Story
akati Bella anajitahidi
kutulia, kwa mbali masikio yake yalianza kusikia mziki wa taratibu sana,
alihisi ni nyimbo za kumuabudu Mungu kwa lugha ya kingereza. Mawazo ya Bella
yalianza kutulia sehemu moja na kufikiria mahali alipokuwa amesikia zile
nyimbo. Akakumbuka ni kwenye gari lao. Mat alikuwa akipenda sana kuziweka
kwenye gari ambalo ilikuwa taksii. Kumbukumbu zikamjia Bella, kuwa anajukumu la
Eric, na lazima ajikomboe kwenye mikono ya Masha. Akajua ile kazi inaweza kuwa
msaada kwake. Ikabidi kuanza kutulia na kurudisha mawazo pale, akanyanyua uso
kwa mara ya kwanza, akakuta bado wakimwangalia.
My Past - Sehemu Ya 5.
|
W
|
akati Bella anajitahidi
kutulia, kwa mbali masikio yake yalianza kusikia mziki wa taratibu sana,
alihisi ni nyimbo za kumuabudu Mungu kwa lugha ya kingereza. Mawazo ya Bella
yalianza kutulia sehemu moja na kufikiria mahali alipokuwa amesikia zile
nyimbo. Akakumbuka ni kwenye gari lao. Mat alikuwa akipenda sana kuziweka
kwenye gari ambalo ilikuwa taksii. Kumbukumbu zikamjia Bella, kuwa anajukumu la
Eric, na lazima ajikomboe kwenye mikono ya Masha. Akajua ile kazi inaweza kuwa
msaada kwake. Ikabidi kuanza kutulia na kurudisha mawazo pale, akanyanyua uso
kwa mara ya kwanza, akakuta bado wakimwangalia.
“Naitwa Enabella.” Aliongea kwa sauti ya chini kidogo, lakini
ilisikika. Mzee Mwasha akatoa tabasamu. “Ndio
umeshamaliza utambulisho wako?” Bella alifikiria kidogo akaamua kurudia
tena. “Naitwa Enabella. Lakini wamezoea
kuniita Bella.” Alitulia kidogo kisha akaongeza. “Nina elimu ya ‘IT’. Lakini Sina cheti chochote, ila nilisoma kwa miaka
miwili, ninao utaalamu kidogo.” “Kwa nini huna vyeti?” Elvin akamuuliza.
Bella alifikiria kidogo, akainama kwa muda kisha akaendelea. “Nilipata matatizo yaliyonisababishia
kutofanya mitihani. Lakini nilihudhuria madarasa yote, nilipata elimu kama
wengine, kasoro ile week ya mwisho ya mitihani ndipo sikuweza kuhudhuria chuoni
kufanya mitihani yangu ya mwisho.” “Ulimaliza
mwaka gani? Au ulitakiwa kumaliza mwaka gani?” Elvin aliendelea kuhoji. “Mwaka huu mwezi wa tano.” Bella
alijibu.
“Una umri gani Enabella?” Mzee Mwasha akamuuliza. “Miaka 20 sasa.” Walinyamaza kidogo wakaangaliana. Wasiwasi
ukamwingia Bella. “Lakini naweza
kujituma.” Bella aliongeza kwa unyenyekevu sana. “Sijui kama unajua hii kampuni inahusika na nini!?” Elvin
alihoji. “Sifahamu.” “Tunaagiza mabomba
kutoka South Africa na kuyauza hapa nchini na nchi za Africa Mashariki. Sasa
kwa taaluma uliyonayo unafikiri unaweza kufanya kazi gani hapa?” Elvin
aliuliza tena. Bella alifikiria umuhimu wa ile kazi kwake na kwa mdogo wake,
ilimlazimu kufikiria harakaharaka sana.
“Labda niulize swali.” Bella alikaa vizuri. “Karibu.” Elvin akajibu. “Mnatumia
mfumo gani katika kuendesha biashara zenu hapa ofisini kwenu? Nikimaanisha
mnatumia kompyuta au mnaandika kwenye vitabu tu?” “Tupo kwenye mabadiliko sasa.
Kutoka kwenye mfumo huo wazamani wa kuandika na kuingiza kazi zote kwenye
kompyuta. Kuna mtaalamu huwa anakuja
kila mwishoni mwa juma kuifanya hiyo kazi.” Elvin alijibu.
“Naweza kuwasaidia.” Bella alijibu huku akiwaangalia wote kwa zamu. “Mkinipa mimi hiyo kazi, nitaomba muda
kidogo kupitia kazi zenu zote, nakujua mnachofanya, ndipo nitakapoweza
kuwasaidia kutengeneza mfumo ambao ni rahisi kwa wafanyakazi wenu wote, na
nyinyi wenyewe, na pengine naweza nikatoa ushauri pia.” Bella aliwatizama
tena usoni kila mmoja wao. Ujasiri ulirudi, akaonekana akijieleza kwa uhakika.
“Nikielewa kazi zenu, yaani nikafahamu hii kampuni na jinsi
mnavyofanya kazi, hamtakuwa na haja yakunifuatilia kila mara. Nina uwezo
wakujituma mwenyewe, na kufanya kazi vizuri.” Bella aliongezea. Mzee
Mwasha alionyesha tabasamu usoni lililompa tumaini Bella.
“Unataka kuanza kazi lini?” Elvin
akahoji. “Wakati wowote mtakao nihitaji,
nitakuwa tayari. Sina kitu ninafanya kwa sasa, nipo tu nyumbani.” Elvin
alitulia kidogo. “Kwa hiyo hata tukikuita
kesho, unaweza kuanza kazi.” “Ndiyo.” Bella akajibu. “Unatarajia mshahara wa kiasi gani?” Elvin alimuuliza. Japokuwa
alihitaji sana hiyo kazi, lakini hakuwa amejua hata watu huwa wanalipwa
mishahara kiasi gani. Alishazoeshwa kupewa mahela na Mzee Masha. Akaogopa
kabisa kutaja mshahara wake. Alibaki kimya akifikiria. Na upande wa waajiri
wake, walimuona Bella ni wa garama sana. Kuanzia mavazi yake, yeye mwenyewe
alivyojiweka na kujiuza pale kwenye usahili, kidogo walibabaika. Chumba kizima
kilijaa harufu ya manukato yake.
“Eti Enabella?” Mzee Mwasha aliuliza. “Sifahamu huwa wanalipaje mishahara. Sijawahi kuajiriwa.” Bella
alijibu kwa upole kidogo. Wote walinyamaza kimya. “Au nianze kwanza kazi, halafu mnilipe kwa utendaji wangu?” Bella alitoa
wazo huku akiuliza, baada yakuona kumezuka ukimya. “Huyo mtu anayekuja kila mwisho wa week kutusaidia kazi, tunamlipa pesa
nyingi sana, tena anakuja mara moja kwa week tu. Kwa hiyo kama utaweza kufanya anachofanya,
utakuwa umetusaidia sana kukata matumizi, na kuanzia hapo tutajua kiasi gani
cha kukulipa.” “Sawa.” Bella akakubali bila shida.
“Ulitaka kuja kuanza kazi siku hiyo anayokuja yeye ili uone anachofanya?” Elvin akamuuliza tena. “Naomba kama naweza kuanza kabla ya kukutana
na yeye, nianze tu. Ili nielewe jinsi mnavyofanya kazi zenu nyinyi kwanza. Sio
lazima mkanilipa, hii itakuwa kwa manufaa yangu mimi mwenyewe, halafu
atakapokuja huyo mtu, akiwa anafanya hizo kazi, nitakuwa angalau nina uelewa ni
kitu gani anafanya au anatakiwa kufanya.” Bella aliweka msisitizo. “Wazo zuri sana Enabella. Besi unaweza
kuanza kesho.” “Nije saa ngapi?” Bella akauliza. “Kuanzia saa 12:30 asubuhi ofisi zinakuwa wazi. Mimi ninakuwepo.”
Elvin akajibu. “Hapo itakuwa mapema sana.
Sitaweza. Labda kuanzia saa nne asubuhi nitakuwa nimefika.” Wote
walimwangalia kwa mshangao kisha Mzee Mwasha akacheka kidogo. “Au nitakuwa nimechelewa sana?” Bella
akauliza kwa upole.
“Asubuhi huwa nachelewa sana kuamka. Lakini saa nne naweza kujitahidi
kuwa nimefika.” Bella aliongea kama mtoto ambaye hana majukumu yanayomkabili.
Alipoona wote wapo kimya, aliingiwa na hofu. “Lakini pia naweza kufika saa 12:30 asubuhi, au muda wowote mtakao
nipangia, nitakuja.” Bella aliongea kwa upole kidogo, akijirudi. “Hamna shida. Wewe njoo huo muda utakao
weza.” “Asanteni sana.” Bella alishukuru. “Karibu sana Enabella. Kesho utakapofika, tutakuzungusha humu ndani na
kukutambulisha kwa watu.” “Sawa.” Bella alijibu kwa kifupi na kusimama. “Nitarudi kesho.” “Karibu sana.” Mzee Mwasha
alisimama na kumpa mkono lakini Elvin alirudisha macho yake kwenye faili na
kuendelea kuandika. Bella akatoka. Bado dereva alikuwa akimsubiri nje ya ofisi
hizo. Alimrudisha nyumbani akiwa amefurahi sana.
*********************************************
Alimkuta Mzee Masha
akimsubiri. Alimuelezea kila kitu. “Nilikuwa
naogopa kweli.” “Wasingeweza kukunyima kazi.” “Kwani uliwaambia mimi ni nani
kwako?” Bella aliuliza lakini alimuona Mzee Masha amebadilika sura,
akaogopa. “Wewe si ulitaka kazi?” “Ndiyo
T. Na ninakushukuru.” Bella alishaingiwa na hofu, alijibu kwa
kujinyenyekeza sana, ili usiku ule usiwe mbaya kwake. Walikaa kimya kwa muda,
kisha Bella akaamua kuaga akawahi kulala. “Nataka
niwahi kulala, ili kesho niamke mapema niwahi kazini.” “Hata kazi yenyewe hujaanza
umeanza kuniona mimi mzigo!? Unaniachaje hapa sebleni peke yangu? Ndio maana
wanaume wengine hawataki wake zao wafanye kazi.” Bella alijirudisha kukaa
pembeni ya Mzee Masha taratibu. “Nitakusubiri
T.” Mzee Masha alimwangalia kwa muda na kurudisha macho yake kwenye tv.
Bella aliumia sana moyoni, lakini hakuwa na jinsi. Ni lazima afanye kila
anachoambiwa. Alijikuta wanalala saa nne ya usiku.
“Bella
aanza kazi.”
Bella aliamka asubuhi na
mapema akiwa na furaha sana moyoni. Ni kama aliyekuwa akianza maisha mapya.
Alimuacha Mzee Masha kitandani, akaingia kuoga na kutoka kuandaa kifungua
kinywa. Alirudi chumbani kumuamsha Mzee Masha, wakapata kifungua kinywa kwa
pamoja, Mzee Masha akaanza kumng’ang’ania tena. “Nitachelewa kazini T. Kwa nini tusiendelee jioni tukirudi?” Mzee
Masha alimchapa kibao kwa nguvu. “Kazi
nimekutafutia mwenyewe, halafu unasema nini? Yaani hiki ninachotaka kufanya
sasa hivi ni ujinga? Sikiliza Bella, kazi yako ya kwanza ni hapa nyumbani, na
huko kazini ni ya pili. Umenielewa.” “Ndiyo.” Bella alijibu huku ameshika
shavu lake lililokuwa likiwaka moto kwa kibao cha nguvu alichokuwa amepigwa.
“Nikukute chumbani ukinisubiri.” Mzee Masha alimuamuru
Bella. Huku akilia, Bella alirudi chumbani akavua nguo zote akapanda kitandani
na kujifunika shuka. Alikaa pale akimsubiri Mzee Masha, aliyekuwa akiangalia
taarifa ya habari ya CNN, asubuhi hiyo. Baada ya kama dakika 45, ndipo
alipoingia chumbani. Alikaa na Bella hapo kitandani karibu lisaa lizima.
Alipomaliza, Bella alisimama kwenda bafuni. Alikaa bafuni akilia sana, mpaka
alipomsikia Mzee Masha akiingia bafuni, akanyamaza.
“Hata ukiingia kazini saa nne, hakuna atakayekufukuza kazi.
Jiandae, dereva yupo nje anakusubiri.” Mzee Masha alikuwa amesimama ndani ya bafu hilo
akiongea na Bella. “Unanisikia lakini?”
“Ndiyo, nimesikia.” Bella alioga harakaharaka, akarudi chumbani kuvaa nguo
zake tena. “Uwe na siku njema T.”
Bella aliaga. “Asante.” Bella
aliingia kwenye gari, lakini alishindwa kujizuia. Aliinama nakuanza kulia sana.
Alilia mpaka dereva alipomwambia wamefika. Alishindwa kushuka kwenye gari, kwa
wakati ule. Alibaki akilia kwa muda, mpaka alipotulia. Kwa bahati mbaya, macho
yalishakuwa mekundu sana, hata rangi ya sura yake ilikuwa imebadilika. “Asante.” Bella alimshukuru dereva,
akashuka kuingia ofisini.
*********************************************
Alimkuta sekretari
kwenye meza yake. “Nimeambiwa ukifika
uende kwenye ofisi ya Elvin. Ni ule mlango wa pili kulia.” “Asante.”
Bella alishukuru na kuondoka. Kabla hajaingia ofisini kwa Elvin alijitahidi
kuvuta pumzi mara kadhaa, ndipo alipogonga mlango wake. “Samahani nimechelewa.” Bella aliwahi kabla ya salamu. Ilishakuwa
saa nne asubuhi. “Karibu.” Bella
hakutaka kabisa kumwangalia machoni. “Karibu
kiti ukae.” Bella alikaa mbele ya meza ya Elvin, huku ameinama. Walikaa
kimya kwa muda, Elvin akimwangalia Bella, na Bella akiwa bado ameinama.
“Kitu cha kwanza ulitakiwa kufanya ilikuwa ni kusalimiana au
kufahamiana na wafanyakazi wengine. Lakini muda huu, wengi wameshatoka,
watarudi jioni.” Bella alinyamaza. Elvin alisimama na kutoa maji ya kunywa kwenye
friji ndogo iliyokuwepo hapo ofisini. Akayafungua na kuyaweka mbele ya Bella. “Karibu maji.” “Asante.” Bella alijibu
kwa sauti ya chini bila hata kumtizama. “Sio
wafanyakazi wote wanafika saa 12:30 asubuhi. Ni wale watu wanaofanya stoo, na
madereva. Mizigo huwa inafika hapa asubuhi sana, na wanao safirisha nchi za
jirani pia, huwa wanapenda kuondoka alfajiri sana. Huwa napenda kuwepo hapa ili
nisimamie mimi mwenyewe. Lakini wafanyakazi wengine, wanatakiwa saa mbili
kamili wawe wamefika hapa, ofisini.” Bella alinyamaza, akifikiria kama
kweli ataweza kufika pale katika mida hiyo. Alijua anajukumu la Mzee Masha,
ambalo hawezi kulikwepa. Alibaki kimya akifikiria chakufanya.
“Sidhani kama nitaweza kuwa nafika hapa kwa muda huo.” Bella alijikaza na
kumwangalia Elvin. Elvin alibaki akimwangalia jinsi macho yake yalivyo mekundu
na yalishavimba kidogo. “Ungependa kuanza
kazi kesho? Unaweza kurudi nyumbani ukapumzika mpaka kesho.” Bella alibaki
akifikiria. Alijua maisha yake hayawezi kubadilika kwa siku moja au kwa
kujionea huruma pale. “Hapana. Naomba
nianze tu leo. Nitajitahidi kuwa namaliza kazi zote utakazokuwa unanipangia
siku hiyo kabla sijaondoka. Hata kama nitafika kwa kuchelewa, nitajitahidi
kumaliza kazi zangu zote. Sitalaza kiporo.” “Ni sawa tu. Kipo choo humuhumu
ndani ya hii ofisi.” Akimaanisha aingie akaoshe uso. Bella alielewa.
Akasimama na kuingia chooni. Aliloweka uso wake kwenye viganja vyake
vilivyokuwa na maji ya baridi, mpaka alipotulia kabisa. Akajikausha, nakutoka. “Asante.” “Karibu. Sasa twende ukaanzie
upande wa stoo. Huko utakutana na mtu ambaye ndiye anapokea mizigo yote na
kugawa kila siku. Ni kijana mzuri sana, atakuelekeza vizuri tu.”
Waliongozana mpaka upande wa stoo.
*********************************************
Ni kweli, yule kijana aliyekutana naye kule
stoo alikuwa ni mnyenyekevu lakini mcheshi sana. Alifahamika kwa jina la ‘Joo’.
Alimkaribisha Bella. Bella alianza siku yake vibaya sana, hakuwa na furaha hata
kidogo. Lakini hakutaka matatizo yake yaingilie kazi yake. Alijitahidi kuelewa
kila alichoelekezwa na kuuliza maswali machache, baada ya muda akawa
ameshaelewa kila kitu na kugundua matatizo mengi sana pale. Bella alikuwa na
kidaftari chake, akawa anaandika kila kitu.
“Naenda kula dada Enabella. Utataka tuongozane.” “Hapana. Mimi
sitatoka. Naomba tu mimi niendelee na kile ulichokuwa ukikifanya wewe, ili
ukirudi tuwe tumepunguza kazi.” “Sawa.” Joo alimuacha Bella akiwa amemuelekeza kitu cha
kufanya. Alikuwa na mrundikano wa kazi nyingi sana, za miezi mingi iliyopita.
Bella alishangaa wanawezaje kufunga mahesabu ya siku au hata mwezi kama huyu
mtu wa stoo anakuwa hajakamilisha kazi yake. Alibaki pale kwenye ofisi ya stoo
akifaya kazi bila hata kunyanyuka. Alifurahia ile kazi, kwani kwa mara ya
kwanza aliweza kupata kitu chakufanya na kufikiria mbali na Mzee Masha. Alibaki
akiandika kwa muda, na kupangilia ile kazi vizuri sana.
“Pata mapumziko, ule kidogo.” Elvin alikuwa amemletea
chakula. “Sitaweza kula. Asante.” Bella
alimgeukia. “Kwa nini?” “Tumbo langu
limejaa sana gesi. Siwezi kuingiza kitu chochote humo ndani. Itakuwa ni kama nina
jiadhibu zaidi. Asante sana.” Bella aligeuka na kuendelea kuandika. “Vipi unaonaje kazi ya hapa?” Bella akatulia
kidogo. “Naruhusiwa kutoa maoni yangu?
Najua ni mgeni kabisa, lakini..” Bella alisita. “Sema tu.” “Nimeona mnaviporo vingi sana. Na ninahisi pia inachangiwa na
mfumo wa utendaji kazi wenu, unamuia vigumu Joo kumaliza kazi kwa wakati. Kwa
nini msitumie kompyuta, mkanunua program ambayo Joo, akiwa anajaza hapa, hata
kama muhasimu akitaka kufunga mahesabu yake wakati wowote anaona kilichopo
stoo, bila kuzungusha hizi vocha? Kwa namna hii ni rahisi sana kupotea. Hata
wewe mwenyewe itakurahisishia kujua nini unacho stoo na nini hauna. Na unatakiwa
kuagiza kwa wakati gani. Sijui unanielewa? Yaani mnaweka utaratibu ambao
wahusika wanaweza kuona kila kitu wanachokitaka, wakiwa kwenye kompyuta zao,
ofisini kwao. Tena kwa urahisi na haraka. Joo anakuwa hana kazi yakuzunguka
maofisini na vocha zote hizi. Najua nimeongea sana, lakini sijui umenielewa?” Elvin alibaki akimtizama Bella kwa muda.
“Kama kitu kama hicho unachoeleza kinawezekana, kwa nini huyu mtu
tunayemlipa kila anapokuja, hajatushauri hivyo?” Bella hakutaka
kuingilia, akaamua kunyamaza. “Wewe
unafahamu hizo program?” “Nafahamu baadhi. Naweza nikashauri, kisha mkaangalia
bei zake.” Bella aliongea mambo mengi kama msomi sana na kama mtu mwenye
uelewa mkubwa sana.
“Umejifunza wapi mambo yote hayo?” Bella alitabasamu
kidogo. “Chuo kikuu cha Youtube.”
“Youtube! Hii hii youtube?” Bella alicheka kidogo. “Ndiyo. Si unajua huko kunapatikana kila kitu. Na mimi ndio natumia
sana kujifunza mambo mengi. Najikuta sina kazi au kitu chakufanya, kwa hiyo
natumia muda mwingi sana kwenye kompyuta. Na nina penda sana mambo ya biashara.
Kwa hiyo nikaamua kujifunza hii IT kwa upande wa biashara.” “Asante sana
Enabella. Ngoja nitaongea na Mzee tuone tunafanya nini.” “Sawa.” Bella
alijibu na kugeukia mezani, kuendelea na kazi. Alimuacha Elvin bado amesimama
akimtizama.
Bella aliendelea na kazi
siku hiyo bila kupumzika mpaka jioni alipoondoka. Huku nyuma alimwacha Joo na
mshangao. Kazi alizokuwa anashindwa kumaliza kwa siku, Bella alimaliza zote, na
kuanza kushambulia viporo vya nyuma.
*********************************************
Muda wa kuingia kwake
kazini haukuwa ukieleweka. Wakati mwingine alifika kazini saa nne, wakati
mwingine saa tano. Na mara nyingi kila anapoingia kazini alionekana hana
furaha. Alitambulishwa kwa wafanyakazi wote, lakini kama kawaida ya Bella,
hakutaka mazoea na mtu yeyote yule. Zaidi ya salamu hakutaka kuzungumzia mambo
mengine mbali na kazi. Alisikia wanawake wa pale wakimsema vibaya, nalo
halikumsumbua hata kidogo, alishazoea. Alichapa kazi bila kuchoka. Kila
anapoingia kazini, ni kweli alifanya kilichompeleka pale.
Sifa zake zilimfikia
Mzee Mwasha kutoka kwa wafanyakazi wengine, hasa wakiume. Mzee Mwasha alimwita
Bella ofisini kwake. Bella alihofia sana, alijua ni sababu ya kuchelewa kuingia
kazini. Alipokaa tu mbele ya meza ya Mwasha, Bella alianza kuongea. “Najua nachelewa sana kuingia kazini, lakini
najitahidi kumaliza kazi zangu zote kwa wakati. Kwa wakati huu siwezi kuahidi
kuwahi, kuna mambo yamenifunga. Naombeni mnivumilie.” Mzee Mwasha
alitabasamu. “Sio hilo nililokuitia,
Enabella. Nilitaka kukupongeza kwa utendaji kazi wako.” Bella alipumua
kidogo, nakujiweka sawa. Elvin alikuwa akimwangalia.
“Asante. Sijui mmefikia wapi kwenye swala la kubadili mfumo mzima
wa utendaji kazi. Niliongea kidogo na na na na…” Bella alishindwa kabisa
kutamka jina na Elvin, akaamua kunyamaza kama aliyepatwa na kigugumizi cha
gafla. “Tumezungumzia kidogo, lakini
inaonekana ni gharama sana. Inabidi kusubiri.” Mzee Mwasha aliamua kujibu. “Nina pendekezo.” Bella aliongea huku
akiwa na wasiwasi kama ni sawa kutoa maoni yake. “Karibu Bella. Ujisikie huru tu kutoa maoni yako, usiwe na wasiwasi.” Bella
alitabasamu kidogo huku akiendelea kumwangalia Mwasha, aliyekuwa akizungumza
naye tokea mwanzo, kwani Elvin alikuwa kimya kabisa, akimtizama. “Nafahamu kabisa kuwa hayo mapendekezo
niliyotoa hayakuwa kwenye budget yenu, na ninajua hizo ‘Accounting programs/systems’
zina gharama sana. Lakini nilipokuwa nikifanya kazi kwenye kitengo chenu cha
uhasibu, nimeona pesa mnayomlipa huyu mtu anayekuja kuwafanyia kazi mara moja
kwa week ni nyingi sana, halafu hata kama akiwafanyia kazi bado anawaacha
kwenye matatizo vile vile, na anafanya kazi kwenye kitengo kimoja tu, na kila
ninapoangalia, haonekani kama atamaliza kazi anayotakiwa kufanya kwenye hizi
siku za karibuni.” Bella akawatizama tena.
“Naomba msinielewe vibaya, sina nia yakumuharibia, lakini nilikuwa
ninapendekezo. Naomba mimi nigharamie hiyo program, tuiweke nakuijaribisha kama
itawafaa. Naomba tuipe miezi miwili ya majaribio. Mkiona inawarahisishia kazi,
na mngependa kuitumia, basi tutaibakisha, na mtanilipa hiyo pesa taratibu na
kwa wakati mtakao amua nyinyi, lakini kama mtaona ni kitu ambacho hamkihitaji,
nitachukua, na kuuza kwa watu wengine.” Mzee Mwasha na Elvin walibaki wametoa macho. “Sio lazima mkaamua sasa hivi, mnaweza
kupata muda wakufikiria zaidi, kisha mtanijulisha.” Bado kimya kilikuwa
kimetanda pale ofisini kwa Mwasha.
*********************************************
Msingi wa elimu waliyopewa na mama yao, na
mazingira waliyokulia, shuleni na hata mtaani, uliwajenga vizuri sana Bella na
mdogo wake. Walifundishwa kuongea mawazo yao, hasa pale wanapoona yanamanufaa.
Na walijituma bila hofu. Kitu kilichompelekea hata Eric kupendwa sana shuleni.
Mzee Masha ndiye aliyekuwa akimkandamiza sana Bella na kushindwa kuongea
kabisa. Alimnyanyasa binti huyo na kumuonyesha wazi kuwa mawazo yake pekee
Masha, ndio yataongoza mapenzi yao, si vinginevyo. Lakini tangia afike hapo,
alikuwa akifurahia sana anachokifanya. Nikama aliingizwa kwenye anga zake.
Hakuona mipaka, alikuwa akielea na kufanya kazi kwa moyo mmoja, tofauti na
wafanyakazi aliowakuta pale. Wengi walikuwa na malalamiko na niwazembe. Hakuna
aliyefurahia kazi yake.
Bella alijitahidi kuwa nao mbali kwa kadiri ya
uwezo wake. Walikuwa na maswali mengi
sana wanayoulizana juu ya Bella bila kupata jibu. Kila siku aliingia na mavazi
ya thamani sana, na kila alipopita, utajua tu Bella amepita. Hakuwahi kuwajibu
maswali yanayomuhusu yeye binafsi. Kama akiona ni swali nje ya kazi, alikaa
kimya na kuendelea na shuguli zake. Walijaribu siku za mwanzoni kumshawishi
mambo mengi ili ajiunge nao, lakini Bella hakutaka kabisa.
“Hapa
ofisini, wanawake tunakikundi chetu cha kusaidiana. Kuna kiingilio. Na huwa tunakopeshana.
Unataka kujiunga?” Mama mmoja mtumzima
kidogo alimfuata Bella kujaribu kumshawishi. “Kukiwa na tatizo lolote ambalo mnataka nichangie, usisite
kunishirikisha. Nitachanga.” Bella alijibu kwa kifupi na kugeukia kompyuta
yake kuendelea na kazi aliyokuwa akifanya. Alisikia wafanyakazi wengine
wakicheka nyuma yake, lakini hakugeuka. Kwa hiyo wote walimuelewa hivyo na
baadaye wakabaki kuheshimu maamuzi yake. Yeye ndiye alikuwa mdogo kuliko wote
pale ofisini, lakini ndiye aliyeonekana kujielewa kuliko wote.
*********************************************
Alipowaona bado wako
kimya hawampi jibu lolote, Bella alisimama. Naomba mniruhusu, nina kazi nataka
nimalizie kabla sijaondoka. “Subiri
kwanza Enabella.” Elvin alimuwahi. “Umesema
unaweza kutuwekea hiyo program?” “Ndiyo.” “Kwa kuiweka tu, utatudai kiasi
gani?” Bella alikunja uso kidogo. “Hapana
siwezi kudai. Si mmenipa ajira kama wafanyakazi wengine au bado hamjafikiria kuniajiri?”
“Tutakuajiri Bella.” Elvin alijibu kwa upole kidogo. “Basi itakuwa ni moja ya majukumu yangu hapa kazini na mtanilipa mwisho
wa mwezi mshahara kama wafanyakazi wengine.” Bella alijibu kwa heshima
kidogo. “Au nimekosea?” “Hapana. Tulipenda kujua, ili
tunapokubaliana tuwe tunajua tunajiingiza kwenye nini.” Mzee Mwasha
alijibu. Kwa wakati ule, pesa kwa Bella haikuwa tatizo hata kidogo. Alikuwa na
pesa za kuchezea kutoka kwa Mzee Masha, lakini ile kazi kwake ilikuwa zaidi ya
ajira. Ni sehemu pekee aliweza kujiona na yeye ni mwanadamu wa kawaida, na
aliweza kufikiria mambo mengine mbali na Mzee Masha. Hata hivyo alitaka
kutengeneza pesa za tofauti na zile za Mzee Masha alizoona nizamkosi kwenye maisha
yake.
“Unaweza kuileta lini hiyo program?” Elvin alihoji. “Hata kesho. Ninayo tayari nyumbani.
Niliinunua muda mrefu kidogo, nikawa nafanyia majaribio nikiwa nyumbani. Naamini
itawasaidia. Naomba na nyinyi muijaribishe, naamini mtaipenda na kuwafaa.”
Bella alikuwa akiongea kwa kujiamini, lakini taratibu sana na kwa unyenyekevu. “Asante sana Enabella. Nafikiri sio vibaya
tukianza mara moja.” Bella alionyesha furaha usoni. “Nitaileta kesho. Asanteni.” Bella alitoka na kuwaacha Elvin na
baba yake ofisini kwa Mzee Mwasha.
*********************************************
Bella aliendelea kufanya
kazi kwa bidi sana, bila kuchoka wala kulalamika. Aliweka ile program kwenye
ile kampuni, wengi waliisifia isipokuwa baadhi ya wasichana aliowakuta pale,
walisema ni ngumu kutumia. Siku moja Bella aliwahi sana kazini kwa kuwa alitaka
kumalizia kazi aliyoacha kwenye ofisi ya masoko kabla muda wa kazi haujafika,
saa mbili. Kwa hiyo kwa mara ya kwanza aliweza kuhudhuria kikao cha
wafanyazi wote pale ofisini.
Wengine walianza
kulalamikia ule utendaji mpya wa kazi, wakisema ni ngumu na upo kwa lugha ngumu
ya kingereza. Joo alisifia na kusema imemrahisishia kazi. “Wewe Joo hebu nyamaza. Unasifia kwa kuwa alikusaidia kufanya kazi zako
zote! Hapo ulipo huna kazi yeyote. Sisi tunaviporo vya miaka. Mpaka tuje
tumalize kuingiza huko kwenye kompyuta itatuchukua muda mrefu sana.”
Msichana mmoja aliongea. “Kwanza hata
mambo ya kompyuta yenyewe hatuyajui! Heri turudi kwenye kuandika kwenye
daftari.” Mwingine aliongeza. “Kingereza
chenyewe shida!” Mwingine aliongeza na wenzake wote wakacheka.
Elvin alishajua
wanafanya kusudi, na wivu unachangia. Wakati wote walikuwa wakimlalamikia Elvin
wakati Bella hayupo, kuwa Bella anakiburi, hawezi kusalimia watu na kwa nini
yeye anaruhusiwa kuingia ofisini kwa muda anaotaka yeye sio muda wa kawaida
kama wao!
Mzee Mwasha na yeye
hakuwa akija kazini asubuhi. Mara nyingi aliingia ofisini mida ya mchana. Kwa
hiyo hakuwepo kwenye hicho kikao, ni Elvin ndiye alikuwa akiongoza karibia kila
kitu, kasoro kwenye maamuzi fulani fulani, bado Mwasha, baba yake ndiye ilibidi
aidhinishe.
“Naelewa jinsi ilivyokuwa ngumu kupokea kitu kipya, hasa kama ulishazoea
au kama ulikuwa na utaratibu ambao ulishauzoea. Lakini kama mkijipa muda,
naamini mtazoea na kufurahia. Naomba hizo kazi zote za nyuma, mniachie mimi
nitazifanya. Nyinyi muendelee
kuingiza hizi za sasa, ili zisiwacheleweshe. Na atakaye kwama kwa lolote,
naomba asisite kuniambia, nitasaidia. Hata kama utahitaji tuwe wote ofisini
kwako, nitahamia hapo kwa muda, kuhakikisha nakuelekeza mpaka unaelewa, na
viporo vyenu vya nyuma nitavifanyia kazi kwa wakati wangu ili nisiwabugudhi
wakati wa kazi.” Hapo Bella aliwafunga midomo na kuwafanya wakose cha
kulalamika tena.
Elvin alikuwa akifurahi
sana moyoni. Ilikuwa ni kama Bella ameletwa na Mungu kumsaidia. Kwani baba yake
alianza kuugua, lakini hawakutaka kuwaambia watu, kwa hiyo Elvin aliachiwa
majukumu mengi sana pale ofisini, yakiwepo hayo ya malalamiko. Walikuwa wakimlalamikia
kupita kiasi, na walikuwa wakimchosha asijue atawasaidiaje. Hakuna kitu kizuri
ambacho wangeweza kukipokea bila shida. Baba yake, alikuwa akiajiri watu ambao
wanashida na pesa. Hakuwa akiangalia vigezo hata kidogo. Ilimradi ukimlilia
shida, basi anakupa ajira. Kwa hiyo Elvin aliachiwa ofisi kwenye mazingira
magumu sana. Alizungukwa na watu ambao walikuwa mzigo, hawakuwa na sifa za kazi
wanazofanya na hawakuwa tayari kujifunza. Akaamua na yeye afanye kazi bora
liende. Sasa kuja kukutana na Bella, ilikuwa kama gari ambalo limeongezwa
mafuta na kufanyiwa matengenezo na kupata dereva mzuri.
****************************************************
Alirudi nyumbani akiwa
na furaha, kwa ajili ya maendeleo ya kazi yake. Aliona mambo yanavyokwenda
vizuri pale ofisini kwake. Na kweli ile program ilikuwa sahihi kabisa. Dereva
alimrudisha, lakini alimwambia Masha yupo tayari nyumbani, anamsubiri. Aliingia
chumbani alipokuwepo Masha na tabasamu kubwa usoni. “Pole na kazi, T.” “Nasafiri Bella, nataka utulie. Umenisikia?” Bella alibaki amesimama akimtizama Masha aliyempokea
kwa mkwara. “Nauliza umenisikia?”
“Nimesikia T. Sina mahali pa kwenda isipokuwa kazini tu. Siwezi kufanya ujinga
wakati wewe umeniamini. Naomba usiwe na wasiwasi T. Nitakusubiri.” “Nikisikia tu unafanya mambo ya ajabu huku
nyuma, sitakusamehe.” Bella alibaki kimya.
“Unanisikia Bella?” “Nimesikia. Kwani utakaa siku ngapi?” “Unataka
kujua ili ujipange kufanya madudu yako huku nyuma? Nitarudi nitakapo rudi.” Bella alizidi kuumia. ‘Nimfanyie nini huyu baba jamani?
Nimefanya kila kitu anachotaka, lakini bado ameshindwa kuniamini.’
Bella aliwaza wakati Mzee Masha akizidi kumtishia maisha yake, endapo atakuwa
na mwanaume mwingine.
“Na kesho nataka ubaki nyumbani, kwa ajili ya kuagana.” “Siwezi T.
Nina kazi ambayo nilazima niifanye kesho. Tafadhali mpenzi wangu. Acha niende
hata masaa machache tu, nitawahi kurudi.” “Unasemaje Bella!?” Mzee Masha alisimama
akamvuta karibu. Bella alianza kutetemeka, huku analia. “Umeanza ujeuri? Ushapata mwanaume anayekudanganya huko?” “Hapana T. Unajua siwezi kuwa na mwanaume mwingine ila wewe. Siwezi
kukusaliti.” Bella alikuwa akilia
sana. “Naomba usinipige, Masha. Tafadhali sana.” Mzee Masha alimsukuma.
“Kazi zitasubiri, lakini sio mimi. Huogopi hata kidogo! Mimi
namiliki biashara zaidi ya mbili hapa mjini, nakwambia kesho naacha kazi zangu
ili niwe na wewe, halafu wewe kwa kazi hiyo moja ya kompyuta tu, tena ya watu, ndio
unaniambia eti huwezi kuacha kwenda kazini kwa siku moja! Na nikuone kesho
unatoa mguu wako humu ndani. Nitakufungia humu ndani mpaka nitakapo rudi.
Umenielewa Bella?” “Nimeelewa T. Kesho
sitakwenda kazini, nitabaki na wewe.” Bella alikuwa kitetemeka kwa hofu huku
akiendelea kulia.
*********************************************
Na kweli, kesho yake
Bella hakutokea kazini wakati ni siku ambayo alitakiwa kumsaidia mhasibu
kufunga mahesabu ya mwezi. Alitamani kupiga simu kumueleza Elvin kuwa hatafika
kazini, lakini asingethubutu hata kuonekana ameshika simu. Ilikuwa ni marufuku
kushika simu au kompyuta yake kama Mzee Masha yupo nyumbani. Alibaki
akimtumikia Mzee Masha vile atakavyo, kwa siku nzima.
Usiku alimsaidia
kufungasha, tayari kwa safari siku inayofuata ambayo ndio hiyo aliyokosa kazini.
Ilikuwa ni zaidi ya mwezi hajaenda kuangalia familia yake. Alikuwa akiondoka na
ndege ya KLM ya usiku huo wa saa tano. Bella alimsindikiza mpaka uwanja wa
ndege, akiwa na dereva. Walimsubiri mpaka ndege ilipoondoka ndipo dereva alipomrudisha
nyumbani.
Kitu cha kwanza
alichofanya aliwasha simu yake na kumpigia Elvin. “Samahani, nimekuamsha?” “Hamna shida. Ndio usingizi ulikuwa
unanichukua. Nilikuwa ofisini muda wote najaribu kuona kama naweza kuwasaidia
kufunga mahesabu.” “Pole sana. Samahani nilishindwa kufika, na nikashindwa
kukutaarifu mapema.”
Elvin alinyamaza. “Mlifanikiwa
kufunga mahesabu yote ya mwezi?” “Tumeshindwa Enabella. Hakuna mwenye utaalamu
huo, ila wewe.” “Samahani sana. Kesho naweza kumaliza.” “Kesho ni Jumamosi
Bella. Watu hawafanyi kazi pale ofisini.” “Mimi naweza kwenda. Naomba kama
inawezekana kesho niende nikajaribu kuona kama naweza kumalizia hiyo kazi.”
“Peke yako? Maana nawajua wale kina mama, hawawezi kukubali kuja ofisini siku
ya kesho.” “Nitafanya peke yangu, halafu jumatatu mkija ofisini nitawaelekeza
nilichofanya.” “Saa ngapi unataka kwenda ili nije kukufungulia? Maana mimi ndio
ninakaa na funguo za pale.” “Naomba wewe uniambie muda utakaoona sio usumbufu.
Mimi nina nafasi kesho siku nzima, hata ukiniambia saa 12 asubuhi nitafika.”
“Kwa kuwa nimechelewa kulala na nimechoka, naomba iwe saa mbili, ili na mimi
nipumzike kidogo.” “Sawa kabisa. Utanikuta nakusubiri.” Palizuka kimya kwa muda. “Hey Enabella!” “Bado nipo.” Bella
aliitika. “Naomba kama hutaweza kufika
hiyo kesho, unijulishe mapema, usiniache nakusubiri.” Bella alijisikia vibaya sana. “Nimeelewa.” Bella alijibu kinyonge
sana. Alijua Elvin amekasirika kwa kutotokea kazini. Alisikia simu imekatwa.
Haraka sana Bella
alijitupa kitandani huku akitokwa na machozi ya furaha, akifurahia uhuru wa
usiku huo. Alilala kama mtoto mchanga kwa uchovu. Aliamka kwa kuchelewa kidogo,
kwa hiyo hakupata muda wa kunywa chai na hakutaka kumchelewesha Elvin.
Alivaa harakaharaka na
kutoka. Akiwa njiani alituma ujumbe, ‘Nipo njiani.’ Baada ya muda mfupi aliona Elvin amejibu. ‘Nilishafika.’ Bella aliogopa kidogo akaangalia muda ilishakuwa saa mbili na
robo. Alijitahidi kuongeza mwendo ili asizidi kuchelewa.
*********************************************
Alimkuta Elvin ofisini
kwake. “Samahani kwa kuchelewa.”
Elvin alimwangalia, “Ni afadhali umekuja,
kuliko kutokutokea kabisa.” Bella alijua wazi Elvin bado amekasirika. “Jana nili…,” Bella alijua hata akimpa
sababu hawezi kuelewa, na hayamuhusu, akaamua aache kujitetea, aombe msamaha
tu. “Samahani kwa kutokutokea jana, na
kushindwa kuwasiliana.” “Ulikuwa ukikumbuka kama tulikuwa tukikutegemea wewe?”
“Ndiyo. Lakini nilishindwa.” “Hata kutuma ujumbe!?” Bella alinyamaza.
Alitamani kama Elvin angeelewa hata kidogo mazingira yake, labda asinge laumu.
“Hii ni kazi Bella. Unapoahidi kufanya jambo, jitahidi
kukamilisha. Kwa sasa wote tunakutegemea wewe. Naomba usisahau hilo. Watu wengi
walikwama jana bila msaada. Na hukutoa taarifa yeyote, tukabaki tunasubiri
mpaka jioni, kwa kuwa pia huna muda maalumu unaoingia kazini. Unakuja
unapojisikia wewe.” Elvin alionekana amekasirika sana lakini alijitahidi kuongea
kiuungwana kidogo. Bella alikuwa bado amesimama mlangoni.
Alisogea karibu na meza
ya Elvin, akavuta kiti, akakaa. “Elvin!”
Bella alianza kwa kuita jina lake. “Kumbe
unanifahamu jina langu!?” Elvin aliuliza kwa kumshangaa. “Maana tangia unaanza hii kazi, sijawahi
kusikia ukitamka jina langu hata mara moja. Mpaka nikawa na wasiwasi labda
hatukukupa utambulisho wakutosha! Lakini baadaye nikakumbuka,
nilishajitambulisha wakati tulipokutana Dubai, tena hata kule hukuonyesha kama
ulinisikia. Sasa sijui umeamua kunipuuza au vipi? Eti Bella?” Bella
alinyamaza akiwa bado ameinama, akiwaza amwambie nini Elvin bosi wake. “Basi, ofisi zote nilishafungua. Ukihitaji
kitu chochote, nitakuwa hapa ofisini kwangu.”
“Maisha yangu hayatabiriki Elvin, nipo katika wakati mgumu sana.
Hakuna jinsi nikaeleza ukanielewa. Nimejawa hofu, ni kama natembea na kifo
mgongoni mwangu. Nashindwa hata kuahidi chochote. Siwezi hata nikakuahidi kama
nitabadilika, katika mapungufu yote ambayo umeshayaona kwangu, kwa kuwa hata sijui kama baada ya dakika moja ijayo nitakuwa hai
au la. Nataamani kukuahidi kama siku nyingine nikishindwa kuja nitakutaarifu au
nikuahidi nitakuwa nakuja kazini kila siku muda fulani, nashindwa Elvin. sio
kwa sababu ninakudharau, au sithamini hii kazi. Hapana. Naomba kukuhakikishia,
naipenda kazi yangu na ninaihitaji sana. Na ndio maana kila ninapopata nafasi
ya kufanya kitu, nakifanya wakati uleule kwa akili zangu zote na moyo wangu
wote, kana kwamba hakuna kesho. Tafadhali naomba univumilie. Nitajitahidi
kufanya hii kazi kwa kadiri ya uwezo wangu, na ninakuahidi kukukamilishia
ripoti mapema iwezekanavyo. Kama kila mtu atakuwa ameweka vocha zake kwenye
kompyuta, nitahakikisha jumatatu unaikuta ripoti kwenye email yako kabla
hujaanza kazi.” Elvin alikuwa kama amepigwa na bumbuazi. Alibaki kimya kwa muda.
“Naomba univumilie.” Bella akarudia tena huku akifuta machozi. “Sawa. Mimi nitakuwa hapa ofisini. Ukihitaji
kitu chochote uniambie.” Bella alifikiria kidogo huku akijaribu kutulia. Alijikausha
machozi yote, akamwangalia. “Kwa nini
usingeenda kupumzika tu, halafu ukarudi baadaye? Kuliko kukaa tu hapa ofisini.
Najua unakuwa na kazi nyingi sana kwa juma zima na siku ya leo ndio siku yako
yamapumziko. Nenda tu. Kama nina maswali nitakujulisha kwa simu.” “Unauhakika?
Maana ni kweli nimechoka.” “Kabisa. Wewe funga tu milango yote, ili mtu yeyote asije
niingilia humu ndani.” “Basi ngoja nikalale kidogo, halafu nitarudi baadaye.”
“Sawa.” Bella alitoka na kuingia ofisi ya muhasibu, akaanza kufanya kazi.
Alikaa hapo ofisini
akiandaa hiyo ripoti siku nzima. Alishangaa jinsi walivyotawanya vocha, kana
kwamba walitaka kumkomoa yeye. Lakini Bella akajitahidi kuzikusanya na
kuzipangilia vizuri kwa tarehe na kuendelea kuziingiza kwenye kompyuta.
*********************************************
Ilipofika mchana Elvin
alirudi na msichana wake. “Vipi? Mambo
yanaelekea?” Elvin akauliza. “Kuna
matumaini. Nahitaji muda zaidi.” Bella alizungusha kichwa kumwangalia
Elvin. “Ungepumzika kidogo angalau
ukale.” “Nitakula baadaye.” Bella alisikia mtu mwingine akiongea kutokea
kwenye ofisi ya Elvin. “Hey Elvin, njaa inauma bwana.” “Nakuja sasa hivi.” Elvin alijibu na
kumgeukia tena Bella. “Kwa hiyo umegoma
kula?” Kabla Bella hajajibu akasogea yule dada. “Mambo!” alimsalimia Bella. “Safi
tu.” Bella alijibu kwa kifupi, kukazuka ukimya.
“Huyu anaitwa Irene. Irene huyu anaitwa Bella ndiye anayetusaidia
kwenye maswala ya IT.” “Mbona yeye utambulisho wake mrefu wangu ni Irene tu?” Irene aliongea kwa
kulalamika huku akimwangalia Elvin. “Unamaanisha
nini Irene?” “Wewe kweli ndio wakuniuliza hivyo Elvin au kuna kitu unaficha?”
“Naficha nini tena? Sina ninachoficha.” Irene aliondoka kwa hasira. “Samahani Bella. Nitarudi baada ya muda
kidogo.” Bella aligeukia kompyuta yake na kuendelea na kazi zake.
Baada ya muda kidogo,
Elvin alirudi akiwa amemshika mkono Irene. “Samahani
Bella, naomba nimalize utambulisho.” Bella aligeuka tena akionekana ana sura
ya kazi, kama asiyetaka usumbufu. “Huyu
anaitwa Irene, ni girlfriend wangu.” “Tunakaribia kuvuka huko bwana,
tunakaribia uchumba.” Irene aliongeza huku anatoa tabasamu. “Oookayyy!” Bella aliitikia huku akiwatizama
kwa kushangaa kidogo. Hakuona ulazima wa utambulisho wote ule, ni kama alikuwa
akiwataarifu, ‘hayanihusu’. Ukimya
ulitanda kidogo, Bella akiwasubiri kama kuna lanyongeza, alipoona wote
wanababaika aliona awe muungwana kidogo, “Nafikiri
natakiwa kuwapa hongera, ni sawa?” “Ndiyo. Maana ni hatua kubwa sana katika maisha.
Kila mwanamke angetamani kuwa na mwanaume kama Elvin.” Irene alijibu kwa
kujivuna kidogo. “Hongera.” Bella
alijibu kwa kifupi. “Asante.” Bella
aliwatizama tena kama vile akitaka kuuliza, kuna la nyongeza? Alipoona Irene
anacheka tu, Bella aligeukia kompyuta yake, akaendelea na kazi zake, akasikia
wanaondoka.
“Umefurahi
sasa?” Bella alimsikia Elvin akimuuliza Irene. “Sasa je? Nilidhani unanitosa mchana kweupe!” Wote walicheka,
akawasikia wakifunga mlango mkubwa wa kuingilia hapo ofisini. Bella alirudisha
mawazo yake kwenye kazi yake.
Alikaa pale ofisini peke
yake, mpaka ilipofika jioni ndipo Elvin alirudi tena. “Unataka kufunga ofisi sasa hivi?” Bella aliuliza pale Elvin
alipoingia pale ofisini. “Nakusikiliza tu
wewe, hata ukitaka kukesha leo, hamna shida, na hivi nililala mchana. Sina
neno.” “Basi naomba tena muda kidogo. Kama unamahali unataka kwenda, ungeenda
tu, halafu nikimaliza nitakupigia.” “Hamna neno. Nitakuwa ofisini kwangu.”
Bella hakupoteza muda aligeukia kompyuta yake tena na kuendelea na kazi.
Aliifanya ile kazi bila
kuchoka mpaka ilipofika usiku kabisa. “Kunywa
angalau maji Bella.” Elvin alirudi tena kwenye ofisi aliyokuwepo Bella. “Ndio nakutumia ripoti sasa hivi. Nimeshamaliza.”
“Daah! Kweli wewe kichwa!” Bella alitabasamu huku akiangalia kompyuta yake,
akiendelea na kazi aliyokuwa anafanya.
Bado Elvin alikuwa
amemsimamia pale pale ofisini. “Nikuulize
kitu Elvin?” “Uliza tu.”“Hii faida unayopata hapa sasa hivi, inalingana na
matarajio yako?” “Hii ni kampuni ya baba, Bella. Na mimi nimeajiriwa kama watu
wengine. Kuna mambo natamani kubadilisha lakini nashindwa. Lengo la baba kwenye
hii kampuni si kutengeneza pesa peke yake, anataka iwe msaada kwa watu wengine
pia. Ndio maana unakutana na watu wengi humu ndani ambao hawana hata vigezo vya
kazi zao.” “Nimekuelewa. Lakini sasa
hivi wewe ndio upo kumsaidia kuendeleza. Nia ya baba ni nzuri, nafikiri ndio
maana hata mimi mwenyewe nipo hapa leo, japokuwa sina vyeti. Naona tumsaidie
kuongeza faida.” Elvin alivuta kiti akakaa.
“Kwa kufanyaje?” “Naomba tuongee jumatatu kama Mungu akitupa
uzima, sasa hivi nimechoka, nataka nikapumzike kidogo.” “Ni kweli. Umefanya
kazi siku nzima bila kupumzika tutaongea jumatatu kama utakuja.” Bella alitabasamu. “Naamini nitakuja.” Bella alifikiria
kidogo. “Unafikiri ni sawa kama
nikichukua baadhi ya kazi nikafanyie nyumbani.” “Nini tena?” “Kuna kazi kubwa
sana za nyuma, ambazo wamebakisha watu wa masoko. Nataka kesho nizifanyie
kazi.” “Huwendi kanisani?” Bella alikunja uso. “Kanisani!?” “Ndiyo. Kuabudu.” “Hapana. Huwa siendagi kanisani. Siku za
jumapili nakuwepo tu nyumbani, ndio maana nataka nikafanyie kazi nyumbani.”
Elvin alibaki akimshangaa Bella jinsi alivyojitoa kwenye ile kazi. “Ni sawa tu. Wewe endelea.” Elvin alimpa
ruhusa. Aliingia kwenye ofisi za watu wamasoko, akakusanya kazi zote za nyuma,
akapakiza kwenye gari yake, akaondoka.
*********************************************
Siku ambazo Mzee Masha
hakuwepo nyumbani, Bella alizitumia vizuri sana. Alikuwa akiamka asubuhi sana
kuwahi kazini, na kurekebisha kazi za kila kitengo. Maneno yalianza kupungua,
ikabaki heshima tu. Maana mwanzo walifanya mbinu nyingi kumuharibia kwenye
uongozi, lakini baadaye walikuja kujiona ni kujisumbua wenyewe. Akili na mawazo
ya Bella yalikuwa kwenye kazi tu, hakutaka kujichanganya kabisa pale ofisini.
Palipokuwa na mgonjwa, misiba, sherehe, na wakachangisha, Bella hakuacha
kuchanga. Alipokuwa akisikia mtu anashida yeyote, japokuwa hatataka kujua kwa
undani, aliweka pesa kidogo kwenye bahasha, na kutafuta muda ambao huyo mtu
yupo peke yake na kumkabidhi. Wanawake wa pale ndani hawakuacha kutupiana
maneno au kusemana, na Bella alikuwa akiwasikia, lakini kila penye masengenyo,
au ugomvi, Bella alijitahidi kuondoka. Aliwaonyesha wazi, hataki mahusiano, nje
ya kazi. Walimuelewa kwa haraka sana, na wakaanza kumpenda. Alipewa ofisi yake
kitu kilicho mfurahisha zaidi.
Aliitengeneza hiyo ofisi
na kuipamba vizuri sana. Mezani kwake aliweka picha kubwa ya Eric, akawa
akiiangalia kila wakati. Alipamba na maua mazuri pembezoni mwa ofisi yake. Kila
kona aliweka vyungu hivyo vya maua, juu ya stuli nzuri sana. Vilionekana ni
vyungu na stuli za thamani kweli. Yote hiyo ilikuwa pesa yake. Akatandika zulia
zuri la thamani pia. Ungependa kuwepo kwenye ofisi hiyo ya Bella.
Kwa kuwa kulikuwa na
wafanyakazi wengi ambao Bella aliona hawana kazi pale ofisini, na wanalipwa
mshahara, Bella alimpa Elvin mawazo ya kuongeza biashara nyingine, ambayo hata
wale ambao hawakusoma ingewafaa na kuwaanzishia kitengo chao, kwa kutumia jina
hilohilo la kampuni lakini biashara nyingine.
Kwa kuwa Mzee Mwasha
alipotea pale ofisini, Elvin alimfanya Bella kuwa mshauri wake mkubwa. Hakuna
kitu ambacho alikifanya bila ushauri wa Bella. Kidogo wakaanza kuwa karibu.
Angalau waliweza kusalimiana na kuulizana hali. Ile hali ya kazi tu kati yao
ikaanza kupungua. Elvin aliweza kuingia ofisini kwa Bella na kutoa salamu tu na
Bella asishangae. Mtu mwingine ambaye hakuwa na tatizo kuingia ofisini kwa
Bella alikuwa Joo. Joo aliingia kufanya utani wa hapa na pale, na watu wote
walianza kujua Joo ndiye mtu pekee anayeweza kumfanya Bella acheke au aache
kazi zake na kumsikiliza yeye, hata akiwa anaongea vitu visivyo na maana. Alikuwa
na utundu wa namna yake, uliokuwa ukimfurahisha Bella. Japokuwa hakuwa akiongea
sana, lakini alikuwa akimsikiliza na kumfanya acheke.
“Mkasa mwingine wakusikitisha
wa Bella.”
Wakati mambo ndio
yanakwenda vizuri, Bella ndio amepata heshima pale ofisini, Mzee Masha naye
akarudi kutoka uholanzi. Aliingia na ndege ya Emirates saa nane mchana. Moja
kwa moja nyumbani kwa Bella. Aliamua kulala huku akimsubiri Bella ajue ni saa
ngapi huwa anarudi nyumbani. Siku hiyo ilikuwa siku ya mvua, usafiri ulikuwa
washida sana jijini Dar. Joo akamuomba Bella amsogeze karibu na daladala za Kariakoo
ambazo alijua lazima zitakuwepo kwa muda huo, kituo cha Posta Mpya.
Kwa kuwa hakuwa na kitu
kinachomuwahisha nyumbani, na walimaliza kazi mapema, Bella alikubali. Hata
hivyo alimpenda Joo, alimfanya asahau shida zote na awe na furaha. Njia nzima
Joo alikuwa akipiga yeye stori za mtaani kwao uswahilini. Bella alikuwa
akicheka sana, akikumbukia maisha ya Kigogo alipokuwa akiishi na Mat, dereva
wao. Kulikuwa na foleni kubwa sana, lakini Bella hakujali. Walipoona hakuna
daladala za Kariakoo, akaamua amsogeze mpaka Tazara, ambako alijua lazima kwa wakati ule
asingekosa daladala.
Walitoka Posta mpya
kuelekea Tazara huku mvua ikinyesha sana, na walikutana na foleni kubwa njiani,
lakini Bella hakujali. Aliendelea kusikiliza porojo za Joo huku akicheka. Hakuwa
na wasiwasi kabisa, kwani alijua hakuna wakumuuliza, na hakuna anayejali, kwani
hata dereva wa Mzee Masha na yeye alikuwa likizo, kwa hiyo Bella akawa hana
wasiwasi kabisa. Alimshusha Joo kituoni Tazara, akaanza safari ya kurudi
nyumbani kwake, akiwa amejawa furaha, anaimba na kucheka peke yake.
Alifika nyumbani kwao
kama saa nne za usiku akiwa amechoka sana. Alipoingia tu alimkuta Mzee Masha
amekaa sebleni. Bella alibaki ameduwaa mlangoni bila salamu yeyote. Alitamani
arudi alipotoka. Alijua kipigo kinachofuata pale sio cha kawaida. Mzee Masha
hakuwa mtu wakusikiliza hata kidogo, kwa hiyo alijua kujitetea ni kujiongezea
matatizo. Bella alibaki akimwangalia huku anatetemeka. Alikuwa amelowa kidogo,
sababu ya kutembea alipokuwa ameegesha gari lake mpaka ndani. Mbaya zaidi Mzee
Masha alikuwa hawezi kukaa sehemu yenye joto. Kwa hiyo mara zote kila awapo
nyumbani aliwasha AC, upande wa baridi na wakati wote nyumba yao ilikuwa na
baridi kali sana. Alianza kusikia ile baridi mpaka kwenye mifupa. Bella alibaki
akitetemeka huku akimwangalia Mzee Masha. Hakuna jinsi angemwambia Mzee Masha
alitoka kumpeleka Joo kituoni Tazara akapona. Alijua kifo chake ndio kimefika.
Alimkumbuka Eric mdogo wake, machozi yalianza kumtoka.
“Umetoka wapi Bella? Na usinidanganye, kwa kuwa nimepiga simu
ofisini kwako nimeambiwa ulitoka kazini tokea saa kumi na mbili.” Bella alibaki akilia.
Mzee Masha alisimama na kumsogelea. “UNATOKA
WAPI?” Bella alipata kibao cha nguvu, akamvuta mpaka chumbani. “Walinzi wameniambia, week zile za mwanzoni
nilipoondoka tu, ulikuwa ukitoka alfajiri sana, na kurudi usiku sana. Ulikuwa
ukienda wapi Bella? Unataka kuniua? Unanitia aibu pale kwa Mzee Mwasha, wanaona
nimewapelekea Malaya. Wewe ni zaidi ya mbwa Bella. Nimejitahidi kukuridhisha
kwa kila kitu lakini hutosheki!” Bella alipigwa usiku huo, kupita kiasi.
“Niambie ulipokuwa Bella, hakika nitakuua leo.” “Hata nikikwambia hutaniamini.” Bella akiwa anatokwa na
damu mdomoni, tena ametupwa sakafuni, alijibu. “Kwa
nini hauniuwi tu, T. Kwa nini huchukui bastola yako ukaniua na mimi nipumzike.
Nimechoka T, umenipiga zaidi ya lisaa, na bado hujatosheka. Naomba unimalize
tu, ili upumzike. Lakini nakuhakikishia, sijatoka sehemu mbaya, na hata
nikikwambia hutaniamini.” Bella alikuwa akilia sana. “Niuwe
tafadhali. Huna cha kupoteza. Najua unauwezo wakupata mtoto mwingine kama mimi
ambaye atakuridhisha. Kwa nini usiniue tu, ukaendelea na maisha yako, kuliko
hivyo unavyoishi kwa wasiwasi. Huniamini kwa lolote, umenigeuza kuwa ngoma,
huni thamini. Unanionea. Unaninyanyasa vile unavyotaka. Unatumia mwili wangu
bila shukurani.” Mzee Masha alimsogelea tena.
“Nimekwambia usithubutu kunipiga tena, Mzee Masha. Inatosha. Leo
ndio iwe mwisho wako, naomba tumalizane. Niue yaishe. Niue T. Ukitoka kwa mkeo
na hasira zako, unakuja kunimalizia mimi, unanipiga kila siku bila kosa. Watoto
wako wakikuudhi, au wakikujibu vibaya, au wakigoma kuendelea na masomo, unakuja
kunipiga mimi.” Bella aliendelea kulia. “Unashangaa nini?
Unafikiri ni wewe tu mwenye uwezo wakurikodi simu yangu? Hata mimi narikodi
simu yako.” “Unasemaje Bella?” “Nimekwambia na mimi na rikodi simu yako. Huwezi kuja kuniua na
UKIMWI, T. Lazima nijue tupo wanawake wangapi.”
“Kwa hiyo unanifuatilia?” “Ndiyo.” Bella alijibu kwa
hasira sana.
“Usinisogelee T. Nimechoka, kama hutaniua leo, naomba uniache.
Kila watoto wako wakikukorofisha au mkeo akikukorofisha, unageuka kuwa kama
mnyama kwangu na kunifanya utakavyo. Kama sio kunitafutia sababu ya kunipiga,
basi utanibaka siku nzima. Nimekuwa jalala lako! Unanitumia kumwaga huzuni
zako, hasira zako na kila kitu kibaya kwenye maisha yako, mimi ndio umenifanya
sehemu yakutupia. Na bado hunithamini. Sidhani hata kama umewahi kumpiga mkeo
kama unavyonipiga mimi. Sidhani hata kama umewahi kuheshimiwa na kutunzwa kama
ninavyokufanyia mimi, lakini bado unanifanyia ukatili wakupita kiasi na Mungu
atakulipa T. Ipo siku atakulipa kwa mabaya yote unayonifanyia. Kama sio wewe
basi Zera naye atapita nilipopita mimi na wewe ukiona sio ukiwa umekufa. Utajua
mateso ninayoishi nayo.” Bella alikuwa amejawa na uchungu sana. Aliinama akawa analia sana
huku damu zikimwagika sakafuni, hata yeye mwenyewe hakuwa akijua zinatokea wapi.
Mzee Masha aliondoka usiku huo bila kuongeza kitu wala kumpiga tena.
*********************************************
Kwa maumivu makali
aliyonayo, Bella alishindwa hata kusimama, alilala pale pale chini mpaka
asubuhi. Aliamka akiwa na maumivu makali sana. Mwili wote ulikuwa umevimba.
Alitambaa mpaka sebleni ilipokuwa imedondoshwa pochi yake na simu yake ya
mkononi. Akapiga simu getini kuita mlinzi. Mlinzi alipokuja alimuomba msaada
wakumbeba mpaka kwenye gari yake. Mlinzi akaja kwa haraka, akambeba mpaka
kwenye gari huku akilia sana maumivu.
Safari hii aliamua
kwenda hospitalini yeye mwenyewe, kwani alikuwa na maumivu makali sana, hasa
kwenye mbavu. Alihisi kule kupigwa mateke kwa muda mrefu, amevunjwa mbavu.
Bella alipandishwa kwenye gari akiwa na lengo la kwenda hospitalini. Alijua
kama kawaida yake, Mzee Masha akishampiga vile, huwa anapotea hata mwezi.
Bella aliendesha mpaka
alipofika Mwenge, akaanza kuona giza. Akaamua akate kona aingie njia ya kiwanda
cha Cocacola ambapo hakuna magari mengi, akaliegesha gari pembeni kabisa ya
barabara. Alikaa pale akisubiri ajisikie vizuri ili aendelee na safari yake,
lakini alishindwa kuona tena, ilikuwa giza kabisa, wakati ilikuwa ni asubuhi
jua limechomoza, akaamua kumpigia simu Elvin. Alibonyeza simu yake, akatamka
jina la Elvin, aliposikia simu yake imetamka jina la Elvin, akaamuru simu hiyo
kumpigia Elvin. Simu yake ilikuwa na uwezo wa kufanya chochote kwa kuamrishwa
kwa sauti bila ya Bella kubonyeza sehemu.
“Bella!” “Nisaidie
Elvin.” Bella alikuwa akisikika
kwa shida sana, kwani alikuwa akilia na yupo kwenye maumivu makali sana. “Uko wapi?” “Kiwanda
cha C..” Bella alishindwa
kuongea. “Bella!
Bella!” Elvin alizidi kupanic. “Uko wapi Bella?” Bella
alikuwa akimsikia Elvin kwa mbaliii. Akajikaza ili kumpa maelekezo yakueleweka. “Mwenge, karibu na kiwanda cha Coc..” Alishindwa kumalizia. Akapoteza fahamu kabisa. “Bella!
Bella!” Elvin aliendelea kuita kwa hofu, bila majibu upande wa pili.
Baadaye sana alisikia
kwa mbali mtu akiongea, na kumpima pressure yake. Bella alijua yupo hospitalini,
akajaribu kufunga macho lakini akashindwa. “Maumivu.
Nasikia maumivu makali sana.” “Wamesema watakuchoma
sindano ya maumivu sasa hivi. Pole Bella.” Aliposikia sauti ya
Elvin, alijua yupo salama. Akapotelea usingizini huku anagugumia maumivu.
Alishtuka tena akiwa
amelazwa kwenye kitanda cha hospitalini. Alitaka kugeuka lakini alishindwa
kabisa, maumivu yalikuwa makali. Alitaka kuongea, lakini mdomo ulikuwa kama
umewekwa gundi, Bella alianza kulia tena kwa kulalamika. Elvin alisimama
alipoona anajaribu kufungua macho. “Jicho
hilo la kulia, lilipasuka kidogo hapo kwenye nyusi, Bella. Wamekushona. Ndio
maana inakuwia ngumu kufungua macho. Na mdomo umevimba sana sababu umepasuka
pia. Usijaribu kufungua utajitonesha. Wamekutundikia dripu ya maji ili kukupa
nguvu na wamekuwekea dawa kwenye hayo maji, ili kuzuia kuvuja kwa damu kwa
ndani. Wamegundua jana usiku kuwa ulikuwa unavujia damu ndani kwenye mbavu za upande
wakulia. Pia mbili zimevunjika. Wameweza
kusimamisha hiyo damu. Lakini usigeuke, utajitonesha zaidi.” Bella alifunga
macho huku machozi yakimtoka, alilia kidogo kisha akapotelea usingizini tena.
Alikuwa chumba cha
wagonjwa mahututi, na alipoteza fahamu kwa siku mbili mfululizo. Walijaribu
vipimo vingi, kwani hali yake ilikuwa ikizidi kuwa mbaya. Ndipo ilipobidi
kufanyiwa vipimo vya mwili mzima, wakagundua anavujia damu kwa ndani. Elvin alishindwa
kuondoka kabisa pale hospitalini. Alijilaumu sana kuto muuliza Bella siku ile
wakati wanazungumza, na Bella alimwambi kuwa anatembea na kifo mgongoni.
‘Hasira zilinifanya nishindwe kumsaidia Bella.
Labda alikuwa anahitaji msaada wangu. Ni mara ya pili hii Mungu anamleta kwenye
maisha yangu. Na mara zote anakuwa kwenye shida, na nimeshindwa kumsaidia.
Kwanza Dubai, Bella alikuwa akilia sana, tena kwa uchungu, na tena hapa!
Nimeshindwa kumsaidia kabisa Bella.’ Elvin aliendelea kujilaumu sana moyoni mwake.
Alikaa naye pale hospitalini asijue ampigie simu nani. Kwani simu ya Bella
ilikuwa haina jina hata moja, zaidi ya namba yake tu, ambayo ilionyesha ndio
aliyopiga kabla hajapoteza fahamu. Hapakuwa na namba nyingine yeyote. Ilikuwa
kama simu mpya kabisa, kitu kilichomshangaza Elvin.
Baada ya kulala kwa muda
mrefu, kwa mbali tena, akasikia watu wakizungumza. “Kapumzike Elvin, mimi nitakuwa naye hapa.” “Siwezi kuondoka mama.”
“Wewe umesikia madaktari wamesema huyu sio mtu wakuzinduka leo wala kesho, mpaka
hiyo damu iingie mwilini vyakutosha. Nenda kalale kidogo, halafu ukiamka
umtafute na Irene. Mwenzako anawasiwasi sana na wewe Elvin. Ni siku ya tano hii
hujamtafuta. Mpaka wazazi wake wanatupigia simu kukuulizia. Wanawasiwasi kama
umebadili mawazo.” “Waambie sijabadili mawazo hata kidogo mama. Lakini nahitaji
muda kidogo. Nilishamuahidi Irene nitamuoa, na nitafanya hivyo. Sina sababu ya
kutokufanya hivyo, wewe unanijua mama.” “Kwa nini wewe mwenyewe usimpigie Irene
ukazungumza naye?” “Wewe unamjua Irene, mama. Atataka aje tukae nae hapa, huku
akilalamika. Itakuwa vurugu tupu hapa. Wewe tafuta jinsi ya kuzungumza nao,
mama yangu. Bella akipata nafuu, tutaendelea na mambo ya uchumba kama
tulivyopanga.” “Pete ulishachukua?” Mama Mwasha alimuhoji mwanae. “Nilishalipia mama. Nitaenda kuichukua, au
mwambie baba akanichukulie.” Kumbe Bella alizimia tena siku mbili
zilizopita, ndipo wakagundua ile damu waliyodhani wameidhibiti hawakuwa
wamefanikiwa, kwa hiyo aliishiwa damu. Wakafanikiwa kumfanyia upasuaji,
wakamsafisha, na kumuunganisha mirija hiyo ya damu, akawekewa damu nyingine.
Hali yake ilikuwa mbaya sana. Ilikuwa ngumu kumtizama Bella mara mbili.
Alivimba uso sana. Mwili mzima ulijaa alama za mikanda ya suruali. Wazi
alionyesha alipigwa vibaya sana.
Bella akarudi kulala. Lakini
akiwa kwenye usingizi mzito Bella alisikia Eric akimwita, ndio maana akashtuka.
“Ric! Riccc!” Bella alianza kumwita
mdogo wake. Elvin alisimama kwa haraka. “Unajisikiaje?”
“Ric!” Elvin alikumbuka jina la Eric, akajua ndiyo huyo Bella anamtaja kwa
kifupi. Kwani ni picha ya Eric pekee ndiyo ilipamba ofisi ya Bella. “Upo hospitalini Bella.” Bella alianza
kulia huku anaongea kitu. Elvin aliinama kutaka kumsikiliza. “Sikusikii Bella. Pumzika tutaongea
baadaye.” Bella alitingisha kichwa kukataa. Elvin alisogeza masikio karibu
na mdomo wa Bella uliokuwa bado umevimba. Alimsikia Bella akitaja namba, Elvin
aliziandika zile namba akagundua ni za simu. “Naomba umpigie simu huyo mtu, tena naomba utumie simu yako, usimwambie
kabisa nilipo, mwambie akamwangalie Ric.” Baada ya muda mrefu
sana, ndipo Elvin aliweza kuunganisha maneno, akaelewa ujumbe mzima. “Sawa nitafanya hivyo.” Bella alirudi
kulala tena.
Alikuwa akilala tu kwa muda
wa majuma mawili mfululizo. Baada ya siku kumi na nne ndipo angalau Bella
aliweza hata kunyanyua mkono. “Vipi?”
“Najisikia vizuri leo.” Elvin alikuwepo pale hospitalini peke yake
akimuuguza Bella. “Pole sana.” Bella
alianza kulia. “Pole Bella.” “Asante. Ric?” “Nilipiga
ile namba ya simu uliyonipa. Nikakutana na mtu anaitwa Mat, akasema atakwenda
kumwangalia Ric shuleni. Nilipopiga siku inayofuata, akasema yupo Arusha,
lakini Ric wamekwenda Nairobi kwenye michezo.” Bella alifurahi sana. “Asante Elvin.” Machozi yalikuwa yakimtoka Bella. “Karibu.” Elvin alibaki akimwangalia
Bella, hakujua chakusema. “Utapona Bella.
Ulibahatisha kupata madaktari wazuri sana. Wamekuwa wakikuhangaikia usiku na
mchana bila kuchoka. Na mimi nimekuwa nikikuombea.” “Asante.” Mara mlango
ukafunguliwa. Waliingia wazazi wa Elvin.
Sifa za Bella
zilishafika kwenye familia ya Mzee Mwasha. Jinsi alivyobadilisha ile kampuni na
jinsi alivyojitoa kufanya kazi bila kudai malipo ya ziada. Kila mmoja wao
aliona anajukumu lakumsaidia Bella. “Pole
sana mama. Pole.” Mzee Mwasha alisogea kitandani kwa Bella. “Asante.” Bella alijibu taratibu lakini
waliweza kuelewa. “Unajisikiaje?”
Mama Mwasha naye akauliza. “Sasa hivi maumivu sio
makali sana.” Machozi yalikuwa yakimtoka Bella taratibu pembeni ya macho yake. “Utapona mama. Umesikia? Utapona.
Tunakuombea, na kabla yakuondoka hapa, tutaomba pamoja. Mungu atakusaidia.”
Bella alitingisha kichwa. Mzee Mwasha akaomba atoke nje na Elvin. Wakatoka na
kumuacha Mama Mwasha na Bella.
*********************************************
“Lazima umpigie simu Irene
sasa hivi, na urudi nyumbani ukamuone. Kila siku anakuja nyumbani kukuulizia.
Anawasiwasi kwamba umebadili mawazo. Watu wote sasa hivi wameingiwa na wasiwasi
Elvin. Huwezi kuanzisha jambo na kuliacha katikati. Umenielewa?” “Ndiyo baba.”
“Sisi tutakuwa hapa na Bella, mpaka utakaporudi. Umenielewa? Rudi nyumbani,
pumzika, ndipo urudi hapa. Hata kama ni usiku, sisi tutakuwepo hapa. Hata sisi
tunamjali Bella. Hatuwezi kumuacha hapa peke yake, mpaka ndugu zake watakapofika.
Unanielewa?” “Nimeelewa baba. Basi ngoja nikamuage.” Mzee Mwasha alimpisha.
Elvin akarudi kwa Bella.
“Hey Bella!” Bella akafungua macho. “Nitarudi
baadaye.” Bella alijitahidi kutoa mkono wake ndani ya shuka na kumpa Elvin.
“Asante sana Elvin. Nakushukuru.”
“Nitarudi. Sitakawia.” Bella alitingisha kichwa huku machozi yakimtoka.
Elvin alisimama akimtizama Bella kwa muda, mpaka baba yake alipomwita tena. “Elvin!” Alishtuka kidogo, akachukua
funguo za gari lake, akaondoka. Bella alirudi kulala.
Aliamka usiku akamkuta
Mzee Mwasha na mkewe bado wamekaa wakimwangalia. “Unajisikiaje?” “Vizuri kabisa. Leo ni tarehe ngapi?” Bella
aliuliza. Alipotajiwa, alifikiria kidogo, akashtuka sana. “Imeshakuwa zaidi ya siku kumi na nne tokea niwe hapa!?” “Ndiyo.” “Nataka kuondoka hapa. Siwezi kuendelea kukaa hapa hospitalini.” Bella alionyesha kupanic sana. “Lazima
niondoke sasa hivi.” Bella alianza kulia, gafla mlango ukafunguliwa. “Mbona analia?” Alikuwa ni Elvin. “Mama?” “Ndio ameshtuka kutoka usingizini
sasa hivi, analia anataka kuondoka.” Elvin akamsogelea Bella. “Hey Bella! Bella? Niangalie.” Bella alizidi
kulia.
“Hali yako bado sio nzuri. Lazima usubiri madaktari wakuhudumie.” “Huwezi kuelewa Elvin, lakini ni lazima niondoke. Nimeshapona,
nitaendelea kunywa dawa nikiwa nyumbani.”
“Umejiona lakini Bella?” “Hii ni kawaida Elvin,
nimeshazoea. Nitakuwa sawa. Naomba ukaongee nao, hizo dawa wanazonipa
waniandikie vidonge, niondoke sasa hivi, siwezi kuendelea kukaa hapa hata zaidi
ya dakika kumi. Tafadhalini. Lazima niondoke, sasa hivi.” “Ni usiku sana Bella. Kwa nini usisubiri kesho?” “Unaniahidi kesho utazungumza nao waniruhusu?” “Nitaongea na daktari.” Bella alitulia kidogo.
“Wazazi wako wako wapi Bella?” Mzee Mwasha aliuliza. Baada
ya muda mrefu sana Bella akajibu. “Tulikuwa
tukilelewa na mama, lakani alifariki.” “Ndugu
zako wako wapi?” Hapo Bella hakujibu kabisa alikaa kimya mpaka Mzee Mwasha
na mkewe walipoaga na kumuacha Elvin akiendelea kuuguza. Wakati Elvin
anawasindikiza wazazi wake, Bella alijitahidi mpaka akaweza kukaa. Alianza
kujichomoa kila mpira uliopo kwenye mwili wake. Alichomoa mpaka dripu ya maji.
Akasimama kwenda chooni.
Alijiangalia jinsi alivyovimba, na kuwekwa bendeji usoni. Bella akaanza kutoa
taratibu. Japokuwa uso ulikuwa umevimba, lakini Bella hakushtuka hata kidogo,
alishazoea ile hali. Taratibu aliosha uso wake, na maji huku akisikia maumivu
lakini pia hakushtuka. Yale maumivu ya sasa hayafikii hata nusu ya maumivu
aliyokwisha wahi kujisikia. Elvin alirudi, akashtuka sana. Alimsikia anaoga
bafuni.
Maji kutoka kwenye dripu
yalikuwa yanamwagika sakafuni, na waya zote zilizokuwa zimewekwa mwilini mwake,
kuangalia mapigo ya moyo, na mipira ya kumsaidia kuhema, vyote vilikuwa
vimezagaa sakafuni pia. Elvin alimwita nesi, wakasafisha, na kubaki
wakimsubiria Bella, waliyedhani ni mgonjwa mahututi, atoke bafuni. Hakuna
aliyeamini alipotoka bila bandeji yoyote mwilini mwake.
Elvin alimuwahi kumshika
mkono ili asianguke. “Ona Bella! Bado
hujapata nguvu.” “Ni kwakuwa sijala
chakula, nimekuwa nikiishi kwa maji tu.” “Mbona umetoa kila kitu?” “Hizo
bandage zitanichelewesha kupona vidonda na sihitaji maji mwilini kwa njia ya
sindano. Nitakula na kunywa maji kama kawaida. Lazima niondoke Elvin. Tafadhali
naomba usinizuie.” “Lakini bado wewe ni mgonjwa, Bella.” “Hapana, mimi sio
mgonjwa, nimepona. Huu uvimbe ni kawaida tu. Utaisha taratibu. Naomba chakula
nile.” Yule nesi na Elvin walikuwa hawamuelewi Bella.
“Simu
yangu iko wapi?” Bella akauliza. “Iliishiwa
chaji ikazima.” “No no no nooo. Naomba niazimie chaja haraka unichajie Elvin,
tafadhali. Lazima hiyo simu iwake, sasa hivi.” Elvin hakuwa akielewa, lakini
alitoka na baada ya muda akarudi na chaja. Aliweka ile simu kwenye umeme hata
dakika tano hazikuisha, akaiwasha. “Mbona
unaniogopesha Bella.” “Samahani Elvin, hata nikikwambia hutaelewa. Ni lazima
nifanye mawasiliano.” Na kweli Elvin hakuwa akielewa.
Bella alipiga simu kwa
Mat. “Shikamoo kaka.” “Hujambo Bella?” “Sijambo kaka. Ulienda kumfuata
Ric? Maana shule zimefungwa.” “Nilipoenda wakaniambia alishachukuliwa. Ulimtuma
nani?” “No no no nooo.” Bella alizidi kupaniki. “Bella?”
“Kwaheri kaka, nitakupigia baadaye.” Bella alikata simu.
“Naomba
pochi yangu.” Bella alimgeukia Elvin
aliyekuwa haelewi. Alitoa wallet yake, akavuta kitabu cha hundi. Akaweka saini
kwenye hiyo hundi, bila kuandika kiasi, kisha akamkabidhi Elvin. “Naomba unisaidie kitu kimoja cha mwisho
bila kuuliza swali.” Elvin alibaki akimwangalia Bella. “Tafadhali Elvin.” “Unataka nini Bella?” “Uhakikishe wanakuandikia dawa
zote ninazotakiwa kunywa, uninunulie. Mimi
nitazifuata ofisini. Na hii hundi, utaandika gharama zote watakazokuwa
wananidai hapa hospitalini, kisha uwalipe. Lazima niondoke sasa hivi Elvin.” “Sikuelewi Bella.” “Nilikuomba usiniulize swali. Naomba unisaidie tu.”
“Lakini wewe bado ni mgonjwa Bella, utatokaje hapa!?” Bella alimpa tabasamu
lakumridhisha. “Unaona ile hali
uliyonikuta nayo? Ilishanitokea kama hivyo, nilikaa nikijiuguza mwenyewe
nyumbani mpaka nikapona. Usiwe na wasiwasi Elvin, mimi nimeshapona. Nitakuja
ofisini baada ya siku chache sana. Naomba nisaidie nguo zangu nivae.” Bila
kupoteza muda, Bella alianza kubadili nguo zake, pale pale bila hata kufikiria,
ikabidi Elvin ageuke.
Alishika viatu vyake mkononi na pochi. “Naomba unisindikize mpaka kwenye gari yangu
tafadhali.” “Au mimi nikupeleke?”
Elvin akauliza. “NOOOOO.” Bella
alikataa kwa nguvu zote na kumshangaza zaidi Elvin. “Lakini asante. Usiwe na wasiwasi. Mimi nitafika salama tu.” Elvin
akiwa haelewi chochote, alimsindikiza Bella kwenye gari yake, Bella akaondoka.
*********************************************
* Je Ni nini
kinachomuwahisha Bella? Na Wapi anawahi? Nani amemchukua Eric kutoka shuleni?
* Uchumba wa
Elvin nao umeanza kuingiliwa na Mikasa ya Bella
Mambo ndio kwanzaaaaa
yanaanza, Elvin akiwa ndio anaingizwa kwenye mkasa wa maisha ya Bella, ambayo
Mzee Masha hataki hata kuhisi kiumbe kingine kwenye maisha ya ENABELLA.
Ni nini
kitaendelea?
USIKOSE SEHEMU YA 6.
0 comments: