Story
li alikuwa na hasira
sana na wale wanawake pamoja na shemeji yake Diva. “Nitawatandika makofi nyinyi wanawake, mpaka niwaharibu sura. Nani
asiyekuwa na aibu kati yenu na Bella? Leo ndio mmesikia kama mama ndio alikuwa
mgonjwa? Mmekuja kumsanifu mama yetu na maneno machafu hapa!” “Kwani mimi sikuja kumuona hospitalini? Kila
mtu anamajukumu yake. Mtu akija kukuona pia unashukuru kwamba anakuthamini.”
“Diva nikinyanyuka hapa nitakuchapa makofi mbele ya mumeo! Naomba nyamaza na
kama huwezi, nyanyuka nenda kwenu.” “Jaribu uone. Pombe tu.” Diva
alimkejeli Eli.
My Past - Sehemu ya 10.
|
E
|
li alikuwa na hasira
sana na wale wanawake pamoja na shemeji yake Diva. “Nitawatandika makofi nyinyi wanawake, mpaka niwaharibu sura. Nani
asiyekuwa na aibu kati yenu na Bella? Leo ndio mmesikia kama mama ndio alikuwa
mgonjwa? Mmekuja kumsanifu mama yetu na maneno machafu hapa!” “Kwani mimi sikuja kumuona hospitalini? Kila
mtu anamajukumu yake. Mtu akija kukuona pia unashukuru kwamba anakuthamini.”
“Diva nikinyanyuka hapa nitakuchapa makofi mbele ya mumeo! Naomba nyamaza na
kama huwezi, nyanyuka nenda kwenu.” “Jaribu uone. Pombe tu.” Diva
alimkejeli Eli.
“Sasa si heri mimi pombe nakunywa kwa pesa yangu, kuliko wewe
mpaka uhongwe ndio upate pesa!” “Mzee Mwasha mkataze mwanao. Muone
anavyomtukana Diva.” Mama Diva aliingilia. “Mbona
umenyamaza? Wewe si jeuri? Nimekuvumilia sana Diva. Nilitaka kukutunzia heshima
yako, lakini tokea umdharau mama yangu naona hustahili heshima kabisa. Na kwa
taarifa yako kama umeshindwa kumuheshimu JJ, fanya hivyo mkiwa nyinyi wawili, kwenu,
sio mbele yetu. Unatudhalilisha sisi. JJ ni kaka yetu, anaheshimiwa humu ndani
kama Mzee Mwasha. Unapomjibu utakavyo mbele yetu, ni kutudhalilisha sisi wote
hapa.” “Nani amekwambia simuheshimu JJ? Ulitaka nimlambe miguu ndio ujue
namuheshimu kaka yenu?” “Ndivyo unavyowafanyia mabwana zako?” “Bwana gani?”
“Unafikiri mimi sikujui kama wewe ni malaya hapa mjini?” “Malaya!?
Umenifumania?” Diva aliuliza. “Unataka
mpaka nikufumanie ndio nijue unalala na bosi wako? Umemwambia mumeo hicho cheo
umepandaje?” Kila mtu alipooza gafla.
“Mimi naona twende, haya mambo yatamchanganya tu Mama Mwasha
wakati mgonjwa.” Mama Danny alitaka waondoke. “Tena
na wewe tulia kimya. Sasa hivi ndio unatambua ugonjwa wa mama? Mmbea mkubwa
wewe, unahamisha maneno nyumba hii unapeleka nyumba ile. Mbona husemi mambo ya
mumeo kama kazaa na muuza baa?” Mama Danny alishtuka sana. “Muone alivyotoa mimacho. Ulikuwa hujui?
Sasa subiri UKIMWI unakujia. Maana mumeo nakunywa naye, na kazi yake kubwa
kulala na kila msichana anayemkubali pale baa.” “Eli naomba unyamze.” “Wambea sana mama hawa. Tena wanafiki.
Wanajidai wao na watoto wao ndio watakatifu sana.” Wote walinyamaza.
Eli akamgeukia Diva. “ Diva vipi jeuri yako?” “Unaongea nini
Eli?” JJ akauliza. “Mkeo anagongwa na
bosi wake. Na ndio maana anakudharau na ndio jeuri yake yote ipo hapo. Kama
huamini na anabisha, nitampigia simu aje sasa hivi, hapa hapa mbele yenu huyo
Jamaa aliyekuwa anatakiwa apate hicho cheo cha mkeo, lakini bosi mtu
akamdhulumu hicho cheo, akampa hawara yake, huyo Diva mkeo halafu yeye
akamuhamisha kitengo. Jamaa akakasirika, akaamua kuacha kazi. Kama wewe
mwanamke, bisha tena nilete uthibitisho. Maana Jamaa anawafuatilia sana na ana uthibitisho
wa kila kitu. Anajua nyumba ya wageni, yaani hoteli mnayokutania, siku zenu
hizo za jumamosi mnazodanganya mpo kazini kumbe mmejifungia huko, mpaka mida yenu
mnayokutana na huyo Bosi wako. Na picha zenu zote pia anazo mkiwa huko hotelini.
Bisha tu, nimwabie anitumie zile picha sasa hivi au yeye mwenyewe aje. Mimi nimezikuta
Bar akiwa na marafiki zake wakifanya mipango ya kuwaangamiza wewe na Bosi wako.
Watu walimpa hiyo akili, akawa anawafuatilia kwa karibu na walimpa ushauri wa
vitu gani vya ushahidi awe navyo ili aje awashitaki kwenye kikao chakufunga
mwaka, cha mabosi wenu wote. Na kwa taarifa yako Diva, hata ofisini kwenu
wamekuchoka. Wamemsaidia jamaa kumpa copy za madai yenu yote mliyokuwa
mkikusanya kwa muhasibu wenu, na pesa zote anazoidhinisha Bosi wako za malipo
mnayojidai mnalipana kwakufanya kazi overtime
siku za jumamosi, kumbe mnakuwa mpo sehemu zenu mnafanya uchafu wenu. Vyote
hivyo anavyo. Kuanzia tarehe, muda na sehemu pamoja na madai yote mliyolipwa
ofisini siku na tarehe zilezile na muda mliojifanya mnafanya kazi kumbe
mnafanya starehe. Ongeza neno, nimwambie atume sasa hivi hapa na nimpe ruhusa
awashitaki, maana mimi ndio nilimpooza kwa heshima ya JJ, nimemtafutia kazi
sehemu nyingine na kumlipa pesa kama kumtuliza, lasivyo ungekuwa pabaya sana wewe
Diva, na hakuna ofisi wangekupokea kwa umalaya wako, ubadhilifu wa mali za uma,
na kingine kutumia rushwa ya ngono kupanda cheo.” JJ alinyamaza.
“Na wewe Mama Banda, toa sura yako humu ndani, hata wewe mwizi wa
waume za watu, kama mmeo anavyolala na wafanyakazi wenu wa ndani. Nguvu
yakumsema Bella na Mzee Masha mnaitoa wapi nyinyi?” “Eli jiangalie wewe mtoto. Kwanza muongo. Banda anajiheshimu wala sio
Malaya.” Eli alianza kucheka sana. “Wewe
mama unataka kuingia aibu wewe! Ngojeni kwanza nikalete mwiko jikoni, wakati
Mama Banda unaendelea kuongea. Mtaumbuka leo nyinyi, hamtakaa mkanyage hapa.”
Eli alienda jikoni akarudi na mwiko wa kusongea ugali.
“Sasa mnisikilize kwa makini, kila mmoja nampa dozi yake, lakini
marufuku kupigana humu ndani. Nawapa dozi zenu, mtaenda kumezea huko nje.
Nikiona mtu ananyanyuka kuanza kutaka kuleta fujo humu ndani kwetu wakati mama
yangu mgonjwa nawachapa wote, tena usoni. Mmejileta wenyewe, na kuanza kujidai
mnamuumbua Bella. Sasa naendelea na wewe Mama Banda unayesema wewe mtakatifu, hujalala
na Mzee Mwanga?” Kila mtu alishtuka. Mama Mwanga akasimama. “Unasemaje wewe Eli?” “Kaa chini na wewe. Unashtuka nini? Si umuulize
huyo rafiki yako?” “Huwezi kuwa unanifanyia hivyo Mama Banda. Si ndio?” Eli akaanza kucheka.
“Waone sura zao. Mbona wote mmetulia?” “Wewe Mama Banda?” Mama Mwanga akamwita kwa
hasira sana. “Sauti hiyo, Mama Mwanga.
Nikikusogelea hapo, utanitambua mimi ni nani. Nendeni kwenu mkasutane vizuri.
Sio hapa kwetu. Hapa mnapewa dozi tu, mtaenda kuugulia maumivu nje ya hilo
geti. Nyinyi si mnajidai kumdharau mama yangu? Leo mtatoka jasho la damu.” “Wewe
Mama Banda ndio wakunifanyia hivyo mimi?” “Nikipindi kile cha matatizo na
mumeo, ukaondoka nyumbani kwako.” Mama Banda alijibu kwa sura ya aibu.
“Wenzako wanajua kuwa unatembea na dereva wa mumeo? Maana
tunakunywa naye kule baa kwa pesa unazo muhonga za mumeo. Anayasema yote.” Eli alimgeukia Mama
Mwandri. Wote walimgeukia Mama Mwandri. “Kumbe
mashoga zako hawajui?” Eli alinza kucheka huku anapiga makofi. “Mngejiona sura zenu! Kama sio nyinyi
mliongia humu ndani kwa dharau. Halafu hapo kati yenu sijamuona hata mmoja wenu
ambaye Masha angemtaka angemkataa. Ni hivyo mwenyewe hajawataka hata mmoja wenu
hapo, kamtaka Bella, roho na wivu vinawauma.” Wote walikuwa wamenyamaza
kimya.
“Mbona hambishi tena? Mmetosheka na dozi au niendelee na wewe Mama
Banda ili uondoke hapa na yako na mumeo?” “Eli! Eli!” Mama yake akamwita. “Naomba niangalie mimi Eli.” Mama yake
alimsisitiza, Eli akamgeukia mama yake. “Naomba
unyamaze, inatosha.” “Wamezidi hawa mama. Tena ndio hawa hawa wanaomsema na
Elvin. Sasa...” “Hapana Eli. Naomba
unyamaze.” Eli alitulia kidogo. “Sawa mama. Lakini nipe kama dakika moja
niwamalizie.” “Hapana Eli.” “Basi mama. Mumshukuru Mama Mwasha. Nilitaka
kuhamia kwa watoto wenu mnaowaabudu. Kutwa mnawatoa mimba halafu…” “Eli?” “Basi mama. Haya tokeni nje, naona muda wenu
wa kumuona mgonjwa umeisha. Na mkamwambie Mama Masha, mke mwenzake yupo hapa,
anafanya kazi alizoshindwa kuzifanya cha mdomo Diva. Haya simameni haraka kabla
sijawasogelea hapo.” Wote wakasimama.
“Diva, naomba nisikukute nyumbani, wala usiguse watoto wangu hata
mmoja.” JJ aliongeza. “Nitaenda
wapi?” “Wewe mjinga nini? Swali gani hilo? Naomba nisikukute nyumbani, mpaka
nitakapo kutafuta.” “Basi naondoka na watoto.” “Nitakunyonga Diva! Naomba
uondoke.” Diva alitoka. Elvin akasimama akaenda kumshika Bella mkono pale
alipokuwa amebaki amesimama. “Twende
Bella.” Elvin naye alitokea mlango wa jikoni akiwa amemshika Bella mkono.
“Nimeharibu nini Mama?” Eli kama kawaida yake alimgeukia mama. “Sana Eli mwanangu.” “Daah! Kumbe heri
ningenyamaza pale pale uliponiambia, eeh?” Kama sio yeye, Eli alirudi kuwa mnyenyekevu
sana. “Ndiyo Eli. Uwe unanisikiliza. Ona umeharibu ndoa ya kaka yako.” “Hiyo
ndoa ilishakufa muda mrefu sana mama, wala usimlaumu Eli. Heshima hakuna,
mwanamke anadharau kama nini! Haridhiki kwa kila ninachompa! Haambiliki! Mwache
aende, nipumzike.” “Hizo ni hasira
JJ. Tulia ufikirie vizuri.” Mzee Mwasha aliyekuwa kimya muda wote
aliongeza. “Kila siku unaniambia
hivyohivyo baba. Mbona habadiliki?” JJ aliuliza kwa hasira. “Hujui shida ninazopata na Diva, baba. Na
mimi nimechoka, mwache aende kwa huyo bwana wake na mimi nipumzike.” JJ
alikuwa akimfuata baba yake na kumuomba ushauri juu ya ndoa yake kila wakati
bila mama yake kujua.
**********************************
Elvin alimtoa Bella nje
upande wa jikoni. Bella alikaa kwenye ngazi na kuanza kulia sana. Alilia kwa
kwikwi kwa muda, mwisho akasimama. “Naomba nirudishe
nyumbani Elvin.” “Unaondoka na mama?” “Hapana bwana Elvin. Mama hatataka kuniona tena.” “Ndivyo alivyokwambia?” “Nakaaje
tena na mama wakati nimekuwa na mahusiano na mume wa rafiki yake?” “Muone! Ujanja wote umekuishia.” “Bwana Vin!” “Wewe ulitegemea
ingekuwa siri daima?” “Najua watu wangejua,
lakini si kwa namna hiyo.” “Wewe unafikiri mama
hakuwa akijua?” Bella alishtuka sana. Mpaka machozi yakakauka gafla.
“Unafikiri mama alikuwa akijua kabla ya hapo?” Elvin akacheka tena
huku akimtizama Bella. “Usicheke bwana
Elvin. Nani alimwambia baba na mama?” “Irene.” Bella aliweka mikono
kichwani. “Elvin! Lini?” “Mama aliniambia
nilipotoka tu Arusha. Unakumbuka siku tunarudi kutoka Arusha, tukamkuta Irene,
baba na mama, pale mapokezi?” “Nakumbuka.” “Basi ndio siku aliyokuwa amekwenda
kuongea na wazazi wangu juu ya mahusiano yako na Mzee Masha.” Bella alikaa
chini. “Sasa ukamwambiaje mama?”
“Nikamwambia nafahamu, na ulishaniambia.” Bella alikaa kimya.
“Usiwaogope wazazi wangu Bella. Ni waelewa sana, na maadamu hayo
ni maisha yako ya nyuma, hawawezi kukuhukumu.” “Uwiii!” Bella alikuwa kwenye
mshtuko sana. “Yaani muda wote nipo nao,
kumbe wanajua maisha yangu ya nyuma!? Wanajua nilishaishi na yule baba,
wanaju…” “We Bella! Hebu acha hizo bwana! Ndio inatakiwa kukuongezea ujasiri,
kujua kuwa wanakufahamu vizuri na bado wanakupenda na kukuheshimu. Acha
kuchanganyikiwa bwana.” “Mimi naona nirudi nyumbani nikatulie kidogo.” “Sasa hapa unamkimbia nani?” “Sijui. Labda
nikapumue kidogo.” Elvin alianza kumcheka tena.
“Si tumekupa chumba? Nenda ukapumulie huko.” “Nawatizamaje tena
ndugu zako?” “Kama ulivyokuwa ukiwatizama zamani. Acha woga Bella bwana. Huwezi
kuepuka hilo. Ni kweli ni maisha uliyoishi na Mzee Masha, mume wa mtu na ni
kama baba yako. Yatakuja mambo mengi tu, ni wewe kujiandaa jinsi ya kuyakabili.
Nakuaminia Bella. Utaweza. Kama uliweza kutoka mikononi mwa Mzee Masha,
anayeogopewa na kila mtu, na umeweza kusimama mpaka sasa hivi, ujue wewe ni
jasiri na hutashindwa chochote kitakacho
kukabili. Usiogope.” “Asante Elvin.” Bella alitulia kidogo.
“Mama amekuomba uende naye India.” “Kweli bwana. Nilishasahau.
Ningependa kwenda Elvin, lakini namfikiria Ric. Wanafunga shule majuma machache
yajayo, nani atamfuata, atakaa wapi, na nani? Hajiwezi Ric kwa lolote. Kama
unavyomuona, atakuwa akicheza game tu, nikirudi nitamkuta amekufa.” Elvin alicheka kidogo. “Mimi nitakuwa naye Bella.” “Kweli?” “Nafikiria
wakipanga hiyo siku ya nyinyi kwenda India, kabla hawajafunga shule, twende
mpaka shuleni, ukamuage, halafu shule zikifunga nitaenda kumchukua tuje tuishi
naye hapa mpaka utakapo rudi. Na nitakuwa nikienda naye kazini kila siku ili
kutoa mawazo yake kwenye michezo.”
“Hapo utakuwa umetatua tatizo kubwa sana.” “Kwa hiyo utaenda na mama?”
Bella alibaki akifikiria kidogo.
“Bella!” “Nitaenda lakini sasa hivi namuogopa sio kama zamani.”
“Huna haja ya kuogopa Bella. Tena ndio mtapata muda mzuri wakufahamiana zaidi.”
“Nitaenda Elvin. Na kazini sasa?” “Mshahara wako utalipwa kama kawaida.” “Simaanishi mshahara bwana, namaanisha kazi. Unawaza pesa tu.”
Bella aliinama na kuchota maji yaliyokuwepo kwenye ndoo, kwa mikono yake yote
miwili, akamwagia Elvin.
“Umeanza Bella!” Bella alianza kucheka huku akisogea mbali
kidogo ya Elvin. “Hakuna umbali utakao
kwenda, nikashindwa kukufikia, nikulipize. Heri usogee karibu, nikulipizie
yaishe.” Bella alikuwa akicheka sana. “Ujue
Elvin kulipiza ni dhambi wewe!” “Njoo Bella.” “Hapana Elvin, jifunze kusamehe.”
Bella na Elvin walianza kukimbizana wakimwagiana maji pale nje, huku wakicheka
na kupiga sana kelele. Waliokuwepo ndani wakashtuka sana, ikabidi watoke.
Waliwakuta wote wamelowana. Kaka zake Elvin na baba yao wote walibaki wakiwaangalia
Elvin na Bella. “Elvin ndio ameanza.”
Bella alijitetea kwa kumnyoshea Elvin kidole. Akajivuta nyuma kidogo ya Elvin
kama kujificha, akainama. Mwasha na wanae walibaki wakishangaa. “Bella! Mama anakuita ndani.” Mzee
Mwasha aliamua kuvunja ukimya maana wote walikuwa bado wanamshangaa Elvin,
waliyejua ni kijana mtaratibu sana.
**********************************
Hawakuwahi kumuona Elvin akifanya mambo ya
kitoto vile. Yeye alikuwa mzuri sana wakupangilia mambo na nimtekelezaji. Kila
mtu pale nyumbani kwao, alipenda kumtumia yeye. Ukiwa na jambo lolote lile, hata
kama limekaa vibaya, ukimkabidhi Elvin, atalipangilia na atalifuatilia kwa
makini sana bila kukata tamaa mpaka kitokee kitu kizuri. Ndio maana hata
walipoona baba yao akisumbuka na biashara zake, magonjwa ya moyo hayaishi
sababu ya wasiwasi, walimuomba Elvin aingilie kati kumsaidia baba yao. Kipindi
cha mwanzoni ilibidi kaka zake wasaidie kulipa mshahara wa Elvin, wakati
akifufua biashara ya baba yao. Mwishowe Elvin aliwaandikia ndugu zake matatizo
aliyoyaona yanaendelea kwenye kampuni ya baba yao, na jinsi ya kuyatatua.
Walichangishana pesa ndugu hao, Elvin akaziba nyufa zote na kurudisha uhai
kwenye kampuni ya Mzee Mwasha. Akaongezeka na Bella ambaye alileta maarifa
mapya yaliyoongeza faida kubwa sana kwenye hiyo kampuni.
**********************************
Bella aliishi nao hapo
ndani akimuhudumia mama yao bila shida wala kinyaa huku akimfariji na kumtania
ili kumfanya asijisikie vibaya kila anapojichafua. Walimtegemea kwa kila jambo
juu ya afya ya mama yao. Kila aliyetaka kujua mambo yanayomuhusu Mama Mwasha,
aliulizwa Bella. Akageuka kuwa mtu muhimu sana kati ya wanaume hao watano. Taratibu
Bella akaanza utundu kwa kila mmoja wao pale ndani. Akawa mcheshi sana
akichekesha kila mtu pale kwenye nyumba ya Mzee Mwasha, zaidi Eli aliyemuokoa
katikati ya kuaibishwa, ndiye walizidi kuwa karibu. Walimpenda sana na akili
zake za kitoto na vile asivyojali mambo madogo madogo. Ni binti ambaye alikuwa
rahisi sana kuishi naye tofauti na alivyoonekana.
“Mimi
nina sumbuliwa na hili swali Bella.” Eli alianza siku hiyo wakati wapo na
Bella jikoni. Lakini wengine wote, mpaka wazazi wao walikuwa upande wa sebleni
wakiwasikiliza. “Hivi wewe Bella,
uliwezaje kuishi na Mzee Masha na akili hizo za kitoto hivyo!?” “Yule baba ni
shetani mkamilifu. Alikuwa ananipiga karibu kuniua. Muulize Elvin. Hataki utani
na mtu.” “Sasa ulikuwa unaishije
nae?” “Daah! Hata sijui jamani! Unafikiri nilikuwa nacheka hivi? Hamna. Nilikuwa
nalia sana, mchana na usiku nilikuwa nalia namkumbuka mama yangu, mpaka
nilipompata Elvin. Nikamsimulia maisha ninayoishi, ndio akanipa ushauri jinsi
ya kujikomboa.” “Kujikomboa tena?
Mimi nilijua alikuwa mpenzi wako.” “Hivi we Eli ujue mimi ni mtoto sana na
niliambiwa na mama yangu nisubiri mambo ya wanaume. Sasa yule baba mtu mzima vile
kwa nini awe mpenzi wangu!” “Si sababu ya pesa? Yule baba anapesa sana.” “Sasa
hizo pesa zake ndio zilitaka kunitoa roho. Alikuwa akinitesa sana. Muulize
Elvin.” “Sasa ilikuaje mpaka mkawa
wapenzi.” “Ujue sitakusimuli wewe, kama unasema yule baba ni mpenzi wangu!”
“Basi mumeo.” “Naondoka Eli.” “Njoo Bella wangu unisimulie. Ujue mimi ndio
nitakuoa?” “Aka. Sitaki.”
“Unamtaka Elvin?” Eli aliuliza. Bella akacheka sana.
“Elvin! Hahahahaha. Elvin ni ‘my BFF’ unajua BFF?” “Best Friend
Forever?” Eli aliuliza. “Ewaa. Basi
ndio mimi na Elvin.” “Humpendi?” “Si ndio maana nakwambia ni my BFF. Hata kama
akija kuoa bado tutabaki kuwa marafiki. Sifikirii hata kuolewa kesho. Nitabaki
na Mama Mwasha wangu tu.” “Hutaki Elvin akuoe?” Bella alicheka tena. “Wewe naona hujamjua Elvin vizuri. Elvin
anajiheshimu sana, halafu ananijua mimi kuliko mtu yeyote hapa duniani. Hata
hiyo nafasi aliyonipa yakuwa rafiki yake tu nashukuru Mungu. Elvin anastahili
msichana mzuri, aliyetulia sio kama mimi nimepita kwenye maisha mabaya sana.
Sitaki hata kufikiria swala la ndoa, Eli. Sitaki hata kufikiria mwanaume.”
Bella alipooza sana. “Mungu ameniokoa
kwenye hatari ya kifo, huko sirudi tena. Inatosha. Alinitesa na kunidhalilisha
sana yule baba. Mpaka nikikumbuka hata
kama nipo usingizini, nikiamka nakuta mto umelowa kwa machozi.” “Pole Bella. Alikufanyaje? Au ilikuaje mpaka ukaishia mikononi
mwake?” Bella alifuta machozi.
“Usilie bwana.” “Si unamjua Zera yule
mwanae?” “Namfahamu sana.
Mapepee.” Bella alicheka huku akifuta machozi. “Alikuwa rafiki yangu sana. Sasa baada ya mama yetu kufariki, tulipata
shida sana. Nikaamua kwenda kwao kuomba msaada. Nikamkuta yeye Zera na mama
yake. Nikawaelezea jinsi tulivyo na shida na kuomba msaada wa aina yeyote ile.
Wakatufukuza nyumbani kwao. Basi tukaondoka, wakati tupo njiani ndio dereva
wao, akatufuata akasema ameambiwa aje atuchukue. Mimi nikajua ni mama yake Zera
amebadili mawazo, akatuonea hurua, ndio amemtuma aje atuchukue. Akatupeleka
hotelini, akatuletea pesa, na kutuambia tule kitu chochote tunachotaka. Tusiwe
na wasiwasi. Kumbe ndio ulikuwa mwanzo wetu wa matatizo.” “Kwa nini hukuuliza
tokea mwanzo?” “Niliuliza Eli. Tena
kabla sijapanda kwenye lile gari siku ya kwanza. Yule dereva akasema, ‘wewe
si unataka msaada? Basi ndio unapewa msaada’. Sasa mimi nikajua ni Mama Masha tu. Kwa kuwa ndiye niliyekuwa nikiongea
naye pale nyumbani kwake, Mzee Masha mwenyewe alikuja wakati tunamalizia
mazungumzo. Hata nilipofukuzwa, hakuchangia hata neno. Nikajua hata hakuwa
ametusikiliza. Kumbe lile libaba, lilikuwa linafurahia
vile mkewe alivyotufukuza ili liwe na mimi. Alinitesa Eli wewe, we acha tu.”
“Pole Bella. Pole sana.” “Yaani hata vidonda alivyoniachia moyoni havijapona na
sijui kama vitakuja kupona tena maishani. Sijui.” Bella alikaa kimya kwa
muda.
“Unajua isingekuwa Elvin, mpaka sasa hivi ningekuwa nikiteseka kwa
yule baba? Nilikuwa nina hela kweli. Nilikuwa naendesha gari hiyo, sijui niya
mamilioni mangapi! Lakini nilikuwa sina raha hata kidogo. Akianza kunipaga,
hataacha mpaka nizimie ndio ananiacha au aone ninakaribia kufa.” “Sasa alikuwa
anakupiga kwa nini?” “Wivu. Tena wivu usio hata
na maana. Akipiga simu usipopokea kwa wakati, ananipiga. Yaani sababu za
kijinga tu.” “Kwani ulikuwa na mwanaume mwingine?” “Eli wewe jamani!?” Bella
alishangaa sana.
“Hivi unajua nina miaka mingapi? Kuna jinsi mama yangu alinilea,
naona ndio amenifanya nichelewe kukua akili za wanaume. Nakwambia sikuwa hata
nawazo la wanaume. Kwanza shuguli ya yule baba! Huwezi kufikiria hata mwanaume
mwingine. Jamani sijawahi ona baba mkorofi kama yule! Siku ya kwanza kulala na
mimi, niliumwa sana Eli. Sitakaa nisahau. Halafu wala hakunipa pole, akaenda
kuniacha kwa…” Bella aliangalia kulia na kushoto. “Wapi?” “Nyumbani kwa Eno.
Ili anitibu.” Eli alishtuka sana.
“Eno huyu Eno Mwasha?” “Usiseme kwa nguvu sasa, wewe ukoje?”
“Eno!?” “Ndiyo. Eno huyuhuyu kaka yako anayeishi Dubai.” “Kwa nini sasa?”
“Nilizimia wewe Eli. Nahisi na mshtuko pia ulichangia.” “Kwa hiyo mnafahamiana
na Eno.” “Nilikuwa na hasira siku ile, sikuongea na mtu hata mmoja, tena na
Elvin alikuwepo hapo nyumbani kwa Eno. Wewe huoni namuogopa sana kaka Eno? Nashindwa
hata kumtizama muda mrefu?” Bella aliendelea kunong’ona. Eli alianza kucheka. “Eno mtu poa sana. Hana
neno.” “Mmmh! Sasa sijui Mzee Masha alimwambia nini? Maana aliniwekea mpaka
damu. Ndio maana namuogopa.” “Haiwezekani Bella!” “Kweli. Nilipoteza fahamu
tukiwa hotelini damu zikinivuja. Nikaja kuzinduka nyumbani kwa Eno na dripu ya
damu mkononi. Eno akanitibu mpaka nikapata nguvu, tukarudi hotelini.” “Maskini
Bella! Kumbe kweli ulikuwa mtoto.” “Masha ndio alinikomaza!” Akafyoza nakumfanya Eli
acheke sana. Waliendelea kuongea wawili pale jikoni.
“Ngoja nikamchokoze Elvin halafu nimsingizie kwa baba yeye ndio
ameanza.” Bella aliaga. “Mwache bwana,
tuendelee kuongea.” “Unapenda stori wewe! Mimi nina hamu yakumchokoza Elvin.
Hata hivyo nimechoka kuongea.” Eli akacheka. “Hivi wewe Bella, utakuja kukua kweli!?” Bella alicheka na yeye. “Mimi mtu mzima mwenzio. Ngoja nikamwangalie
Mama Mwasha kipenzi changu ndio nimchokoze Elvin. Hivi nilikujibu kuhusu Vin?”
“Kuhusu nini?” “Kama hukumbuki basi.” “Njoo bwana Bella, mbona hivyo?” “Sasa
mtu mwenyewe unasahu maswali yako mwenyewe! Vin huwa hasau mambo.” Bella
alikasirika usoni na kukunja mikono yake kifuani kama katoto kadogo kakavuta
mdomo.
“Nakumbuka bwana. Si nilikuuliza kama unampenda na unataka akuoe?
Ukanizungusha na maneno mengii, hata sijajua jibu ni lipi. Si ndio hivyo?”
“Sasa je? Unawezaje kusahau maswali muhimu kama hayo?” “Sijasahau bwana. Kwa
hiyo unampenda na unataka yeye ndio akuoe?” “Kama unaniwekea majibu mdomoni,
basi sikujibu naondoka.” “Usiondoke bwana Bella, si unijibu?” “Sitaki. Kwanza
wewe mwenyewe ulisahau, unaonyesha sio maswali ya muhimu.” “Njoo Bella.”
“Sitaki naenda zangu kwa Vin!” Bella aliondoka huku Eli akiendelea kumwangalia
na kucheka.
**********************************
Ilikuwa lazima chakula
cha usiku Bella na Elvin wale pamoja. Elvin alikuwa akienda kazini asubuhi
nakumuacha Bella na mama yake nyumbani. “Sasa
wewe Bella, utakaa na njaa mpaka saa ngapi? Heri ule tu. Elvin anaweza
kuchelewa sana leo, si ndio wanafunga mwezi?” “Akirudi halafu akakuta
nimeshakula, hatakula tena. Labda nimpelekee chakula hukohuko kazini.” “Mmh!”
Mama Mwasha aliguna. “Wewe shida yako
uende tu ukamchokoze mwenzio.” Bella alicheka. “Ulijuaje mama? Nataka nikamuone sura yake ilivyo sasa hivi. Atakuwa
kama ndio mwisho wa dunia! Na wale watu wa idara ya wamasoko walivyo wakorofi!
Wanakuwa hawamalizi kazi zao mpaka mwisho wa mwezi. Basi Elvin anapooza huyo!”
“Nenda kamsadie basi.” Bella alifurahi sana. Aliruka pale alipokuwa amekaa
pembeni ya Mzee Mwasha, nakuanza kucheza. Mzee Mwasha na mkewe, wakaanza
kucheka.
“Hivi Bella wewe utakuja kukua kweli?” “Wewe mama subiri. Nikifika
tu nitakupigia picha zake nikutumie umuone alivyopooza mwanao.” “Umsaidie bwana
Bella, usimchokoze.” “Kama ndio hivyo haina haja hata ya kwenda.” Akarudi kukaa. “Basi kidogo tu halafu mfanye kazi, muwahi
kurudi.” “Yess.” Bella alikimbia chumbani kwake kwenda kubadili nguo, baada
ya muda mfupi alitoka chumbani. “Mama!
Wewe ukiwa na shida yeyote unipigie simu, nitarudi haraka sana.” “Asante Bella
mwanangu.” Bella akatoka.
**********************************
Ilikuwa ngumu Bella na
Elvin kuachana kwa muda mrefu. Wakati mwingine Bella alimtembelea Elvin kazini,
kisha wanatafuta sehemu ya kwenda kula pamoja au Elvin alirudi nyumbani kwa
ajili ya chakula cha mchana. Walipopata tarehe ya kwenda nchini India kwa ajili
ya matibabu ya Mama Mwasha, ilimlazimu Bella kwenda kumuaga mdogo wake. “Tutaenda wote Bella.” “Afadhali. Lakini itabidi kukata tiketi ya
asubuhi turudi usiku, tusimuache mama bila mtu. Naona jana hakulala vizuri.” “Basi
nitaenda kuangalia tiketi za kwenda na kurudi siku hiyo hiyo.” Bella na
Elvin waliondoka na ndege ya asubuhi sana kuelekea jijini Arusha.
Walipotua tu, walikwenda
moja kwa moja shuleni kwa kina Eric. Wakapata muda mzuri sana naye. “Kwa hiyo nitakuwa naishi kwa kina Elvin?”
“Kwa muda mpaka nitakapo rudi.” Eric
akanyamaza. Bella wakaangaliana na Elvin. “Kwani
hutaki kuishi kwa kina Elvin?” “Nataka,
lakini nataka na wewe uwepo Bella. Nilikuwa na hamu na wewe kweli. Ngoja
nikuletee barua nilizokuwa nimekuandikia.” Eric alikimbia bwenini kwao,
akarudi na barua nyingi sana alizokuwa amemwandikia dada yake.
“Ulinisahau Bella!” Eric aliongea kwa uchungu sana. “Hapana Ric. Unajua siwezi kukusahau hata iweje. Mambo
yalibadilika. Sikuwa na…” Bella alifuta machozi. “Nakupenda sana Ric. Nahangaika
kwa ajili yako. Siwezi kukusahau hata iweje. Halafu unajua nini?” “Nini?” “Nimekutafutia shule ya palepale Dar, tuwe tunaishi
wote.” Eric alifurahi sana. “Kwa
hiyo hakuna kutengana tena?” “Hakuna. Safari hii ukirudi nyumbani, ndio basi.”
“Nyumbani au hotelini?” Bella hakuwa ameenda kwa mdogo wake tokea
alipoachana na Mzee Mwasha. “Sasa hivi
tuna nyumbani kwetu Eric. Sio pakubwa, lakini ni kwetu.” Eric alimkumbatia
dada yake. “Asante Bella. Najua
unahangaika sana. Asante.” “Lakini Ric, mbona ni kama ulionekana unapapenda
sana hapa?” “Kwa kuwa uliniahidi ukikaa sawa, utakuja kunichukua. Kwa hiyo ndio
maana ikabidi niwe mvumilivu ili nisikutie wasiwasi.” “Miaka yote hiyo! Kwa
nini hukuniambia? Mimi nilijua unapafurahia hapa.” “Hapana Bella. Mimi nataka kuishi
na wewe. Sitaki kuishi huku peke yangu.” Bella alimkumbatia Eric. “Basi Ric, kuanzia sasa hivi tutakuwa wote.”
“Sema kuanzia siku utakayorudi kutoka India.” “Naamini sitakaa sana, mama akitibiwa tu, tutarudi.” “Atapona?” Eric
aliuliza kwa wasiwasi. “Tunaamini Mungu,
atapona Ric.” Elvin alijibu. “Mungu
asaidie huyu mama wa sasa hivi apone, asimchukue kama mama yetu. Sinilikwambia
mama yetu hakupona?” “Uliniambia Ric.” “Alikufa. Hakupona.” Bella aliinama
akijaribu kuzuia machozi. “Ukifunga tu
shule, nitakuja kukuchukua Ric. Usiwe na wasiwasi.” “Asante Elvin.” Eric
alishukuru.
“Safari ya
India.”
Usiku wa kuamkia siku ya
kwenda nchini India kwa ajili ya matibabu ya Mama Mwasha, ulikuwa mgumu sana
kwa Elvin na Bella. Wote hawakuwa na furaha hata kidogo. Elvin aliwahi sana
kutoka kazini wakabaki wamekaa kwenye meza ya kulia chakula. Hapakuwa na utani
mwingi sana usiku huo, kila mtu alijua Bella aliyezoea kumchokoza kila mtu ana
tatizo. “Vipi Bella mwanangu.” Mzee
Mwasha alimfuata mezani akamuuliza.
“Natamani ningekuwa na begi kubwa nikamuweka Elvin humo ndani, tukaenda naye.”
Wote walicheka. “Muone alivyo mchokozi!
Na huko utajifunza kutulia, utakuwa huna mtu wakumchokoza.” “Nitapooza sana.” Bella
alifikiria kidogo. “Eti baba nikikuletea
mchumba wa kihindi si utampokea?” Mzee Mwasha alicheka sana. “Unataka kuolewa na Muhindi, mwanangu?” “Utafanyaje
sasa, kama ndio tunahamia hukohuko?” “Tunawaombea Mungu mambo yaende sawa, muwahi
kurudi.” “Kama tukikaa sana utakuja kutuona baba?” Bella aliuliza kwa
upendo sana. “Nitajitahidi kuja kuwaona
Bella. Na tutakuwa tukiongea kila siku.” Bella alionekana kufurahia.
Alijawa upendo wa kitoto lakini uliomfanya kila mtu karibu naye ajisikie
vizuri.
**********************************
Watoto wote wa Mzee Mwasha walimpenda sana mama
yao na kuonyesha kumjali mama yao kuliko baba yao. Sasa Bella alipokuja pale
alijisogeza karibu sana na Mzee Mwasha. Japokuwa Mzee Mwasha alikuwa Mzee mpole
sana na mwenye hekima, lakini Bella alimfanya acheke kila wakati. Popote
alipoenda alimletea Mzee Mwasha zawadi hata ya pipi. Na alijisahau kabisa
kumwita Mzee Mwasha, akageuka kuwa baba kila wakati. Kila alipomuona ametulia,
alimfuata na kumwambia wajipige picha wakiwa wamekaa hivi au vile, wakati
mwingine alimfundisha kucheza games za simu yake mwenyewe Mzee Mwasha. Alikuwa
akimcheka vile Mzee Mwasha alivyokuwa na simu nzuri, lakini aliitumia kupiga na
kupokea simu tu. Ali download games nyingi sana na
kucheza naye kwenye simu huku akimwambia washindane. Wakati wote alipenda kukaa
pembeni ya miguu ya Mwasha kama wanaangalia kitu kwenye luninga.
**********************************
Eno alishaondoka kurudi
kazini nchini Dubai lakini aliahidi kuwafuata nchini India endapo mama yake
atafanyiwa upasuaji huko. “Namimi
nitakuja Bella kama mtakaa muda mrefu huko, usilie bwana. Nitaenda kumfuata
Ric, tutakuja kuishi naye hapa. Umesikia?” Bella alitingisha kichwa.
Alishindwa kabisa kuongea wakiwa uwanjani hapo wakisubiri muda wa ndege ufike
waondoke. Mzee Mwasha alimkumbatia. “Utakuwa
sawa Bella, usiwe na wasiwasi. Kama Elvin alivyosema, kama mtakaa huko kwa muda
mrefu tutakuja kuwatembelea. Cha muhimu umuangalie mama, umesikia?” Bella
alitingisha kichwa huku akilia na kutoa tabasamu la kuwafariji wakati yeye
mwenyewe alionekana akiwa hana furaha.
Tangia ampate Elvin,
akamsaidia kumtoa mikononi mwa Mzee Masha, hawakuwahi kutengana. Na walishazoeana
kupita kiasi. Kila wakati walikuwa wote na kula wote kila siku usiku. “Sasa nikirudi nisipomkuta Elvin?” Bella alimuuliza Mzee
Mwasha huku akilia. Mzee Mwasha akacheka. “Hana
pa kwenda huyu. Utamkuta tu.” Eli aliendelea kucheka. “Sasa wewe unafikiri huyu Elvin atakwenda wapi?” Alimuuliza Bella. “Sijui mimi!” Elvin alimvuta kutoka kwa baba yake, akamshika
mkono akasogea naye pembeni.
“Niangalie Bella.” Bella alikuwa akilia sana. “Naogopa Elvin.” “Usiogope, nitakuwa
nakupigia simu kila siku usiku kabla ya kulala, halafu majuma mawili yakipita
bado hamjarudi, nitakuja kuwaangalia. Sawa?” “Usipokuja?”
“Nimeshawahi kukuahidi kitu halafu nikashindwa
kufanya?” Bella alitabasamu, akatingisha kichwa kukataa. “Basi ujue nitakupigia simu kila siku na
nitakuja kama mkikaa zaidi ya majuma mawili. Naomba utulie, naamini kila kitu
kitaenda sawa. Umesikia?” Bella alitingisha kichwa. “Hapana Bella, nataka uitikie.” Bella alicheka. “Nimeelewa bwana, wewe ukoje?” Elvin akacheka. “Haya twende tukanunue maji unywe, wakati
mnasubiri kuondoka.” Bella alitulia kabisa kidogo akaanza kuongea na watu
wengine mpaka muda wa kuingia kwenye ndege ulipofika.
Alienda kumkumbatia Eli
na kumbusu shavuni. “Uhakikishe Vin,
anakula. Sio unachelewa kurudi nyumbani. Unanisikia wewe Eli?” Eli alicheka. “Sawa
mama.” Akambusu tena kisha akamsogelea Mzee Mwasha. “Ubaki salama baba yangu, eeh!” “Na nyinyi msafiri salama. Tunawaombea
Bella. Kila kitu kitakuwa sawa.” “Upone kabisa baba.” Bella aliongeza. “Si unaniombea?” Mzee Mwasha alimuuliza.
“Tunakuombea mimi na Elvin kila siku. Na
amesema atakuwa ananipigia simu kila siku usiku kabla sijalala, kwa hiyo
tutaendelea kukuombea.” Mzee Mwasha akatabasamu. “Asante mwanangu. Na ujue tunakutegemea huko. Uwe unatujulisha kila
kitu kinachoendelea.” “Usiwe na wasiwasi baba. Nitakuwa karibu sana na mama, na
nitahakikisha kila wakati anafuraha.” Akamkumbatia tena Mzee Mwasha na
kumbusu, kisha akamsogelea Elvin. “Umeniahidi
utakuja Vin.” “Yakizidi majuma mawili Bella. Kumbuka nitakuwa na Ric.” “Oooh!
Nimesahau. Basi wewe baki na Ric, mimi nitakuwa na mama, usiwe na wasiwasi.”
Elvin alicheka. “Nakupendea hapo tu
Bella. Unaakili nzuri sana. Lakini tutaongea, wala usiwe na wasiwasi. Baada ya majuma
mawili tu tutakuwa wote au hata muda huo unaweza usifike.” Bella
alitabasamu na kumkumbatia Elvin kwa nguvu. Alilia kidogo hapo kwa Elvin,
akaondoka huku akilia.
Safarini kuelekea nchini India.
Wakiwa njiani kuelekea
nchini India, Bella alikaa karibu na daktari Mtanzania ambaye alichaguliwa
kwenda nchini India kusomea zaidi mambo ya moyo. Bella alifurahi sana.
Alimuelezea kinachomsibu Mama Mwasha na kwamba wanakwenda huko kwa ajili ya
matibabu zaidi. “Lakini hatuna mwenyeji
huko.” “Ndio mmepata mwenyeji wa kwanza.” Bella alicheka. “Ndio wewe?” “Mungu anakutanisha watu kwa
sababu.” “Umeishi nchini India kwa muda gani?” Bella alihoji. “Miaka miwili sasa, lakini nipo tayari
kurudi nyumbani, nimebakisha mwaka mmoja tu?” “Kwani wewe ulikuwa daktari wa
nini kabla ya kwenda huko nchini India?” “Unawajua ‘Physician’?” “Wale wanaotibu
kila kitu?” Bella alijibu kwa kuuliza swali. “Ewaaa. Au unaweza kusema wale ambao wanakuwa hawajasomea bado kitu
fulani maalumu au wenzetu wanasema ambao bado hawaja ‘specialize’ kwenye kitu
fulani. Sasa mimi nilipata hii nafasi ya kuja kusomea mambo ya moyo, nikaona
heri nije mapema tu kabla sijaanzisha familia.” “Kwa hiyo mpaka sasa bado huna
mke wala watoto!?” Bella alishangaa sana huku akimkazia macho kumwangalia
vizuri, yule daktari alicheka.
“Ndio natafuta sasa hivi, ili angalau tupate muda wa mwaka mmoja
wa mahusiano kabla ya hatujafunga ndoa. Nikimaliza tu shule yangu ya huko
India, nitaoa.” Bella alianza maswali yake. “Sasa
huyo mchumba unamtafutia wapi?” “Popote
tu nitakapompata. Mungu anaweza kukutanisha na mwenzi wako mahali popote pale.”
“Sasa utajuaje kama huyu ndio mke wangu wakati unakutana na wasichana wengi
sana?” Yule daktari akacheka. “Sio
kila ninaekutana naye navutiwa naye.” “Sasa mpaka sasa hivi umeshakutana na wangapi
walio kuvutia?” “Unamaswali wewe?”
“Nataka kujua, ili na mimi nikifika umri wa kutafuta mume wangu nianze
kuangalia wanao nivutia.” “Bado huna mchumba?” “Wewe!!” Bella alishtuka
sana nakujiweka vizuri, akamgeukia huku ametoa macho na kushika moyo wake.
“Mbona unashtuka?” “Hivi wewe unajua mimi nina umri gani?” “Sijui.
Kwani una umri gani?” “Mimi ni mtoto mdogo sana wewe! Sitakiwi hata kuzungumzia
mambo hayo.” Yule daktari alicheka sana. “Kweli
tena.” “Wenzako wanaolewa wakiwa na umri kama wako.” “Hao wanaharaka.”
Bella alijibu. “Wewe huna haraka?”
“Kwanza lazima unijibu swali langu ndio na mimi nitakujibu.” “Swali gani?” “Vin huwa hasahau.” Bella
alijibu na kumchanganya kidogo yule daktari.
“Nimekuuliza umeshakutana na wasichana wangapi ukavutiwa nao? Na
vitu gani vinavyokuvutia kwa msichana? Nataka kujua nikiona unaongea vitu vya
maana, nitaiga.” “Si umesema wewe haupo tayari?” “Sio kwa ajili yangu na wewe!
Ni kwa ajili ya Vin. Nataka nikikutana naye
nijidai mimi ndio mtaalamu wa hayo mambo, nimfundishe. Akiniuliza umejuaje,
namwambia nimejua tu na nitamwambia afuate ushauri wangu.” “Viini ni nani?”
“Haitwi hivyo bwana! Usiharibu jina lake. Anaitwa Vin!” “Si ndivyo
nilivyosema?” “Kama huwezi kusema Vin, basi sema Elvin, ndio jina lake lote.”
“Ooh! Kumbe ni Elvin!” “Umejitahidi
kidogo. Angalau hivyo.” Yule daktari akacheka.
“Unajua Elvin ananiona mimi nina akili za kitoto sana? Sasa wewe
nimwagie shule yote ili nikikutana naye, nimpe darasa la nguvu. Na usianze
kuniambia mambo yasiyo na maana. Kwa kuwa Elvin ana akili sana yakufikiria. Kama
ni kitu chakijinga anajua tu huu ni ujinga.” “Kwani huyo Elvin ni nani?” Ilikuwa ni kama
amefunguliwa mdomo mpaka yule daktari alijuta kumuuliza Elvin ni nani. “Wewe humfahamu Elvin Mwasha!?” Bella
aliuliza kwa kushangaa sana tena kwa sauti ya juu. “Simfahamu.” “Basi wewe ni mgeni pale Dar. Umekuja Dar mwaka gani?”
“Nimezaliwa Dar, Bella.” “Na bado humfahamu Elvin!?” “Simfahamu.” “Elvin
Mwasha! Hujawahi kusikia hilo jina?” Bella aliendelea kuuliza kwa kushangaa
zaidi kana kwamba yule daktari amesema hamfahamu Raisi wa Tanzania. “Hapana Bella.” “Basi Elvin ni..” Bella
aliongea habari za Elvin tu mpaka wanafika nchini India. Alimwaga sifa za Elvin
tu. Akilala akiamka anamshika bega yule daktari kumshtua ili amuelezee habari
za Elvin. “Unajua Elvin amesema tukikaa
huku zaidi ya majuma mawili atakuja kututembelea?” “Sijui Bella.” “Basi
atakuja. Elvin akiahidi kitu, lazima anakitimiza. Elvin….” Bella aliongea
na kuongea mpaka walipotua uwanja wa ndege wa kimataifa wa Indira Gandhi katika
mji wa New Delhi.
“Mbona unaondoka wakati umesema wewe ndio mwenyeji wetu!?” Bella alitoa macho
baada yakuona yule daktari anaondoka kimya kimya bila kuaga. “Nitawatafuta.” “Wewe ni muongo. Husemi
kweli. Utatutafutaje wakati hata namba yetu ya simu hauna. Elvin alisema…” “Naomba tupumzike habari za Elvin tafadhali
sana Bella. Please.” Yule daktari alimkatisha kabla hajaanza tena habari za
Evin, alionyesha kuchoshwa sana.
“Si
nataka kukwambia Elvin alisema mtu muongo ni hatari sana! Kwani ulifikiri
nataka kusema nini!?” “Basi naomba namba yenu ya simu, nikitulia nitawatafuta.” Yule daktari alitaka kujirudi. “Hatutaki tena!” Bella alikataa kwa
kupandisha mabega huku amekunja uso na mikono yake. Yule daktari akaanza
kucheka. “Hivi wewe Bella una miaka
mingapi?” “Mingi yakujua kuwa ulikuwa
unatukimbia na wewe sio mtu mzuri. Unaona kabisa sisi niwageni hapa nchini. Nimekwambia
mama yangu ni mgonjwa, hatuna pakwenda, wewe unasomea mambo ya moyo ambayo mama
yangu anasumbuliwa nayo, halafu ni mwenyeji hapa nchini, badala utusaidie,
unatukimbia!!” Mama Mwasha na yule nesi walikuwa wakimsikiliza Bella muda
wote tokea kwenye ndege mpaka pale uwanjani jinsi anavyoongea na yule daktari.
Mama Mwasha alikuwa ameshakalishwa kwenye kigari cha kusukumia wagonjwa, ‘wheelchair’ ameinama anacheka kimya kimya.
“Haya, samahani Bella.” Bella akacheka. “Nimekusamehe. Kwa hiyo utatuchukua utuweke nyumbani kwako?” Yule
daktari alicheka huku akimtizama Bella. “Kwani
nyinyi mlikuwa mkienda wapi?” “Hotelini halafu kesho ndio twende kwenye
hospitali ya yaa.. yaaa…” Bella alisahau jina la hospitali waliyokuwa
wakienda. “Ngoja nisome. Nimeiandika
kwenye simu yangu.” Bella alitaka kutoa simu, akairudisha “Lakini naona hamna haja ya haya yote. Hamna
sababu ya sisi kuhangaika wakati tumepata mwenyeji wetu, tena Mtanzania
mwenzetu halafu ushakaa huku zaidi ya miaka miwili, daktari wa mambo ya moyo!
Wewe utatusaidia. Au?” Yule daktari aliendelea kucheka. “Nitawasaidia Bella.” Bella alifurahi
sana. “Sasa njoo nikutambulishe kwa mama
yangu.” Bella aliwatambulisha vizuri. “Nimefurahi
kukufahamu mama.” “Asante mwanangu.” Yule daktari aliwachukua mpaka
nyumbani kwake.
Alikuwa amepangisha
vyumba vitatu yeye na wasichana wengine wawili ambao na wao ni Watanzania waliokuwa
wakisomea mambo ya IT nchini India lakini Bella alikuja kugundua hakuna hata
mmoja wao aliyekuwa akisoma kati yao, zaidi ya kustarehe na kula pesa za baba
zao nchini hapo. Walipewa chumba kimoja, wakaingiza mizigo yao yote ndani ya
chumba hicho.
“Bella wewe!” Mama Mwasha alianza kucheka mara alipoingia mle ndani ya kile
chumba. Naye Bella akaanza kucheka na kumnong’oneza, “Alitaka kutukimbia.” “Ulimchosha na habari za Elvin.” Bella
alifikiria kidogo. “Njia nzima
unamzungumzia Elvin tu, unafikiri atajisikiaje?” “Sasa yeye alitaka tuzungumzie
nini? Wakati mimi simfahamu na yeye hanifahamu, sasa si heri tuzungumze habari
za Elvin!” Mama Mwasha alitingisha kichwa. “Kweli kazi hapa ninayo.” Bella alicheka. “Unataka ulale kidogo? Eti mama yangu?” “Nijinyooshe kidogo. Mgongo
umechoka.” “Basi lala, wakati mimi nakutafutia chakula.”
**********************************
Baada yakupata msaada wa
yule daktari, waliamua kumrudisha yule nesi. Bella alisema anaweza kumuhudumia
Mama Mwasha yeye mwenyewe. Waliona ni jambo zuri, kwani walipunguza msongamano
kwenye nyumba ya watu, na gharama pia. Yule daktari aligeuka kuwa msaada mkubwa
sana. Walishirikiana na Bella kumpeleka Mama Mwasha hospitali na kufanyiwa
vipimo kwa upya kwa muda mfupi sana, tena bila shida kwakuwa yule daktari
alifahamiana na Madaktari bingwa waliokuwa kwenye kitengo hicho cha moyo. Kwa
hiyo hawakupata shida hata kidogo. Na Bella alihakikisha anamganda yule daktari
kwa kadiri ya uwezo wake kuhakikisha wanapata huduma ya haraka ili wasiendelee
kukaa pale nchini India kwa muda mrefu.
Mji huo aliokuwepo Bella
na Mama Mwasha huko nchini India wapo masaa mawili na nusu tu mbele ya
Tanzania, na kwa Dubai ambapo Eno alikuwepo ilikuwa ni nyuma ya Lisaa tu kwa
India, kitu kilichorahisisha mawasiliano kati yao. Walipiga simu kila wakati
kujua linaloendelea nchini India. Masikio na akili ya familia hiyo ya Mwasha,
vyote vilikuwa nchini India kwa Bella, wakifuatilia hali ya mama huyo kwa
karibu sana. Kila wakati Bella alikuwa na kazi ya kuwatuliza wanaume hao watano
akiwemo Mzee Mwasha, akiwaambia mama Mwasha anaendelea vizuri.
**********************************
“Sasa saa
hizi watakuwa wameenda wapi mama jamani!? Nilikwambia uwe unamwangalia Bella.
Bado anaakili za kitoto, huyo daktari asije.., yaani aka…” Elvin alipiga simu
kuwasalimia, lakini aliambiwa Bella ametoka na daktari. “Unawasiwasi
wa bure Elvin mwanangu. Huyo Bella anaweza kujiangalia yeye mwenyewe. Huyo
daktari mwenyewe analala hoi kwa usumbufu wa Bella.” “Kwani mnaishi na huyo
daktari kwenye nyumba moja? Nilifikiri anawasaidia tu na nyinyi mnaishi
hotelini! Kwani pesa haikutosha? Kwa nini sasa mama na wewe umekubali kuishi na
huyo daktari jamani! Kwa hiyo wameshakuwa na mahusiano ya karibu kiasi cha
kwamba Bella ndio amemzoea hivyo? Na yeye anamtania?” “Elvin? We Elvin! Unajua
hata hujaniuliza hali yangu naona unaulizia habari za Bella tu na huyo daktari
tokea ulipopiga simu?” “Samahani mama. Nahofia asije akamchezea Bella. Bella….”
“Unarudi kule kule. Hatuwezi kuongea jambo jingine mbali na Bella? Eti Elvin
mwanangu?” “Basi mama. Unaendeleaje?” Mama Mwasha akaanza kucheka.
“Unacheka nini sasa mama jamani? Namuhofia sana Bella. Lakini
tuendelee na hali yako. Wamekwambiaje?” “Nahitajika upasuaji, lakini siunajua
wenzetu huku hawakuchani kwa nje? Watatoboa tundu kidogo, wataningiizia tu
vimirija na kurekebisha kila kitu.” “Sasa itabidi tuje.” Elvin alishtuka kidogo. “Wamesema tusiwe na wasiwasi
kabisa. Ni kitu cha muda mfupi. Ila itabidi nilale hapo hospitalini kwa siku
mbili kuniangalia kisha wataniruhusu. Halafu baada ya siku tano natakiwa kurudi
kumuona dokta.” “Mbona wanawaweka sana hivyo!?” “We Elvin!? Hivi unajua hata
week moja hatujamaliza tokea tuje huku? Sidhani hata week mbili tutamaliza
huku. Naomba uwe mvumilivu.” “Sio kwa ajili yangu mama, ni kwa ajili yako.” Mama Mwasha alijua
kabisa anayehofiwa ni Bella na huyo daktari. Wivu ulishaanza kumsumbua Elvin na
mama yake alijua.
“Mimi nipo
kwenye matibabu Elvin, usiwe na wasiwasi.” “Sawa. Naomba akirudi Bella mwambie
anipigie.” “Si ni usiku sana huko? Ungelala mtaongea kesho.” Mama yake alimchokoza
Elvin. “Hapana mama, kwanza nyinyi ndio mpo mbele masaa mawili na nusu,
nashangaa kwa nini mpaka sasa hivi hajarudi nyumbani! Naomba akirudi mwambie
anipigie nitasubiri.” “Haya baba. Usiku mwema.” Elvin akakata simu.
**********************************
Mama Mwasha alifanyiwa
matibabu mazuri sana. Daktari aliyekuwa akimuhudumia alipoona anaendelea
vizuri, waliruhusiwa moja kwa moja. Walimshukuru sana yule daktari kwa
kuwatunza pale nyumbani kwao, wakaanza kupanga safari ya kurudi nyumbani. “Heri turudi tu mama. Naona Elvin
anawasiwasi kweli na wewe. Kila wakati anapiga simu.” Mama Mwasha
alicheka tu. Kila alipokuwa akimsikiliza Bella na Elvin, aliwaona wamejawa
mapenzi mazito sana ndani yao, lakini Bella alijawa na utoto mwingi. “Ni kweli Bella.” Walikata tiketi ya
kurudi, kisha Bella akampigia Elvin simu kumpa taarifa za kurudi kwao nyumbani.
“Sasa kwa
nini hamjakata tiketi yakuondoka kesho Bella?” “Huyu dokta amesema amepata za
kuondoka baada ya kesho kutwa.”
Elvin
alizidi kuchukia. “Mimi naenda kuzibadilisha.”
“Hamna haja Elvin.” “Kwa nini? Au unafurahia kuishi na huyo daktari huko?” “Vin
jamani! Naepuka usumbufu kwako.” “Kwangu sio usumbufu, nataka mrudi nyumbani
Bella.” “Tutarudi. Hata hivyo itamsaidia mama kupata muda wa kupumzika zaidi.”
“Nimeongea na mama, amepona Bella. Wewe ndio unataka kukaa huko. Umeshaanza
kumpenda huyo daktari?” “Hapana Elvin jamani! Basi nenda kabadilishe hiyo
tiketi tuondoke kesho. Kwanza mimi mwenyewe nina hamu ya kukuona Vin.” “Mbona
sasa hutaki kurudi nyumbani?” “Nataka, lakini si ndio nilikuwa nikimuuguza
mama? Nikwambie kitu?” “Nini?” “Nimekununulia zawadi nzuri. Najua utapenda.
Nilimuomba huyu daktari anizungushe madukani mpaka usiku kukutafutia zawadi
wewe Vin.” Elvin alitulia kidogo.
“Umekasirika
Vin?” “Hapana, asante kwa zawadi. Na mimi ninahamu na wewe Bella. Nataka urudi
nyumbani.” “Basi nenda kabadilishe tiketi kama utapata ya siku ya karibuni.
Nitafurahi sana kukuona Elvin.” “Ukirudi nimepanga tutaenda mapumzikoni na
Ric.” Bella akafurahia hilo
wazo. “Wapi?” “Ni
Siri. Utapaona ukifika huko.”
Mama
Mwasha alikuwa akiwasikiliza Bella na Elvin wakati wakiongea. Ulikuwa ni wakati
wa usiku wamelala kitanda kimoja na Bella. Waliongea kwa muda mrefu Bella
akicheka taratibu huku akimpa maneno mazuri Elvin, mpaka akatulia.
Uwanja wa
Ndege wakimsubiri Mama Mwasha & Bella.
Familia hiyo ya Mwasha wote
walikuwa uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere, mapema sana wakimsubiri mama yao
na Bella wawasili kutoka nchini India. Vilijaa vicheko na utani pale uwanjani
kwani na Eno naye alikuwa amefika siku hiyo hiyo kutoka nchini Dubai. Wakati
wamesimama wakiongea ndugu hao, Diva naye akawasogelea na kujaribu kusalimia
kila mmoja kwa kumpa mkono kama sio yeye. JJ aliingiza mikono yake yote miwili
mfukoni na kubaki akimwangalia huku Diva amebaki amemnyooshea mkono. “Nakusalimia tu JJ.” “Unataka kushikwa na
wanaume wangapi wewe? Kwaza unataka nini hapa?” JJ alimuuliza kwa ukali
kidogo, huku baba yake na wadogo zake wakiwa kimya wamegeukia pembeni. “Niliwasikia baba na mama wakiongea jana
usiku kuwa Mama Mwasha anarudi leo.” Diva alijibu kwa upole. “Kwa hiyo!?” JJ aliuliza kama
akimshangaa. “Ndio na mimi nimekuja JJ?”
“Umesikia swali langu lakutokea mwanzo au unataka kuharibu hali ya hewa hapa?”
Diva alitulia kidogo. “Nia yangu ni nzuri
JJ. Nataka kumsalimia mama na kujua anaendeleaje.” “Acha kunifanya mimi mtoto
mdogo wewe! Si ulikuwa unakataa tusimpeleke kutibiwa? Ameugua akihitaji msaada
wako ukashindwa hata kuwa mnafiki kidogo tu! Sasa hivi unasema nini? Ondoka
Diva.” Diva alitulia. “Diva!”
“Nimebadilika JJ.” “Unataka nini kwangu wewe?” “Naomba kurudi nyumbani.” “Utalia
Diva wewe! Ondoka.” “Naomba basi kuja kuona watoto.” “Huyo bwana wako hazai?”
“Nimeshaacha mambo hayo JJ. Sasa hivi nimetulia.” “Ujue unawazimu Diva wewe!
Hata mwezi haujaisha, unasema umetulia? Ondoka Diva usitafute matatizo wewe.”
“Kweli nimebadilika JJ. Na kazi kule
nimeacha kabisa, natafuta kwengine.” “Kwengine au bwana mwingine? Ondoka Diva.
Tafadhali usiendelee kuniudhi.” “Basi JJ.” Diva akatulia. “Ondoka sasa.” “Naomba basi nimsubirie mama
nimuombe yeye msamaha.” “Ondoka Diva.” “Basi naomba umruhuhusu Mlinzi
anifungulie geti pale nyumbani angalau niwaone watoto wakati wewe upo kazini
kama hutaki kuniona tena.” “Na safari hii ukirudi tena pale nyumbani,
kitakachokupata usinilaumu. Nimebadili kampuni ya ulinzi. Vitu vyako vyote
nimevipeleka kwenu. Huna ulichobakiza pale kwangu. Nakushauri usirudi tena.”
“Na watoto?” “Ulikuja kwangu na watoto?” “JJ jamani!” “Nenda kanishitaki
mahakamani. Vyombo vya sheria si vipo? Nenda kadai haki yako mahakamani kama
kuna unachokidai kwangu. Usinitafute tena.” Diva alianza kulia.
“Ondoka Diva. Usiharibu zaidi ya ulivyoharibu. Mama anafika sasa
hivi, sitaki akute hii hali hapa. Kama umeshindwa kuniheshimu, naomba
umuheshimu mama yangu.” “Nakuheshimu JJ.” “Basi ondoka.” “Uliniambia
utanitafuta JJ. Basi nasubiri. Mimi nitakuwa nyumbani.” “Uwe unaishi nyumbani kwenu, au uamue kuolewa tena, au kuzunguka na
mabwana zako, hainihusu tena.” “Nimebadilika JJ.” “Ondoka Diva.” Diva alianza kuondoka akasimama. “Naomba unisalimie watoto.” JJ akageuka kumpa mgongo, hakutaka
kuendelea kuongea naye tena, Diva alivyoona vile akaondoka.
**********************************
Hakuwahi kumuona JJ wa
vile tangia wanaoana. Alishazoea kumkosea na yeye JJ ndiye aliyeomba msamaha na
akitaka yaishe. Diva aliishi na JJ kwa kiburi sana. Alishtuka kuona siku
zinazidi kwenda bila JJ kumtafuta na huko shuleni pia aliwaambia Diva
haruhusiwi kusogelea watoto. Na kwa kuwa hata huko shuleni kwa wanae hakuwa
akielewana na mwalimu hata mmoja, haikumsumbua JJ kumdhibiti. Walimu walifanya
kama walivyoagizwa na JJ. Kwanza JJ ndiye aliyekuwa akihangaika na mambo ya
shule ya watoto wake. Sio Diva. Yeye alifika pale kukosoa hiki au kile. Akilalamikia
hiki juu ya wanae au kile, mpaka alifahamika pale shuleni.
**********************************
Baada ya muda kidogo
walishangaa kuona wale kina mama na waume zao pamoja na watoto wao wamefika
pale uwanjani pia. Mwasha aliwasalimia wazee wenzake, na kuwashukuru kwa kufika
pale. Walikuwa na maua mengi sana, kama kumpa Mama Mwasha pole kwa kuugua. Ndege
ilitua uwanjani hapo na kushangaa Mama Mwasha akitembea bila hata kushikwa
mkono na mtu. Kila mtu alikuwa akishangaa jinsi alivyonekana na uzima mkubwa
tofauti alipokuwa anaondoka. Bella alimkimbilia Elvin na kumkumbatia kwa muda
mrefu sana akilia. “Nimefurahi kukuona
Bella.” “Nilikuwa na hamu na
wewe, Vin!” “Hunishindi mimi.” Waliendelea kuongea
huku wamekumbatiana. Hakuna ambaye hakuwaona jinsi walivyokuwa wamekumbatiana
kwa mapenzi mazito. Irene alibaki ameinama. Eric alifurahi sana kumuona dada
yake. Bella alimkumbatia Eric kwa furaha sana. “Miss you Bella.” “Me too.” Bella alisalimia kila
mtu huku amemkumbatia mdogo wake na kumbusu kila wakati.
Kila mtu alimpa maua
Mama Mwasha, akabaki amebeba maua mengi sana. “Haya maua anastahili kupewa Bella jamani. Alikuwa halali huyu mtoto
kwa kunihudumia. Sio kipindi nipo hapa Tanzania tu ambapo watu walikuwa
wakinionea kinyaa, sababu ya kujisaidia hovyo, lakini hata nilipokuwa naye
India. Bella amenitunza huyu mtoto! Mungu na yeye atamlipa. Tumeondoka pale
hospitalini madaktari wote wanatufahamu majina sababu ya Bella. Alikuwa hatulii
akiona hali yangu sio nzuri, au kama madaktari wakitoa maelezo ambayo
hatujaelewa. Bella alikuwa akifuatilia mpaka tutakaporidhika. Namshukuru Mungu kwa ajili ya Bella. Sikuzaa
mtoto wa kike, lakini naona Mungu ametuletea Bella, amekuwa kama mtoto wangu
niliyemzaa.” Mama Mwasha alimwaga sifa za Bella palepale uwanjani mbele ya
marafiki zake wote, wanae na Mumewe.
“Asante sana Bella.” Watoto wote wa Mama Mwasha walimsogelea Bella
na kumpa mkono. Mzee Mwasha alimkumbatia Bella. “Sasa unahitaji kwenda mapumzikoni.” Bella akacheka. “Umeona baba eeh?” Bella aliuliza huku
akicheka. “Mimi nitampeleka Bella.”
Eli alichokoza. “Elvin ameshaandaa mpaka
sehemu ya kwenda, kwa hiyo Elvin ndio atawapeleka Bella na Ric wakapumzike.”
“Watu mnanipinga! Basi na mimi naandaa sehemu yangu ya kwenda na Bella,
wakirudi tu na sisi tutaenda. Au unasemaje Bella?” Wote walianza kucheka.
Taratibu walimuona Irene, anaondoka na kurudi kwenye gari, akifuatwa na
marafiki zake nyuma. Wale wakina mama na waume zao pia waliaga, nakuwaacha pale
uwanjani Mzee Mwasha na familia yake wakitaniana na kucheka. Walirudi nyumbani
wakiwa na furaha sana.
**********************************
Walialikwa watu baadhi
jioni hiyo, kwa ajili ya tafrija ndogo ya kumshukuru Mungu kwa ajili ya kupona
kwa Mama Mwasha. “Kama wageni
wanakuja usiku, naomba mimi nikalale kidogo. Lakini nina maongezi na Elvin
kidogo. Unifuate chumbani ukishamalizana na Bella.” “Sawa mama.” Wote
walikuwa wakijishugulisha kwa maandalizi ya tafrija ya usiku huo. Kasoro Elvin,
Eric na Bella walikuwa wakiongea na kucheka. Kila mmoja kati ya watoto hao
wakiume wa Mama Mwasha walijua kazi zao, kwa hiyo waligawana na kufanya kazi
bila tatizo. “Basi na mimi naenda
kulala.” “Twende wote Bella.” Eric na yeye akasimama. “Unataka kulala?” “Nitakuwa nacheza game pale pale kitandani
utakapokuwa umelala wewe. Nina hamu na wewe Bella.” Bella akacheka. “Haya twende na mimi nina hamu na wewe
Ric. Nimekuletea zawadi.” “Game nyingine tena?” Bella na Erica waliendelea
kuongea huku wakiongozana chumbani, ndipo Elvin alipoenda kuongea na mama yake.
**********************************
Elvin alimkuta baba yake
chumbani kwao. “Funga mlango kabisa.”
Elvin alishtuka kidogo. “Kwema mama?”
“Kwema lakini kuna kitu nataka nikwambie.” Elvin alimwangalia baba
yake na mama yake, wote aliwaona hawana sura za furaha. Elvin aliogopa kidogo. “Kaa hapo kwenye kochi.” “Mbona unanitisha
mama! Kuna nini?” Mama Mwasha alitulia kidogo. “Unajua kama Bella ni mjamzito?” Elvin alistuka sana. “Hapana.” “Tena ana mimba kubwa tu.” “Yeye
ndio amekwambia?” “Ndio maana
nakwambia wewe Elvin. Bella hajielewi kabisa. Anaweza akanilalamikia kidogo tu
juu ya anavyojisikia, lakini hajui kama ni mimba. Yaani kwa kifupi Bella
hajielewi hata kidogo. Nilitaka kumwambia wakati tupo India, nikaona anaweza
kuchanganyikiwa na wewe haupo wakumtuliza. Nikaamua nimwache, nije nikwambie wewe unayemuwezea, ili utafute jinsi
ya kuongea naye.” Elvin aliinama. “Mungu
wangu!” Elvin alisikika akiwaza kwa sauti.
“Kwani mbali na Mzee Masha, alishakuwa na mwanaume mwingine?” Mama Mwasha akauliza. “Hapana. Bella hakuwahi kuwa na mwanaume
kabla na baada ya Mzee Masha.” Elvin alitulia kidogo. “Mungu wangu!” Elvin aliendelea kulalamika.
Mzee Mwasha aliamua
kuingilia kati. “Elvin! Nimemueleza mama
juu ya nia yako yakutaka kumchumbia Bella. Na kwamba hata pete ulishanunua
ulitaka usiku wa leo kwenye tafrija ndio umvishe. Sasa baada yakujua hilo,
tunataka kujua msimamo wako bado utaendelea na swala la uchumba?” “Mungu
Wangu!” Elvin alisimama akiwa
ameweka mikono kichwani akionyesha kuchanganyikiwa zaidi.
**********************************
Harakati
zote za kuandaa pete ya gharama sana kwa ajili ya kumchumbia Bella, zinaingia dosari kwa
taarifa za ujauzito wake. Tena mtoto wa Masha!
Je, Nini Kitaendelea? Bado Elvin
atachumbia au ndio basi tena?
Masha atafanyaje akisikia Bella ni mjamzito?
Ulimwengu je?
Usikose muendelezo kujua kitakacho Jiri kwa Bella na ndoa ya JJ pia.
0 comments: