio yake. “Kama haitakuwa usumbufu kwako.” “Hamna usumbufu kabisa. Basi nitakuwepo
hapo nyumbani muda si mrefu.” “Karibu sana.” Hapakuwa na jinsi Happiness angeeleza furaha yake mtu
mwingine akaelewa. Alikuwa akiruka ruka huku machozi yakimtoka kwa furaha.
Alijiambia atatumia huo muda ipasavyo.
Elvin alifika nyumbani kwao, akiwa na wasiwasi sana na
muda, asijue furaha waliyonayo hata wazazi wake Happiness. Hata wazazi wa Happy
walimpenda sana Elvin, wakatamani kama angalau wangekuwa na uwezo kidogo sio
fukara vile, labda Elvin angempenda mtoto wao, bila kujua mipango inayoendelea.
Na wale Waajiri wa
Happiness walihakikisha hawana pesa nyingi sana ili kumtia shauku Happiness
yakutengeneza pesa zaidi. Kwa hiyo alipoajiriwa kwenye ofisi ya Mwasha,
wakaacha kumlipa na kumsisitiza ajitahidi kuolewa nakuanza kufaidi pesa za
Mwasha yeye mwenyewe kama mke wa Elvin mpaka watakapompa ramani nyingine.
Elvin alikuwa ni kijana mwenye tabia ya kiugwana. “Samahanini sana najua nimekuja
muda mbaya, lakini nahitaji kuongea na Happiness.” “Hamna shida kabisa
mwanangu. Msubiri kidogo, nikamwite.” Alimkuta
Mama na baba yake Happiness barazani. Mama yake, alisimama na kuingia ndani.
Aligonga kwa muda ndipo Happiness alipofungua. Alishtuka sana kuona uso wa
mtoto wake. Alikuwa amevimba sana macho na nimekundu kwa kulia. Mama yake
alibaki akimwangalia kwa kumuhurumia sana mwanae, kwani alikuwa amejifungia
humo chumbani siku nzima bila kutoka. Hakuwa amekula kitu chochote siku nzima. “Elvin amekuja, anakuulizia wewe.” Happiness alitabasamu, wazi alionekana
ni habari alizokuwa akizisubiria kwa muda mrefu. “Nakuja sasa hivi.” Happiness alijibu kwa upole, mama
yake akataka kuondoka. “Mama!” Happiness alimwita, mama yake
akageuka. “Samahani
niliposhindwa kukufungulia mlango asubuhi na nikawa mkali sana kwa kila mtu.
Nilikuwa kwenye wakati mgumu sana.” “Pole sana Happy. Jitahidi uwahi kutoka
huko chumbani, usimuweke sana mwenzio.” “Sitakawia.” Happiness alijaribu kunawa uso mara
kadhaa ili kuwa sawa, lakini bado macho yalikuwa yamevimba sana.
Akaamua kutoka vilevile. Elvin alishtuka sana alipomuona,
akasimama. “Vipi Happiness?
Mzima?” Happy alijaribu kutoa
tabasamu la kinyonge lakini Elvin alijua kuna kitu hakipo sawa. “Tunaweza kutoka kidogo
tukazungumze?” Elvin aliuliza
kiustarabu sana. Happiness aliitikia kwa kichwa huku machozi yakimtoka. “Najua muda umekwenda wazazi wangu,
lakini naomba nitoke na Happiness kidogo, sitachelewa kumrudisha.” Elvin aliomba ruhusa. “Bila shaka.” Baba yake akajibu. “Twende Happy.” Elvin aliongoza njia mpaka kwenye gari
yake, akamfungulia mlango, Happy alipopanda akaufunga mlango wa gari.
Elvin na Happiness.
“Umeshakula?” Happy
alitingisha kichwa kukataa. “Basi
twende tukatafute mahali tule wakati tunaongea.” Elvin aliondoa gari. “Vipi lakini? Mbona unalia?” Kama aliyekuwa ameambiwa aanze kulia.
Happiness aliendelea kulia kwa kwikwi sana, kitu kilichomtia wasiwasi Elvin.
Alishakaa na wasichana waongeaji, Irene na Bella, lakini Happiness alikuwa
msichana mkimya sana. Elvin alisimamisha gari nje ya sehemu aliyotaka wakale
akamgeukia Happiness. “Niambie
nini kimekuudhi Happiness! Ni kazini?” “Nilijua
umepuuzia ujumbe wangu Elvin.” Elvin
alijisikia vibaya sana.
“Sijui nini kilitokea jana, nikaacha simu kazini. Na sina
matumizi sana na hii simu zaidi ya mambo ya kikazi, kwa hiyo nilipofika
nyumbani nikagundua nimeiacha ofisini, sikuwa na wasiwasi kabisa, nikijua
hakuna wakunitafuta siku hizi za jumamosi na jumapili. Nimelala karibia siku
nzima ya leo, yaani nimeamka ndio nikaamua kuifuata ofisini, ndipo nikakutana
na ujumbe wako, na hapohapo nikakupigia. Naomba unisamehe sana. Sina sababu ya
kukupuuza Happiness. Unajua ninavyokuheshimu. Naomba uniwie radhi.” Happiness alitulia kidogo. “Sio
kwamba ni kosa, ila mimi mwenyewe nilijidharau sana, kuona nimekutumia ujumbe
halafu hukujibu.” “Daah! Huna sababu
yakujidharau Happiness, ni bahati mbaya tu imetokea. Twende tukale kwanza,
ndipo tuzungumze.” Walishuka kwenye gari wakaingia kwenye huo mgahawa na kila
mmoja aliagiza chakula alichokipenda.
Haikuwa kawaida ya Happiness kwenda kwenye migahawa ya
maana kiasi hicho, kutokana na uwezo wake. Lakini sio Elvin mtoto aliyezaliwa
kwenye maendeleo na kuzungukwa na watoto wa matajiri wa pale mjini. Akaja
kukutana na Bella mtoto wa viwango vya juu. Kwa hiyo kimaisha Elvin na
Happiness hawakuwa sawa hata kidogo. Hata nyumba waliyokuwa wamepangiwa ilikuwa
ni nyumba ya kawaida sana pale jijini.
“Bella alikuwa akipenda sana chakula cha hapa.” Elvin
alivunja ukimywa. “Tulikuwa
tukipenda sana kuja naye hapa. Tulikuwa tukikaa au niseme kujificha kona ile
palee, kwa kuwa Bella alikuwa anaweza kukufanya ukacheka mpaka ukaingia aibu.
Kwa hiyo kila tulipokuwa tukija hapa, tulikuwa tunajificha pale, ili afanye
fujo zake zote na mtu asituone.” Elvin
alikuwa akiongea na tabasamu kubwa huku akivuta hisia zilizoonekana
kumfurahisha sana moyoni. Alishangaa kumuona Happiness siku hiyo amenyamaza
kabisa bila kuchangia neno lolote. Elvin akaamua anyamaze kidogo lakini
akakumbuka kitu kingine. “Unajua Bella…” “Samahani Elvin.” Happiness alimkatiza Elvin. “Naomba na mimi unipe muda wako
hata dakika tano tu, unisikilize kidogo.” Elvin
alitulia kidogo na kumwangalia Hapiness kwa makini. “Namaanisha kunisikiliza na mimi,
na kunipa dakika hata moja ya Bella kati ya muda wote unao mpa hapa duniani.” Elvin alibadilika sana usoni.
“Najua unampenda sana Bella, na hakuna mwanamke anayeweza
kuchukua nafasi yake kwenye moyo wako, lakini naomba unipe nafasi na mimi.
Japo kidogo tu Elvin. Nimekuwa nikikusubiri kwa muda mrefu sana. Tokea
nilipokuona kanisani, nilibaki kumwambia Mungu yeye anayejua ni kiasi gani
nakupenda, akutunze kwa ajili yangu. Nimemshukuru Mungu kunipa kazi kwenye
kampuni yenu, nikaona tupo karibu, lakini kila nilipojisogeza kwako ili nipate
nafasi angalau machoni kwako tu, imeshindikana. Imenilazimu nikwambie tu ili
ujue ni kiasi gani nakupenda na ninakusubiri ili siku moja uje kuwa mume
wangu.” Elvin alikuwa kama
amechomwa sindano ya ganzi ya mwili mzima.
Ni kama ulimwengu ulisimama kwa muda, akaanza kukumbuka
maongezi yake na Happy juu ya mwanaume anayempenda. Akili yake ikafunguliwa
gafla akaanza kuona juhudi alizokuwa akizifanya kwake. Alimuhurumia sana, kwani
yeye hakuwa hata na wazo la mahusiano ya kimapenzi kwake.
“Nakupenda Elvin.” Happiness alirudia, Elvin alikuwa kama ameshtuliwa kutoka
usingizini. “Kwanza nikuombe
radhi Happiness. Sikuwahi hata mara moja kukupuuza au niseme kukudharau. Akili
yangu haikuwahi hata kukufikiria upande wa mapenzi. Na sio kwa sababu nyingine
yeyote, lakini nafikiri ni heshima niliyokuwa nayo kwako. Wakati wote nimekuona
kama dada yangu, tena mwenye tabia nzuri sana. Hakuna msichana aliyeteka akili
zangu kama Bella. Amefanikiwa kuingia katika kila kiungo changu. Siwezi kulala
au haiwezi kupita hata dakika moja bila kumfikiria Bella. Ndio maana imekuwa ngumu sana hata kurudiana na Irene.
Irene amejirudi sana, amekuwa msichana mzuri kitabia, lakini hata aliponiomba
turudiane nilimkatalia kabisa kwa kuwa sikutaka kuja kumuumiza baadaye. Bado
nahitaji muda kuweza kuyafuta maisha niliyoishi na Bella. Yalikuwa ni mafupi
lakini yameathiri maisha yangu kuliko nitakavyoweza kuongea. Namuuliza Mungu, ni kwa nini
alinikutanisha na Bella halafu akamchukua! Ni swali linalonisumbua sana.
Nimekaa na wewe Happiness, wewe ni msichana mzuri sana, unahitaji mwanaume
atakayekupenda na kukuenzi, sio mimi hata kidogo.” Elvin aliendelea.
“Nakuhakikishia mimi sipo kwenye nafasi ya kuwa mume bora
kwa sasa hivi, kwa msichana yeyote yule hata awaje isipokuwa Bella.” “Kwa hiyo hata akirudi leo utamuoa?” “Bila kupoteza hata
siku moja mbele. Nitampokea kwa mikono miwili na kumkimbiza kanisani nikafunge
naye ndoa haraka sana. Ndivyo hali yangu ilivyo mbaya kwa sasa. Sijui
unanielewa? Natamani kama ningekuwa hata na nafasi kidogo tu moyoni mwangu
Happiness, ningekwambia sawa, labda ukinipa muda nitajitahidi kuwa mume
anayefaa kwenye maisha yako. Lakini najihisi kama nimeoa, nina mke tayari
ambaye ni Enabella. Kuwa na msichana mwingine au hata kufikiria kuoa ni kama
namuolea Bella mke wa pili. Nipo kwenye kifungo kigumu sana Happiness. Sitaki
uingie huko. Sitafurahi kuja kukuona ukiamka pembeni yangu ukiwa huna furaha na
mimi ndio nimeku sababisha. Sitaruhusu hilo litokee.” Happiness
aliishiwa nguvu. Akatamani aondoke muda huo huo lakini akakumbuka uhai wa ndugu
zake unamtegemea yeye na juhudi zake siku hiyo. Akaamua azidi kupambana.
“Nakupenda sana Elvin, nakuomba nipe nafasi. Naweza nisiwe
kama Bella, lakini nakuahidi nitakuwa na wewe katika kila hali utakayokuwa ukipitia. Nipe nafasi.
Nikishindwa, mimi mwenyewe nitaondoka.” Elvin alibaki akimwangalia Happiness jinsi anavyoongea kwa
hisia kali. Elvin alivuta pumzi ndefu, kisha akaweka mikono kichwani. “Naomba nipe muda nifikirie
Happiness. Tafadhali. Sikuwa na wazo la kuja kuoa kabisa. Yaani leo ni kama
unataka kuanzisha safari mpya kabisa katika maisha yangu ambayo sikuwa
nimeitarajia hata kidogo. Tafadhali nipe muda.” “Nitaendelea kukusubiri Elvin,
huku nikikuombea. Nakuahidi kukupenda na kukutunza daima. Nitakuwa na wewe
katika kipindi hichi kigumu unachopitia. Naomba uniamini nakupenda.” Elvin alibaki akimwangalia Happiness
na mikono yake kichwani. Gafla alisimama akaanza kuzunguka pale mgahawani,
Happiness akimtizama.
Baada ya kuzunguka
kidogo, akamuona anaelekea chooni. Akatoka akionyesha wazi aliosha uso.
Hakurudi hata kukaa tena. Akaweka pesa chini ya glasi yake ya juisi iliyokuwa
imefika nusu, akamgeukia Happiness. “Samahani
Happiness, tunaweza kuondoka?” Wazi
alionekana alikuwa kwenye wakati mgumu sana. Ni kama aliyepigiwa kengele na
kutakiwa aamke, na yeye hakuwa tayari kuamka kabisa.
Elvin alikuwa ni kijana aliyeishi maneno yake. Mwaminifu
sana na mcha Mungu. Hali ya kuwa na mwanamke mwingine ni kama usaliti mkubwa
sana kwa Bella ambaye ameshakufa muda mrefu sana uliopita, lakini yeye alikuwa
na ndoa na Bella ya milele. Alimrudisha Happiness mpaka nyumbani kwao, njia
nzima hakuongea kitu. Happy alimuona jinsi alivyoshtuka, ni kama aliyepewa
habari za msiba. Happy aliona azidi kukazia maneno ili hata wakiachana,
akamfikirie na yeye pia. Kabla ya kushuka Happy aliamua aongee naye kidogo. “Elvin, sijakwambia unioe kesho
wala kesho kutwa. Nilitaka ujue na mimi nipo, nakupenda kwa dhati na
ninakusubiri uje kuwa mume wangu. Namaanisha kila ninalo kwambia. Nakupenda
sana na nina endelea kukusubiri.” Happy
aliongea kwa upole kama kawaida yake.
“Hiyo siku utakayokuwa tayari kuoa, nilitaka unifikirie
mimi.” Elvin alibaki akimwangalia. Alipoona kimya, Happy aliamua
kushuka kwenye gari. Elvin alimwita, na yeye akashuka. “Samahani sana Happiness. Nashukuru
kuniambia, wala hujakosea kabisa. Lakini…” Elvin alishusha pumzi kwa nguvu sana
na kuanza kuangalia kulia na kushoto kana kwamba ulimwengu wote unamuangukia
yeye. “Daah! Sikutegemea
kabisa. Nipo kwenye hali mbaya sana sasa hivi. Zimeibuka hisia ambazo
nilijitahidi kuzizika kwa muda mrefu sana. Naomba nikapumzike.” “Samahani sana Elvin, sikukusudia
kukuumiza.” “Hapana na wala hujaniumiza. Nahisi mimi nina matatizo Hapiness.
Wewe umefanya jambo zuri sana, na ninakupongeza. Asante sana kwa upendo wako,
lakini…. Daah! Hapana Happy nitakusumbua sana. Hutafurahia maisha ukiwa na
mimi. Sitaki kuja kukuumiza. Nataka niendelee kukuona ukiwa na furaha wakati
wote. Ndani yangu sipo kama hivi unavyoniona nje au sipo kama watu
wanavyonifikiria nipo. Ni kama nilikufa na Bella. Nipo hovyo kweli! Natamani
kama tungekutana kwenye mazingira tofauti, kabla ya Bella, au kabla ya hivi
nilivyo sasa. Nakuthamini sana Happy, sitaki kukuumiza. Hapana Happiness.
Sitaweza kabisa kuwa na wewe au mwanamke mwingine. Samahani sana.” Elvin aliingia ndani, akashukuru
wazazi wa Happiness akaondoka.
********************************************
Njia nzima machozi yalikuwa yakimtoka Elvin. ‘Huu
utakuwa usaliti kwa Bella kabisa.’ Elvin alirudi moja kwa moja mpaka nyumbani kwao,
alifunguliwa geti na mlinzi, akaegesha gari yake sehemu yake, akabaki amekaa
ndani ya gari huku ameweka mikono kichwani. ‘Kwa nini ulimchukua Bella?’ Elvin aliendelea kumuuliza Mungu wake. ‘Kwa nini ulimleta kwangu wakati ulijua kabisa
ungemchukua? Unajua ni kiasi gani nampenda Bella, bado ulimchukua yeye na mdogo
wake. Unanitesa bila sababu. Nilikukosea nini wewe Mungu? Nimejitahidi kuwa mwaminifu
kwako tokea utoto wangu, kwa nini unanilipa magumu hivi?’ Elvin alikaa mle ndani ya gari akilia kwa muda mrefu sana
huku akimuuliza maswali Mungu wake.
Wazazi wake walisikia wakati geti linafunguliwa, na wakajua
ni yeye tu kwani huo haukuwa muda wa Eli kurudi nyumbani. Baada ya kusubiri kwa
muda mrefu na kuona haingii ndani, mama yake akaamua kutoka nje kumwangalia.
Alisogea mpaka kwenye mlango wake akamkuta mwanae yupo kwenye hali mbaya sana.
Alizikumbuka siku zile akimuombolezea Bella. Akafungua mlango wake wa gari, “Twende ukapumzike Elvin.” Elvin alikausha machozi usoni mwake,
akatoka ndani ya gari. Alikwenda chumbani kwake moja kwa moja akapanda
kitandani, huku mama yake akimfuata nyuma. Na yeye aliingia akajilaza palepale
kitandani kwake.
********************************************
*Bella
ametoweka. Hakuna anayejua alipo, lakini walisha fanya kumbukumbu yake na
kukubaliana na kifo chake, huku mdogo wake naye akiwa amekufa akijilaumu
kusababisha kifo cha dada yake.
Je,
Nini kilimpata Bella? Swali lililoshindwa kujibiwa na kila mtu, hata pesa ya
Masha imeshindwa kujibu swali hilo.
*Familia
ya Mwasha ipo mtegoni. Nia ni kulipizwa kisasi kwa garama yeyote ile. Unafikiri
chanzo ni
v
Eli… aliyetoa siri za watu wote
wakagombana na Diva kuachika. Au
v
JJ…aliyeshindwa kumsamehe Diva, na kumzuia
hata kuwa karibu na watoto wake, viumbe anavyo vithamini na kuvipenda
sana Diva kwenye maisha yake. Au ni
v
Mwasha na Mkewe…Kwa usaliti kwa Mama Masha
au Irene, kwa kumpokea Bella, mke mwenzao. Au ni
v
Elvin… Aliyemkataa Irene hata baada ya
kifo cha Bella, Irene alirudi kwa magoti na kumsihi Elvin warudiane, lakini pia
alimkataa.
Je,
Nani adui ya Familia hiyo wacha Mungu!?
Wakiwa
wametulia, maisha yakiendelea, wakijua ipo amani japo wamempoteza Bella na
Eric, kumbe wapo watu wasio lala wala kusinzia kwa ajili ya kuwaaangamiza kila
mmoja wao, tena kwa garama kubwa sana.
Usikose
Sehemu ya 12.
Itaendelea kwenye website za mtazamohalisi.com
0 comments: