Story

Nilipotea! -PART 3 - Sehemu ya B.

Thursday, July 01, 2021 naomimwakanyamale 0 Comments

Tunda alichoka kabisa. Akidhani ile bibilia ingemtia hofu yule mzee, lakini ndio ikawa njia moja wapo ya kumtongozea. Akageukia dirishani. Moyoni akaanza kumwambia Mungu, ‘Nilikuomba unisaidie nisirudi huko tena, lakini mtu wa kwanza unanikutanisha naye baada ya maombi, ni huyu! Ni njia gani hii unatumia kunisaidia? Unanikutanisha na mtu kama huyu ambaye anauwezo wa kunipa msaada wa vitu unavyojua wazi ndio ninahitaji kwa sasa! Kwa nini hunihurumii? Nimeteseka miaka yote, ndio kwanza nafurahia utulivu nilio nao. Umenipa furaha na amani, kisha unachukua kila kitu kwa wakati mmoja! Umechukua kazi yangu, umenifukuza pale kwenye ofisi, halafu unaniletea mtu wakunisaidia kurudi kwenye yale yale maisha niliyokwambia siyataki!’ Tunda aliendelea kumlaumu Mungu kwa kunung’unika moyoni.

Akapitiwa na  usingizi, mpaka aliposhtuliwa na yule Mzee kumwambia ashuke wakale. Tunda akakataa. “Asante, lakini sitakula.” “Kwa nini?” “Nataka nipate muda wa kuongea na Mungu. Wewe nenda tu.” Yule Mzee alimtizama Tunda kwa muda mrefu kidogo, kisha yeye akashuka.

Alibaki peke yake kwenye basi, akafunga dirisha ili kupunguza fujo za watu wanaotaka kumuuzia vitu. Akainama nakuanza kuomba upya huku akijiuliza yeye mwenyewe maswali na huyo Mungu aliyetambulishwa na Net. Tunda aliomba huku akilia kwa hofu ya itakuaje. Akaendelea kumsihi Mungu asimjaribu zaidi. Alijua wazi mshahara aliolipwa na pesa nyingine alizonazo, haziwezi kudumu kwa muda mrefu.

Alifikiria wapi pakwenda mara baada ya kushuka kwenye hilo basi! Nini chakufanya mara baada ya kujua pakwenda! Yule mama alikuwa sahihi kabisa, hakuwa na cheti. Kama pale kwenye ile ofisi aliweza kufanya kazi vizuri, wakaona utendaji kazi wake na bado wakataka vyeti, nani atampa kazi bila vyeti wakati hawamfahamu? Maombi ya Tunda yalichanganyikana na maswali mengi sana. Alibaki ameinama ili aombe, akajikuta haombi tena anawaza tu.

 Tunda na fundisho la watoto njiani.

Aliamua kukaa vizuri na kugeukia dirishani aendelee tu kuwaza. Aliona watoto wadogo wawili wakicheza wakati mama zao wakiuza matunda. Mtoto mmoja alikuwa mkubwa kidogo kwa mwenzake. Yule mtoto mkubwa alikuwa na gari alilokuwa ametengeneza vizuri sana kwa vijiti, alivyovipangilia kwa ustadi, mpaka akatengeneza muundo wa gari. Akaweka matairi ya mifuniko ya soda{Visoda}. Tunda alimuona jinsi alivyokuwa akiendesha lile gari pembeni ya mama yake, akienda mbali kidogo na kurudi, lakini si mbali na macho ya mama yake.

Mtoto wa pili, yule mdogo, alikuwa akichezea vumbi tu, mwishowe yule mdogo akamuomba yule mtoto mwenye gari ampe achezee na yeye. Bila tatizo, akampa.

Yule mtoto mdogo, alionekana kufurahia zaidi lile gari kuliko mtoto mkubwa ambaye ni mmiliki. Alitoa milio mbalimbali kwenye mdomo wake kuonyesha akiigiza mlio wa magari ya kweli, kitu kilichomvutia Tunda na kuanza kucheka na kujikuta akifungua dirisha na kuendelea kumtizama yule mtoto aliyeazimwa gari. Alitoa mlio wa honi, kuweka breki kwa nguvu, huku akiendelea kucheza na gari ya mwenzake.

Mwenye lile gari alipoona yule mwenzake anafaidi na gari yake zaidi yake, akaamua ampokonye, tena kikatili, kwa jeuri kwa kuwa lilikuwa lake. Tunda akashtuka kwa kumuhurumia. Ulizuka ugomvi kati yao, lakini mwishowe mwenye nacho alishinda baada ya wazazi kuingilia kati.

Yule mdogo alianza kulia sana, akitaka lile gari ambalo halikuwa lake. Na yule mwenye nalo akaanza kuchezea kama yule mdogo alivyokuwa akifanya. Alitoa milio ileile, na alifanya zile zile mbwembwe kama mwenzake alivyofanya lakini haikupendeza hata kidogo. Mwishowe akaigiza kuweka breki kama yule mtoto, lile gari liligonga jiwe na kuharibika kabisa.

Lakini kabla ya lile gari kuharibika. Wakati yule mkubwa akiendelea kuchezea gari lake, yule mdogo aliacha kulia, akaokota boksi la biskuti, akatumia meno yake kutengeneza madirisha na mlango. Kisha akaokota pale pale vijiti vile vya kutolea uchafu kwenye meno ambavyo watu walisha tumia na kutupa tu. Akaunganisha kadhaa ili viwe virefu na vigumu. Akatoboa sehemu ya kuchomeka matairi, akaweka vile vijiti. Tunda bado akiwaangalia tu. Yeye ndani ya basi, wale watoto nje pembeni kwa mama zao, na wao wakiongea yao na kubembeleza wateja.

Kwa kuwa yule mtoto mdogo hakuwa na visoda, au mifuniko ya chupa za soda, yeye aliweka makaratasi magumu kidogo ndio yakawa matairi yake. Akaokota tena kijiti au mti mdogo, lakini mrefu na mwembamba akachomeka nyuma ya lile boksi, iwe kama usukani wake wakuongoza lile gari. Tayari akawa ametengeneza gari zuri tu, tena kwa muda mfupi, akaanza kuliendesha.

Wakati ndio analifurahia gari yake hiyo, ndio mwenzake akapata ajali na yakwake, ikaharibika. Kwa hiyo akabaki yule mdogo ambaye alinyang’anywa gari, akiwa na lake. Tunda alimuona yule mdogo akicheka sana. Akimcheka mwenzake, yule mkubwa aliyekuwa amekaa chini hana tena gari. Lilikuwa ni tukio la muda mfupi tu, lakini lilichukua akili za Tunda zote na kumfanya atulie na kutafakari.

            Basi lilianza kuondoka huku bado Tunda akiwawaza wale watoto. Alijiambia ni ujinga kuwaza jambo la kitoto kama lile, lakini bado akili ilimrudisha pale kwenye wale watoto. Akasikia swali mayoni mwake, Kama yule mtoto asingepokwanywa lile gari, je angepata wazo la kutengeneza gari lake?’ Tunda alifikiria kidogo akaamua kujijibu. ‘Lakini kweli! Afadhali alivyopokwanywa akapata akili ya kutengeneza gari lake.’ Tunda akajijibu. ‘Lakini alilia sana!’ Tunda akawaza kwa kumuhurumia yule mtoto.

             Likapita swali jingine. ‘Kama angeendelea kulia pale alipokuwa amekaa pembeni ya mama yake, bila kusimama na kuchukua hatua ya kutengeneza gari lake, angepata gari jingine?’ Tunda akafikiria na kukumbuka lile tukio tena. Alikumbuka jinsi mama yake alivyokuwa akimbembeleza kwa kumpa matunda ili atulie lakini yule mtoto alikataa kata kata, aliendelea kulia akitaka gari ya mwenzake mpaka alipoamua kunyanyuka na kutengeneza gari lake.

       ‘Afadhali alitumia akili. Angekubali tu kubembelezwa na mama yake akala yale matunda, angesahau kabisa kitu anachokita, gari. Akabaki hana gari mpaka sasa.’ Tunda akajijibu na swali jingine likamjia tena. ‘Kwani angekubali faraja ya mama yake, akaacha kutengeneza gari yake, ingeondoa ujuzi alionao wakutengeneza gari?’ ‘Hata kidogo. Si angekuwa ni mjinga tu, amekataa kutumia ujuzi wake na kubaki akililia gari la mwenzake!’ Tunda akajibu haraka haraka tena kwa hasira.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya hapo Tunda akapitiwa na usingizi, kisha akashtuka sana. Ikawa kama kitu kimemuamsha huko usingizini “Mimi ni mjinga sana, hata yule mtoto anaakili kunizidi mimi!” Tunda akamwambia yule Mzee na kumuacha akimshangaa. “Sipo hata nusu ya yule mtoto!” Tunda akarudia kumsisitizia yule Mzee, lakini yule mzee aliyekuwa amekaa pembeni yake akamtongoza, alijua Tunda anaota kwa kuwa alikuwa amelala. “Binti, punguza sauti. Ulikuwa umelala, na hapa tupo kwenye gari.” “Hapana sioti.” Watu wapembeni yao waliwageukia na wa mbele pia waligeuka kwani Tunda alikuwa akiongea kwa sauti iliyojaa kufunguka kimawazo.

“Ni kweli yule mtoto ana akili sana. Sikiliza nikwambie hiki kisa, kimetokea sasa hivi mliposhuka kwenda kula.” Tunda akasimulia kile kisa chote cha wale watoto na kuvuta masikio ya abiria wengi sana ndani ya lile basi. “Nisikilize vizuri. Mimi nimetoka Arusha sasa hivi sababu ya kufukuzwa kazi ambayo niliifanya vizuri sana. Sikuwahi kuiba, wala kukosea hata siku moja. Niliifanya kwa makini na juhudi zangu zote. Niliifanya ile kazi mpaka usiku bila kuomba malipo ya ziada.”

“Lakini leo asubuhi mwenye ofisi amemleta mtu mwingine, na kunifukuza mimi kazi kikatili, kwa kuwa tu sikuwa na vyeti.” “Kwa nini na wewe huna vyeti?” Yule Mzee aliuliza swali lililomfanya Tunda aliyekuwa akisimulia kwa kuchangamka apooze ghafla. Abiria wengine wakaongezeka kusikiliza. Maana wengi walikuwa wakisinzia mara baada ya kula chakula basi liliposimama. Ila kwa sauti ya kuchangamka ya Tunda, hata waliokuwa wamelala, wakaamka na kuendelea kumsikiliza Tunda aliyegutuka baada yakubaini ule mfano unamuhusu. Kwanza kwa sauti hiyo ya Tunda, lazima utataka kuisikiliza hata ukiwa mbali, utageuka tu ili kutaka kuiweka kwenye sura husika. Kuiona sura ya hiyo sauti.

“Sikusoma baba yangu. Nilipata hiyo bahati ya shule lakini ilichanganyikana na majanga mengi yaliyonifanya nishindwe kusoma kabisa. Sikubahatika kulelewa na wazazi wote wawili. Nimekuwa nikihama hama huku na kule.” Tunda akaelezea kisa chake kilichowavuta watu wote sasa kwenye lile basi huku wakimuomba aongeze sauti. Akapiga magoti kabisa kwenye kiti chake, nakusimulia. Wazazi wengine walianza kumtukana mama yake Tunda, wengine bibi, wengine mama wa kambo wengine shangazi ilimradi basi zima pakageuka kukawa gumzo juu ya Tunda.

 “Lakini baadaye niliishi maisha machafu sana, mpaka nikakutana na mtoto wa huyu mama aliyenifukuza kazi.” Napo hapo Tunda aliwaacha midomo wazi. “Mmmh! Pole sana mwanangu. Dunia mzunguko! Inaweza kukufanya ukafanya jambo ambalo hata hukutegemea.” Mama mmoja mtumzima pembeni yake aliongea.

“Ndio muache kuwasema machangudoa. Hamjui kwa nini wanafanya wanayofanya.” Dada mwingine kiti cha mbele alidakia. “Ndio maana yake. Maana kuna watu wanapenda kweli kuhukumu watu.” Mwingine akadakia. Abiria wengine wakawageuzia na wao macho kuwasikiliza na wao wakizungumza kwa jazba.

“Lakini mimi Mungu amenipa nafasi nyingine. Mtoto wa huyo mama alinirudisha kanisani, nikatubu, Mungu amenisamehe. Nilitolewa majini kwa mapepo kwenye huu huu mwili watu waliokuwa wakiutamani na kutumia. Wasijue walikuwa wakilala na majini pia. Anyways, baada ya yote, huyo kijana akanipa na hiyo kazi niliyopokonywa.” Tunda aliwakata maneno.

“Bahati yako wewe ulimpata huyo kijana. Sasa unakuta ndio kama hivyo mtu hana maisha, leo unamwambia aache uchangudoa, unataka aishije? Wewe umepata kazi, ndio maana umeacha.” Huyo dada aliongeza, kila mtu alihisi yule dada na yeye ni changu.

“Lakini nisikilize dada, nakwambia leo nimefukuzwa kazi. Hapa nilipo naelekea Dar, sina pakwenda, sijui chakufanya na wala simfahamu mtu yeyote huko Dar japo nimeishi kwa miaka mingi na nilikuwa na kwangu tena pazuri, kama nilivyowasimulia. Nipo kama hivi mnavyoniona.” Tunda akaendelea akiwa amejawa nguvu hata asijue amewezaje kuzungumza vile bila woga.

“Mlipokuwa mmeenda kula nilibaki humu ndani nikilia, ndipo nikaona kisa cha hawa watoto. Nikikwambia kulia, nilianzia kulia kule hotelini. Lakini huu mfano wa huyu mtoto mdogo, umenifundisha au unanihusu. Huku kulia kutanichelewesha na mimi kupata changu. Kurudi kuwa Changu ni kama nakubali faraja ya matunda ya muda mfupi, itakayonifariji kwa muda mfupi tu, nakusahau nini nataka katika maisha.” Tunda akaendelea.

“Lazima nisimame na mimi nitengeneze chakwangu. Hata kama sijasoma, na mimi nitaanza kwa kuokota maboksi, vijiti vyakutolea uchafu kwenye meno ambavyo watu wanatupa, nitatengeneza gari yangu kama yule mtoto.” Kisha akauliza swali. “Kwani huyu aliyetengeneza hili basi tulilopanda sasa hivi, si binadamu kama sisi tu? Alikubali kuacha vishawishi vyote, akajikana na kukaa chini, akaunganisha vyuma na mipira mpaka tukaliita basi.”

“Basi na mimi nitatafuta cha kwangu. Sitaki kulia tena wala kumchukia mtu. Nitajichelewesha kupata vyangu.” Tunda alishangaa kuona watu wote kwenye basi wakimpigia makofi. Alishtuka sana, kwani bado alikuwa amepiga magoti kwenye kiti chake akiongea kwa sauti na yule dada kwenye kiti cha mbele  kabisa aliyekuwa akitetea uchangu. Akawa kama ameshtuliwa, akarudi kukaa vizuri na aibu ya ghafla usoni.

“Unaakili binti. Nakupongeza.” Yule mzee aliyemtongoza na kumpa wazo hata lakumtafutia hoteli akajikuta akimpongeza tena Tunda. Lakini kwa sauti ya chini iliyojaa aibu kidogo na kujirudi. “Asante.” Tunda akacheka taratibu. “Na naomba nikuombe radhi.” “Wala usijali baba yangu. Ulikuwa mtihani wangu huo. Mungu alitaka kunipima, ajue nimeamua vipi kutorudi nyuma. Pale uliponiambia vile, ukaniona nimegeuka dirishani, nilikuwa nikimlilia Mungu aniepushe na watu kama wewe. Kwa kuwa ndivyo nilivyoanza kazi ya uchagudoa hivyohivyo.”

“Nilitoka hospitalini nikiwa sijui pakwenda. Wakati nimeenda kula mahali, nikakutana na mmiliki wa hilo eneo. Ndiye niliyeanza naye hiyo biashara. Akaniweka hotelini kama vile ulivyonishawishi mwanzo. Sasa na wewe ulivyonitongoza, na ahadi ya pakuishi, niliumia sana. Nikakumbuka niliingia kwenye ule uchafu mwanzoni kabisa sababu sikuwa na pakwenda. Sasa nikaona historia inataka kujirudia tena. Inakuwa vile vile na sababu ile ile. Ila nimekusudia baba yangu, sitarudi nyuma. Hata kama nitalala stendi ya mabasi, acha nihangaike tu mpaka nione mwisho ni nini.” Yule mzee alijisikia vibaya sana, na dhamira ikamsuta.

“Binti naomba unisamehe sana. Nimepitiwa na shetani tu.” Tunda akacheka. “Yameisha baba yangu.” “Ila kile chumba nilichokwambia ni kweli kilikuwepo, ila sijui kama dalali alishapata mteja! Kama upo tayari kuishi maeneo ya Temeke, naweza kumpigia simu yule dalali ili asikikodishe tena ili wewe ukaishi huko.” “Kodi ni kiasi gani?” “Yule mzee akamtajia.” Tunda akafikiria kidogo.

“Naomba nikulipe ya miezi mitatu wakati najipanga upya.” “Nitaongea na mke wangu tuone, maana ndio nyumba anategemea sana yeye.” “Unaweza kuwasiliana nao hao watu wawili ili mpaka tukifika Ubungo kituo cha mabasi, niwe najua kama nimepata au nihangaike kwingineko?” “Sawa.” Yule Mzee akakubali.

Alimpigia simu dalali, dalali akamwambia ndio ametoka kumpeleka mtu na mkewe hapo kwenye hicho chumba, wamepapenda na wamekubaliana kesho awapeleke kwa mke wa yule Mzee wakaandikishiane mkataba. “Basi hebu usubiri kidogo, usikikodishe kwanza niongee na mke wangu.” “Wanalipa kodi ya mwaka Mzee.” “Naelewa. Lakini hebu subiri.” Akakata simu.

“Vipi? Amesemaje?” Tunda akauliza kwa wasiwasi kidogo. “Anasema amepata mteja, tena mwenye kodi ya mwaka. Ngoja nimpigie simu mke wangu kwanza kabla hajawakodisha.” Tunda akakosa raha. Akabaki kimya.

“Mimi nitalipia hiyo kodi ya huyu binti.” Tunda akashtuka sana. Akamgeukia huyo aliyesema. Alikuwa ni kijana tu. Alikuwa amependeza, akaonekana nadhifu, kijana aliyefanikiwa. Shingoni alikuwa amevaa cheni aliyofanya juhudi za makusudi kuonekana. Ilikuwa dhahabu. Tunda muelewa vitu vya thamani, aliweza kutambua uhalisia wa ile cheni shingoni kwa yule kaka. Na saa nzuri sana tena ya thamani. Alikuwa amekaa kiti cha nyuma kabisa. Watu wote wakamgeukia.

“Kwamba?” Yule Mzee akauliza kutaka uhakika kabla hajazungumza na mkewe. “Nimesema mimi nitalipa hiyo kodi ya mwaka mzima ya huyo binti. Kama kumtia moyo kwa maamuzi magumu anayofanya.” Tunda aliogopa sana. Hakutaka kuja kudaiwa mapenzi baadaye. “Na wala hizo pesa hutazipata kwangu, utazikuta kanisani kwetu. Nitamkabidhi mama Mchungaji wetu. Utakapokuwa tayari, ukiipenda hiyo nyumba, wewe njoo kanisani kwetu utachukua pesa yako. Hata kama hutaipenda hiyo nyumba, tafuta nyingine, ila ujue pesa ya kodi ya mwaka mzima unayo tayari.” Tunda alianza kulia kwa furaha.

“Sikilizeni jamani.” Yule kaka akasimama. Akaanza kuongea mambo ya Mungu. Watu walikuwa wakimwangalia bila kupepesa macho. “Huyu Mungu yupo na wakovu ni halisi. Ukubali ukatae.” Yule kaka alianza kwa kusema hivyo.

“Wengine tumeua, tukauza madawa ya kulevya, tukavunja majumba ya watu, tumepita humo magerezani kama watu wanavyokwenda dukani kununua sukari, mpaka Mungu alipoingilia kati. Huyu dada anachoongea mimi namwelewa kabisa. Kuna mahali unapitishwa na maisha, msaada uliobaki pekee nikusalimisha maisha kwa Yesu. Ni uamuzi mgumu, lakini unalipa sana baadaye unapoamua kukubali nakubadilika.” Yule kijana akaendelea.

“Mimi nilipokubali kuokoka, nilipoteza kila kitu mpaka mke alinikimbia jinsi nilivyofilisika. Tena akaolewa na mwenzangu tuliyekuwa tukifanya naye biashara zetu za magendo. Nilirudishwa chini kabisa, nikawa masikini, omba omba. Nilikuwa na sababu zote zakurudi kufanya niliyokuwa nikifanya kwa kuwa nikweli nilikuwa nikitengeneza pesa ya haraka, lakini sikuwa na amani niliyokuwa nayo kama baada yakumpa Yesu maisha.”

“Wengi walinicheka na kuniambia nimepotea njia, lakini nilijua hawajui vile ninavyojisikia moyoni. Nilirudi kuosha magari Ubungo, mpaka nilipopata wazo lakurudi migodini kutafuta madini. Sikuwa na maandiko mengi kutoka kwenye bibilia, na nilikuwa mchanga sana Kiroho, lakini nilikuwa nikimkumbusha Mungu kuwa ‘fedha na dhahabu ni mali yake.’ Na mimi ni mali yake, nikawa nikimuomba Mungu anikutanishe navyo. Basi kila nilipokuwa nikizama kule machimboni nilikuwa nikimkumbusha Mungu hayo maneno. Ilinichukua miaka miwili migumu ya shida, nikiwa kule kwenye machimbo ya dhahabu, mpaka nikafanikiwa. Na mimi sasa hivi namiliki sehemu yangu huko.”

“Nilipochelewa ndege leo asubuhi, na kukosa gari ya kukodi kunipeleka Dar, nilipata amani sana yakupanda hili basi, kwani imekuwa muda mrefu, tokea nipande basi. Nimefurahi sana kukutana na huyu dada. Na inawezekana lilikuwa kusudi la Mungu ili nikutane na Tunda. Mungu akubariki sana dada yangu.” Akamtizama sasa Tunda, maana alikuwa ni kama anazungumza na basi zima.

“Hakuna sababu yeyote itakayokufanya kuishi kwenye dhambi na ikawa sawa. Hakuna. Hata ukijitetea vipi, hakuna. Dada Tunda nakuombea Mungu akutie nguvu, umeanza hii safari si rahisi, lakini Mungu hatakuacha, na kwa kuwa umefunguliwa ufahamu wako mapema, naona hutapata shida kama wengine.” Yule kaka akaendelea.

“Tatizo la wana wa Mungu wengi ni pale tunapoonywa na kukataa kubadilika. Au pale tunapoonyeshwa njia, tunakataa kufuata njia ya Mungu, na kutengeneza njia zetu. Tunachelewa na wakati mwingine hatufiki kabisa. Tunakubali faraja kama wewe ulivyosema. Faraja ya matunda, nakusahau vitu vikubwa tunavyotaka. Kama Mungu amekwambia akota boksi la biskuti utengeneze gari, okota na tengeneza. Acha ubishi, huwezi kujua katika kuinama huko, utaokota nini kingine!”

“Wengi wanapenda kuletewa wakiwa wanaomba Mungu. Haiwi hivyo kabisa. Muujiza wako uko pale unaponyanyuka na kuchukua hatua. Pengine yule mtoto asingekubali kutengeneza gari yake, ungekuta bado analia mpaka sasa, na asingegundua mbali ya vijiti, hata boksi pia linaweza kutengeneza gari. Tusibaki kung’ang’ania vya watu. Tutafute vya kwetu.” Yule kaka aliongea kwa mifano huku akisema maandiko kwa kichwa kitu kilichomshangaza sana Tunda.

‘Mwenzangu anaonekana amekaa kwenye wokovu muda mrefu! Anauwezo mkubwa wakusema maandiko ya bibilia bila kusoma!’ Tunda aliwaza. Alishangaa uweza wa kuchanganya kila analoongea na neno la Mungu. Ilimtia moyo sana Tunda. ‘Kweli huyu Mungu ana watu wengi! Wengine wanampenda na kuishi kwa dhati, wengine wanacheza. Ni uamuzi wako wa kuamua uishije naye.’ Tunda aliendelea kuwaza wakati yule kaka akizungumza mpaka akamaliza na kurudi kukaa nakuacha watu wote kimya kila mtu akitafakari lake.

Walipofika Ubungo, yule kijana akamsogelea Tunda, akampa kadi yenye mawasiliano ya Mchungaji wake. “Kuanzia kesho ukimpigia simu atakuwa na pesa yako. Mungu akubariki sana, na kamwe usirudi nyuma.” “Asante sana kaka yangu.” Yule kaka alikuja kufuatwa na gari nzuri ya kisasa, akaondoka. Tunda alibaki ametoa macho. Alipokea muujiza wake bila kutarajia.

Maisha yamrudisha Tunda Jijini Dar, Na bila kutarajia, katikati ya Jaribu kali, pakatokea mlango wake wakutokea.

Tunda hakutoka hata hapo kituoni Ubungo. Akaenda kwenye ile hoteli pale pale ndani ya Ubungo. Alishalala hapo na baba Tom, kwa hiyo alipafahamu. Akachukua chumba hapo. Kulikuwa kumejaa kumbukumbu ya mambo mengi aliyoyafanya humo ndani ya hiyo hoteli na baba Tom, lakini ikawa siku hiyo nayo amemuona Mungu. Akatulia kwa muda akiwa amekaa kitandani tu. Asiamini yupo hapo na hata siku hiyo, katikati ya jaribu gumu, lakini hana mtu anayetakiwa kumuhudumia kimapenzi ili kupata pesa.

Akajisiki machozi yakianza kumtoka. Akaamua kupiga magoti na kumshukuru Mungu huku akilia. Alikaa kwa muda mrefu magotini akilia mbele za Mungu wake, akaishia kujiambia hataweka kitu mdomoni mpaka mambo yake yakae sawa. Mpaka aushuhudie muujiza wake kwa macho. Ni kama aliamua kufunga.

Siku inayofuata, aliamua kutafuta sehemu ya kulipia ya kupiga simu. Akampigia simu huyo Mchungaji ili kujua kama kweli kuna pesa au la. Mchungaji akamwambia ni kweli mkewe alipewa pesa na kupewa maelekezo amkabidhi yeye. Tunda alifurahi sana. Kilichofuata ni kwenda kuona hicho chumba. Yule mzee wa kwenye basi mwenye nyumba alimpa namba yake ya simu na ya dalali. Alishazungumza na dalali, akamwambia atamsubiri Temeke hospitali ndio kituo atakachokitumia kufika kwenye hiyo nyumba.

Bila kupoteza muda, Tunda akiwa ameacha mizigo yake hapo hotelini, akapanda daladala mpaka Temeke kuona hicho chumba. Na kweli, aliweza kumtambua huyo dalali kwa nguo alizomwambia atamkuta nazo, kwa kuwa Tunda alimwambia hana simu, amwelekeze alivyo ili asimpotee. Akamchukua kutoka hapo kituoni mpaka kwenye hicho chumba. Tunda akaridhika nacho.

Akapapenda, akamuomba yule dalali atumie simu yake. Tunda akaongeza muda wa maongezi, akampigia tena simu yule Mchungaji, akampa namba ya simu ya mkewe. Tunda akampigia simu mke wa Mchungaji, yule mama akaamua amfuate.

Baada ya muda kama wa lisaa, alishangaa gari nzuri sana, SUV nyeupe, kubwa, imevimba vizuri, ikasimama mbele kidogo kituoni, pale pale Temeke hospitalini kama walivyokubaliana. Tunda na yule dalali wakamuona mwanamke akishuka kwenye hiyo gari. Alikuwa mtanashati, wakisasa. Akajitambulisha na kumwambia yeye ndiye waliyekuwa wakiongea naye kwenye simu, akamwambia wengi wamezoea kumwita mama Penny. Tunda akamsalimia na kujitambulisha na yeye.

Yule dalali akawapeleka kwa mwenye nyumba. Hakuwa akiishi mbali na hapo. Mama mchungaji akalipa ile kodi yote, Tunda akakabidhiwa funguo.

“Una kitanda?” Mama Penny akamuuliza wakati akimrudisha Tunda hotelini. “Ndiyo. Nina kila kitu, lakini nimefungia mahali. Itabidi kesho nitafute gari nihamie kwangu.” “Usiwe na wasiwasi, nitawatuma vijana wa pale kanisani na gari ya kanisa ikusaidie kuhama.” Tunda hakuwa akielewa kinachomtokea.

Akamgeukia mama Penny. “Nakushukuru sana dada yangu. Mungu akubariki. Asante kwa kila kitu.” “Karibu.” Alijibu kwa ufupi tu. Akamshusha hapo hotelini Ubungo, akaondoka na kumuacha Tunda na funguo za chumba chake na sebule.

Ile furaha ikageuka kilio kwa Tunda. Alilia Tunda, asiamini kama Mungu amemrudishia kwake. Kwa Tunda huo ulikuwa ni muujiza wa kama kumfufua maiti. Ilikuwa ni zaidi ya kuponywa. Historia yakufukuzwa kwenye majumba ya watu, kwa Tunda, haikuacha kujirudia.

Ametoka kufukuzwa kwenye nyumba ya watu Arusha. Mama Cote alimtoa nyumbani kwake usiku. Akampokonya chumba alichopewa na Net, funguo za gari na kazi. Anampa nini huyo Mungu kumfungulia mlango mkubwa kama huo! Tunda alilia, asijue nini chakusema mbele ya huyo Mungu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake asubuhi alipigiwa simu na mtu wamapokezi kuwa anamgeni pale mapokezi. Alipotoka alishangaa kukutana na mama Penny na vijana. “Uliamka salama?” “Ndiyo. Japo sijala.” “Sasa itabidi ujikaze. Nimewakamata hawa vijana wakusaidie kuhama kabla siku haijaanza, wakakimbilia kwenye majukumu yao. Wakishakuhamisha ndipo tutatafuta sehemu ya kula.” “Sawa. Nashukuru sana.” Tunda akachukua mizigo yake yote aliyokuwa nayo pale hotelini, wakaweka kwenye gari ya mama Penny. Akalipia kile chumba, wakaondoka pale.

Tunda alikuwa kwenye gari ya mama Penny, na wale vijana walikuwa wakiwafuata nyuma kwenye gari kubwa kidogo, aina ya Kenta. Walitoka hapo Ubungo kuelekea Salasala nyumbani kwa Net alipokuwa ameacha vitu vyake.

Walipofika pale, akawaambia wasubiri nje akagonge kwanza. Aliwaambia hiyo nyumba inalindwa na mbwa mwenye mafunzo ya kijeshi. Ndiye Max. Tunda alishapewa habari za Max. Net alikuwa akimsifia sana huyo mbwa. Alikuwa akisema kwa huyo mbwa mmoja tu kulinda hiyo nyumba yake, ni sawa na kulindwa na askari watatu wa kimarekani, tena waliokwisha kwenda kupigana vita huko Iraq. Huyo Max alikuwa akihudumiwa nakutunzwa kwa hali ya juu.

Tunda aligonga kengele nje ya geti, baada ya muda Emma akatoka. Wakasalimiana, akamwambia bado Net hajarudi nchini. Akamweleza kuwa amefika hapo na wale watu kuchukua baadhi ya vitu vyake. Emma alikwenda kumfungia Max, ndipo akarudi kufungua geti na ile sehemu alipohifadhiwa vitu vyake.

Kutokana na ile sehemu kuwa ndogo sana, ilimbidi Tunda kuchukua vitu baadhi, vingine akaacha pale pale. Emma alivifunika vile vilivyobaki kama mwanzoni ili visiingie vumbi, wao wakaondoka. Huku Tunda akiviambia vitu vyake vilivyobaki pale kwenye stoo ya Net, ‘ipo siku tutarudi kuwa pamoja. Nipeni tu muda.’ Roho ilikuwa ikimuuma sana Tunda. Ni kweli alikuwa na vitu vizuri. Hata wale vijana waliokuwa wakimsaidia kubeba, walisifia na kuongeza umakini kwenye kubeba.

Walimrudisha mpaka Temeke kwenye chumba chake, wakamsaidia kupanga vile vitu, kisha wale vijana wakaondoka. Tunda alikuwa akicheka sana jinsi wale vijana walivyokuwa wakitaniana na mama Penny. Walionekana wamezoeana vizuri. Yule mama alipohakikisha Tunda ameweka kila kitu chake vizuri, alimchukua mpaka nyumbani kwake Tabata.

Walimkuta dada wa kazi, akiwa anaandaa chakula cha mchana. Na yeye yule mama akaingia jikoni nakuanza kumsaidia yule dada huku akimuuliza maswali Tunda. Baada ya muda mfupi sana, Tunda akajisikia yupo nyumbani. Mama Penny alikuwa mcheshi wakupitiliza.

Mchungaji naye akaingia. “Wewe siulikuwa ukicheka kila ninaloongea? Sasa kaja mwenyewe, utapasuka mbavu.” Tunda alikuwa akicheka sana. Mchungaji na mkewe walikuwa kama ni mtu na rafiki yake. Walitaniana kwa kila kitu.

“Hivi kuna wakati huwa wanakuwa serious hawa?” Tunda alimuuliza msichana wa kazi.  “Mmh! Sikumbuki. Labda wakiwa kanisani kidogo, lakini watu wameshawazoea. Mtakaa mkicheka hapa, mpaka mnaenda kulala. Hawaishiwi maneno hao na vituko.” Tunda alikaa hapo mpaka usiku akarudishwa kwake na yule mama.

“Kesho unaratiba gani?” Yule mama akamuuliza Tunda kabla hajashuka. “Bado natafuta kitu chakufanya.” “Sasa mimi ninafanya kazi ya kupamba kumbi za sherehe. Kesho nina kwenda kupamba ukumbi mahali. Kuliko ukae tu nyumbani, ni heri twende wote. Mimi sipendi watu wanaokaa kaa kihasa hasara, mwishowe shetani anapata nafasi ya kukupa kazi zake.” Tunda akacheka.

“Unafikiri nakudanganya? Shetani anapenda mijitu isiyo na kazi. Iliyokaa kaa tu haina kazi zakufanya, ndiyo anaanza kuipa kazi zakijinga.” “Basi tutaenda wote dada yangu.” Yule mama akacheka kidogo kama aliyefurahia utayari wa Tunda.

“Sasa mimi mambo yangu ni asubuhi ili jioni niwe na familia yangu. Kwa hiyo asubuhi nakuja kukufuata. Au unasemaje?” “Sawa kabisa.” Yule mama akacheka, akafungua loki ya mlango pembeni ya mlango wake, ndipo Tunda akaweza kufungua  mlango wake, wakaagana na kushuka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alianza kulia tena mara baada yakufika chumbani kwake, akapiga magoti pembeni ya kitanda chake. Alishindwa hata kumwambia Mungu asante. Alibaki amepiga magoti akilia. Moyo wake ulijaa shukurani sana mbele za Mungu. Nyumba ilikuwa nawapamgaji wengine wanne, wote walikuwa na familia kasoro Tunda. Ilikuwa uswahilini tu, tena wala si uzunguni kama alikokuwa akiishi karibu na baharini.

Uswahilini hapo ni kelele mida yote tena kitanda chake kiliwekwa pembeni ya dirisha alilokuwa akisikia kila kitu wapita njia wakizungumza nje. Choo anatumia na watu zaidi ya 15. Alishaambiwa kuna zamu za kusafisha sijui choo, uwanja na mambo mengi. Ni maisha ambayo hakuwahi kuishi binti huyo. Lakini alijawa na furaha ya aina yake. Alikubali yote bila shida. Furaha aliyokuwa nayo moyoni, ni kama alipewa jumba la thamani sana.

Alipanda kitandani kwake, asiamini kama amerudi kukilalia kitanda hicho alichokipenda na kukithamini sana. Aligaragara kwenye hicho kitanda akinusa hayo mashuka yake kwa furaha sana. Akaanza kuongea na vitu vyake kama binadamu. Akakumbuka kazi aliyoambiwa atafuatwa asubuhi asubuhi. Ikabidi alale haraka ili aamke akiwa na nguvu.

Tunda aanza Safari ya Kupata chake. Bila kujijua, kwa kutii agundua kipaji chake.

Aliamka asubuhi na mapema kuwahi kuoga kabla wengine hawajaamka na watoto wao, akachelewa. Akaoga na kuvaa akabaki kwenye kiti akimsubiria mama Penny. Akasikia mlango wa bati, mdogo tu wakuingilia ndani ukigongwa, akajua ni mama Penny. Akatoka akiwa amebeba na pochi yake, ni kweli alikuwa mama Mchungaji. Wakasalimiana, wakarudi kwenye gari na kuondoka. Na hilo likamfurahisha mama Penny, hakutegemea kumkuta akiwa tayari kwa kiasi hicho.

Waliongea mambo mawili matatu mpaka walipofika kwenye ukumbi wenyewe. Ulikuwa ukumbi wa kawada sana huko Mbezi ya kimara. “Si unaona hili liukumbi lilivyo baya? Sasa utaona nitakavyo pabadilisha mpaka wenyewe watashangaa.” Akajisifia yule mama. Wale wale vijana waliomuhamisha Tunda jana yake, waliingia na ile ile gari iliyomuhamisha Tunda siku iliyopita, ila safari hii ilibeba viti vya maharusi na mapambo. Walianza kushusha huku wakiendelea kutaniana.

“Leo mama wametupa godauni.” “Hilihili leo, mpaka paeleweke hapa! Masaa matatu tu, tunaondoka humu ndani. Nataka nikampikie mume wangu ugali wa bada. Mnaujua lakini bada au mnanitolea mimacho tu?” “Umeanza mama Penny.” “Kumbe! Ndio muoe muache kula magengeni! Wakati wenzenu wanaoa nyinyi mmekazana mnaomba. Mtaomba mpaka Yesu anarudi anawakuta bado mnaomba. Hebu njooni tuombeni kwanza ndio tuanze kazi.” Wote walikuwa wakicheka.

Tunda alikuwa akiwashangaa furaha waliyonayo na yule mama. Wakashikana mikono, wakaanza kuomba kwa pamoja ndipo wakaanza kazi. Walianza kazi kwa nguvu zote. Wale vijana wakijua chakufanya. Na kweli baada ya masaa matatu na nusu ule ukumbi ulibadilika kabisa. Walianza kupongezana. Mama Penny akawalipa pesa yao pale       pale wakaagana.

“Na wewe hii ndiyo pesa yako.” “Wala sijafanya kazi kubwa sana!” Tunda alitaka kukataa. Yule mama akambadilikia. “Huwa sipendi watu wajinga. Unanisikia Tunda? Kila mtenda kazi anastahili ujira wake. Au husomi bibilia wewe?” “Nasoma.” “Sasa!? Au maandiko ya bibilia yalisema kila mtenda kazi sana ndiye anastahili ujira? Acha kuzubaa! Mjini hapa. Kusanya pesa, jenga nyumba, nunu magari ya maana, uache kuishi uswahilini. Unafikiri nitakuwa nakuja kukuchukua kila siku?” “Hapana.”

“Ndio unatakiwa uchangamke, unasikia? Umelipiwa kodi mara moja tu, ujue inayofuata ni juu yako. Huwezi jua. Mara nyingine Mungu anatokea mara moja tu, na akitokea usiachie hiyo bahati. Sasa hivi unakusanya kila kinachoingia. Hata kama kidogo. Halafu huwezi jua hii ndiyo inaweza kuwa ajira yako. Au unaonaje?” Yule mama akamuuliza.

“Nimeifurahia sana.” “Basi jipe muda. Omba Mungu hizi tenda ziwe nyingi, ujifunze kwa haraka, na wewe uwe na yako kama hii.” “Kama hii tena, sio uniajiri?” “Wewe mtoto wa wapi lakini!?” Tunda alitulia kidogo. “Mbona neno ‘changamka hapa mjini’ ni kama hulielewi!? Wewe Dar yote hii unafikiri harusi leo zinafungwa ngapi, au kuna sherehe ngapi zinazotaka wapambaji?” Tunda akacheka baada ya kufikiria kidogo.

“Muone kwanza! Ushapata jibu eeh? Sasa ndio uchangamke haraka, jifunze, pata ujuzi halafu unachanganya miguu. Sio ukae hapa unasubiri ajira. Nikikufukuza kama yule mama wa Arusha? Unahama tena kuajiriwa kwengine? Hapo Mungu alikuwa anakufungua macho anakwambia uwe na chako! Shule sio kila kitu. Mwenzio nimesoma, lakini napamba maukumbi. Naingiza pesa nyingi tena kwa muda mfupi. Umeona kuna sayansi niliyotumia hapa? Ujuzi tu na utundu.” Akawa ni kama anamfungua akili zaidi Tunda.

“Asante sana.” “Asante kavukavu tu?” Mama Penny akamuuliza Tunda, akaanza kucheka tena. “Sasa nifanyaje?” “Ukipata tenda ya kwanza unaninunulia pafyumu nzuri. Sio zile zakuita nyuki au kuleta mafua.” Tunda aliangua kicheko zaidi, wakaondoka pale.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Yule mama alikuwa akifahamika sana. Kwa juma moja hakuacha kupamba kumbi si chini ya tatu. Kuanzia kichen party, send off, harusi, na kila shughuli zilizokuwa zikihitaji wapambaji, aliweza kupata yeye hizo tenda, mpaka alikuwa akikataa. Alikuwa akiingiza pesa nyingi kwa juma.

Kwa kuwa alikuwa na watoto wadogo na huduma ya kanisani, mara nyingi alimtuma Tunda kwenye vikao vya harusi kwenda kuonyesha picha za kumbi walizokwisha kupamba na kuongelea gharama. Baada ya muda mfupi kweli Tunda akaanza kuwa mwenyeji na mjuzi wa ile biashara.

Akajiongeza. Akatengeneza albamu nyingine. Akapangilia picha na bei vizuri. Ikawa rahisi kila akitumwa na mama Penny, anaonyesha picha na bei. Kwa muda mfupi Tunda akaonekana amefikishwa kwenye uwanja wake anaomudu. Yeye ndio mtoa ushauri kwa mama Penny, kitu kilichomfurahisha sana mama Penny. Lugha nzuri ya biashara akawa anayo. Hakuna alikotumwa kwenye vikao viwe vya harusi au kiofisi, akarudi bila hiyo kazi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 “Sasa tunaanza kugawana. Wewe unapamba huku na mimi napamba kule.” Tunda akaingiwa hofu. “Yaani bila wewe? Sitaweza peke yangu.” “Wewe mtoto vipi!? Hata watoto wachanga huwa wanaacha kunyonya. Ulipokuwa ukikubali kupokea kazi za watu, tena nyingi kwa tamaa, ulifikiria nini? Unataka tuongozane kama makondoo mpaka lini!? Kwanza mimi huwa sipendi kufuatwa fuatwa nyuma.” “Nikiharibu sasa?” Tunda alijawa na wasiwasi.

“Shauri yako! Mimi hainihusu. Itakuwa ni juu yako wewe na hao waliokupa kazi. Mimi nachukua ukumbi mmoja tena wakaribia na kwangu, nikimaliza kazi yangu nitakupigia simu bosi wangu uje ukague, ukiridhika nataka pesa yangu uliyolipwa.” Tunda akazidi kuchanganyikiwa.

“Sasa na ule ukumbi wa tatu nani atapamba?” “Kwani wewe ulivyochukua kumbi tatu, kwa siku moja, ulitegemea nini? Mwenzio nina mume na watoto. Kazi yangu moja tu kwa siku na wewe unajua. Ulivyochukua kazi zote hizo, ulifikiri nini?” “Jamani mama Penny!? Basi tufanye wote hizi zote halafu siku nyingine nitajipanga vizuri.” Tunda akabembeleza akiwa na hofu.

“Akuu wewe mtoto usinivunjie ndoa yangu. Baba paroko unamsikia Tunda.” Yule mama alimwita mumewe. “Atalijua jiji! Na akikutana na walevi lazima wamshushie kipondo kama ukumbi haujaisha kwa wakati.” Mchungaji na mkewe wakaanza kumcheka Tunda, huku wakikumbushiana visa vya kazi hiyo ya upambaji kama wahusika wanakuwa hawajaridhika na kazi.

“Sasa nitafanyaje?” Tunda akauliza akilalamika. “Omba funguo za ukumbini ukalale nazo kwako. Amka hata saa kumi za usiku, nenda kaanze kupamba. Tena nakupa Josh na Julius wakusaidie. Wote wale wachapa kazi. Ukiamka mapema kwenye saa kumi jioni, utakuwa ushamaliza kupamba kumbi zote mbili.”  Hilo likamfurahisha Tunda.

“Sasa mapambo?” Tunda akauliza tena. “Mapambo!?” Mama Penny naye akauliza kama anayemshangaa. “Nauliza mapambo nitapata wapi?” “Piga magoti uanze kuyaomba kwa Mungu. Utakuta Mungu kakushushia huko huko ukumbini yanakusubiri. Kila ukumbi atakuwekea mapambo yake. Anza kuomba.” “Jamani mama Penny!” Kila mtu akaanza kucheka mpaka msichana wa kazi jikoni.

“Kumbe! Wewe hujui hii ni nyumba ya Mchungaji? Hapauzwi mapambo hapa. Ushauri utakaopewa ni kuomba. Ukiona hapa unabanwa, rudi kwako kule uswahilini, kwenye kelele, kajifungie anza kuomba kwa kulia.” “Au piga magoti nikuwekee mkono Tunda.” Mchungaji akaongeza. “Jamanii!” Tunda akazidi kulalamika.

“Changamka Tunda. Mjini hapa!” “Basi naenda kununua vitu vyangu.” “Kumbe unaakili?” “Usafiri sasa?” Tunda akauliza tena. “Piga magoti Mchungaji akuwekee mikono ili mkimaliza kuomba, ulikute gari hapo nje linakusubiri.” “Jamani mama Penny wewe!” “Kwani wewe huamini nguvu ya maombi? Au hujasikia kama kuna miujiza?” “Naamini lakini si kihivyo!” “Basi changamka. Una siku tatu za kukamilisha kila kitu uingie kazini.” Tunda akaondoka.

Tunda aanza biashara yake ya kupamba.

Usiku huo hakulala. Akaanza kuandika kila kitu alichokiona kwa yule mama, ambacho alijua atakihitaji na yeye. Kesho yake asubuhi akaanza kuzunguka madukani akiwa na Julius ambaye ni mpambaji wa mama Penny na ni dereva wa ile Kenta.

Akaanza kununua vitu kama vile alivyoviona kwa mama Penny. Anamwita Julius, anasogeza gari, wenye duka wanamsaidia kupandisha vitu kwenye gari, Julius anamsubiri, yeye anazunguka madukani peke yake.

Viti vya kukalia maharusi ndivyo vilimtoa jasho. Alitaka kama vya mama Penny, ila bei ilikuwa kubwa. Akaanza kujishauri akikumbuka akiba ya pesa aliyokuwa nayo. Inamaana kazi yote tangia aanze kazi kwa mama Penny na ile aliyolipwa Arusha, itaishia hapo kwenye manunuzi! Akajishauri Tunda. Lakini alitaka awe anafanya kazi nzuri kama mama Penny. Ikabidi ajikaze tu, anunue kila kitu vile vile na vizuri zaidi, mpaka akaishiwa kabisa.

Walirudi nyumbani kwa mama Penny na mchungaji  Tabata akiwa na mizigo yote aliyokuwa amenunua Tunda. Tunda mwenyewe alikuwa hoi. Amechoka na ule weusi ukaongezeka kwa kupigwa na jua pamoja na vumbi.

          “Naomba unikopeshe pesa nikaongeze kwenye mapambo.” Mama Penny akaanza kucheka. “Umeshaanza kupata akili eeh? Safi sana. Sasa hapa kwetu kukopa ni mara  moja tu, na unalipa ndani ya juma moja. Ukizidisha siku saba unaanza kulipa na riba.” “Mama Penny jamani!?” “Haya nenda kakope kwenye mabenki.” 

“Haya basi nitakulipa nikilipwa baada ya kupamba.” “Hiyo ndio akili. Sasa uchangamke na siku za alhamisi na ijumaa hapa mjini pia kunakuwa na sendoff na Kitchen party. Zote hizo siku hakikisha unapata kazi.” “Si nitachoka sana!” Tunda akashangaa. “Sawa. Nenda kalale. Kwanza hivi umepaona nyumbani kwake?” Mama Penny akamuuliza mumewe.

“Hapana.” “Kama chumba cha mbwa! Hapafai.” “Jamani mbona pazuri tu.” “Kama pazuri mbona mizigo yako ipo hapa? Si ungetoka Kariakoo na kuipeleka kwako?” “Mama Penny wewe? Pale padogo halafu nahofia wezi.” “Sasa unakataa nini na unaongea nini hapa? Dari lenyewe limeshuka mpaka mlangoni! Yaani kuingia inabidi uiname na unakuwa kama unatumbukia ndani hivi. Tena kama wewe baba Paroko na miguu mirefu hiyo! Lazima uiname ndio uweze kuingia mlangoni, na ukifika ndani itakulazimu kukaa tu. Lasivyo utagonga dari.” Tunda alianza kucheka huku anatingisha kichwa.

“Nitahama bwana.” “Utahama bila pesa? Nakwambia fanya kazi kwa bidii. Unasema utachoka! Tena kesho kuna kazi nimepewa ni kupamba ukumbi wa tamasha, pale Mlimani City, sitaweza kwenda namsindikiza mume wangu kwenye huduma Morogorooo. Sasa itabidi uwahi ukapambe na hao vijana.” Tunda akachoka kabisa.

“Utaniua mama Penny! Mlimani City? Nikiharibu?” “Ndio utakuwa umeniharibia biashara. Na tunakuomba ule uondoke Tunda. Nina mazungumzo ya faragha na mume wangu.” Msichana wa kazi alikuwa akicheka muda wote.

“Sawa bwana.” “Na tunakupa miezi miwili tu, hakuna tena kutumia gari yetu kubebea vifaa vyako vya kupambia. Tafuta gari yako, mrembo. Mjini hapa, watu tunaishi kwa mahesabu. Hakuna kuomba chumvi kwa jirani.” “Gari!?” “Na hivyo vifaa vyako hapo stoo, kuanzia mwezi wa kumi na mbili utaanza kulipia hicho chumba.” “Jamani mama Penny wewe!?”

“Sitaki hodi za asubuhi asubuhi wakati unakuja kuchukua vifaa vyako ukapambe. Ni usumbufu Tunda.” “Si kwa muda tu!” “Muda wenyewe ndio nakwambia mwisho ni mwezi wa kumi na mbili. Kwa hiyo wakati unapumzika huko kwako hutaki kufanya kazi kwa bidii, ujue unatakiwa gari na nyumba kubwa.”

“Patamu hapo. Na vyote hivyo si chini ya mamilioni ya pesa. Ukiiba tu, sisi tunakutenga. Ukihongwa tu, mimi Mchungaji nakupandisha madhabahuni nakutangaza kuwa wewe ni mzinzi, kisha nakutenga mbele ya watu.” Mchungaji akaongeza. Yule mama alisaidiana na mumewe kumshambulia Tunda.

“Hivi nyinyi mlikutana wapi?” Iliibidi Tunda kuuliza jinsi wanavyopokezana maneno kwa kupatana, kama wamepanga. “Maana mnafanana kila kitu!” Wote wakacheka. “Kanisani. Mimi nilikuwa kiongozi wa vijana, na bibie hapa alikuwa ndani ya kundi. Akanipenda ndio nikamuhurumia nikamuoa.” “Uringe. Alihangaika huyu, muone maneno mengi hivyo hivyo. Nilimtoa jasho!” Tunda alikuwa akicheka sana.

          “Kwa hiyo mlianzana tokea wadogo?” “Nimemfundisha hesabu za sekondari huyo, usimuone hivyo. Nilivyomuona anapenda pesa, nikaona nioe kabisa ili yeye awe anatafuta pesa mimi nahubiri injili. Ukimfatilisha huyu, ndani ya miaka miwili utakuwa mbali sana Tunda. Kazana, jiamini, utaweza tu.” “Umesahau kumwambia na awe anatoa fungu la kumi kanisani.” Mama Mchungaji, yaani mama Penny, akaongeza, nakumfanya Tunda aangue kicheko zaidi.

“Na sadaka kubwa kubwa. Umesikia Tunda? Sio zile sadaka unatumbukiza kwenye kapu la sadaka umekunja ngumi. Na baraka za Mungu zitakuwa ndogo ndogo hivyo hivyo”  “Nitatoa.” Tunda akakubali akicheka

 

Tunda aanza kupambana jijini.

Mwanzo wa Tunda haukuwa rahisi hata kidogo. Ilikuwa kazi tu. Hakuna masaji wala kutengeneza kucha na kubadili nywele kila week. Alianza kufanya kazi kwa bididii zote, akili ikiwa imetulia kazini asiharibu. Ndani ya juma moja alikuwa akipata kazi si chini ya nne. Zote hizo anasukumiwa na mama Penny. Kuna siku nyingine alikuwa akipamba kumbi mbili mpaka tatu.

Tunda akawa busy. Mchana na usiku yupo na kazi. Hakuna waxing tena kwenye huo mwili kutoa vinyweleo. Kazi tu. Anasaka pesa kwa juhudi zote. Na Mungu akawa akimfungulia milango kwa namna ya ajabu. Akawa ni kweli anapata kazi. Kila akijisikia kuchoka na kutaka kukataa kazi, alikuwa akijisuta na kukumbuka maisha yake. Basi anatoka kitandani bila hata alam.

Alianza kuingiza pesa na kufahamika mjini kwa kazi nzuri ya upambaji. Na akaongeza uaminifu kama mama Penny. Mkikubaliana aina fulani ya mapambo, basi ujue atakuwekea hayo hayo mapambo. Kama ni maua Rose, ujue hatachanganya wala kukuibia. Uwe na pesa usiwe, basi atakupambia kutokana na pesa yako na vile mlivyokubaliana.

Alipata familia kubwa pale kanisani kwa kina mama Penny. Tunda alijawa furaha, upweke wote ukaisha. Akawa mtu wa furaha wakati wote, na nyumbani kwa mama Penny ikawa ndio kituo chake kikubwa. Na mama Penny akafanyika dada kweli kweli. Ukimkosa Tunda kwenye simu, muulize mama Penny. Mchana na usiku wawili hao walikuwa wakiwasiliana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya mahangaiko mengi akichapa kazi mchana na usiku, akafanikiwa kuhama Temeke, akapata nyumba. Haikuwa nzuri kama ile aliyoishi La dolce Vita, lakini ilikuwa na ukubwa unaolingana na ile. Vyumba viwili kama ile, inajitegemea, maeneo ya Kimara, karibu sana na Ubungo. Akaenda kuchukua vitu vyake vyote kwa Net, akahamia kwake. Akaongeza bidii ili kupata usafiri pia. Kazi akafanya mchana na usiku bila kuchoka wala kulalamika. Hakuna tenda yeyote alipata akaacha.

Alipopata pesa, mama Penny akamsindikiza Tunda kununua gari. Kwa kuwa alikuwa na mambo mengi, alinunua gari nzuri lakini sio kama ile ya Mama Mchungaji iliyokuwa ya aghali sana. Tunda akapata usafiri wake wakumzungusha mjini.

Kila mama Penny alipopata kazi nyingi alimpa na yeye. Watu wakaanza kumfahamu yeye kama Tunda sasa. Akaanza kutafutwa yeye kama Tunda sio kwa kupitia tena mama Penny. Na kazi zake zilikuwa nzuri sana. Akaanza kuuzika kama Tunda, na watu wakaweza kutambua kazi zake.

Hakuwa amesoma, lakini kwa hakika kile kilikuwa kipaji chake bila kuuliza. Kilijionyesha kwenye kila kumbi aliyokuwa akipamba. Alijiongeza na ungeweza kutofautishi ukumbi aliopamba yeye au mama Penny, japo walitumia karibu kila kitu kinachofanana. Kipaji chake cha upambaji kilimkutanisha na watu waina mbali mbali. Wasomi na wenye pesa. Wake za mawaziri na mabalozi.

Alipoona kazi inakuwa kubwa, hana haja yakusaka kazi, zinamfuata tu, akatafuta ofisi na kuajiri watu wawili waliokuwa wakipokea kazi kutoka kwa watu. Alifungua website ambayo ilijaa picha zakuonyesha kazi zake. Kwa muda mfupi sana Tunda akawa mashuhuri pale jijini. Lakini katika yote hakuacha kuwa karibu na Mungu wake. Msingi wa kusoma bibilia na kuomba aliokuwa amefundishwa na Net, hakuacha hata kidogo. Kila akirudi nyumbani kwake, atapiga magoti na kuomba Mungu japo kwa ufupi.

 

Kwa Mara ya Kwanza, Tunda amsaka  baba yake jela.

Alianza kuulizia kwenye magereza ya pale mjini, kutaka kujua alipofungwa baba yake, mpaka akajua kule baba yake alipokuwa amefungwa na siku ambazo wanaruhusiwa kutembelewa. Akaamua kwenda kumtembelea baba yake huko gerezani Segerea. Baba yake alifurahi sana kumuona Tunda. Lakini alikuwa amedhoofu na hakuwa na furaha hata kidogo.

“Wamenisingizia mwanangu. Kwa kuwa sina hela, nashindwa kutafuta mwanasheria mzuri wakunitetea.” “Mimi nitakutafutia baba.” Hilo likamfariji sana baba yake. Mtoto ambaye hakuwa hata anamtegemea, ndio anaahidi kuwa mkombozi! Akashukuru.  “Unafanya nini sasa hivi? Umependeza mama.” Ilibidi baba yake kuuliza. Maana ni kweli Tunda alionekana ametulia na pesa ipo.

Swali alilokuwa akilikwepa wakati ule akizunguka na wanaume, ndilo hilo baba yake anamuuliza. Lakini safari hii akamjibu baba yake kwa ujasiri wote. “Mungu ananilinda na kunitunza kwa namna ya ajabu baba! Mimi mwenyewe bado nipo kwenye mshangao baba yangu. Napamba kwenye kumbi za shuguli mbali mbali! Na wala sikurudi shule. Nilifundishwa tu.” Tunda akamuelezea juu ya wakovu aliopokea, familia ya mama Penny na mafanikio yake. Baba yake akafurahi sana, wakawa wanaongea mpaka muda ulipoisha, Tunda akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alianza kuzunguka kwenye ofisi za wanasheria pale mjini. Akiongea nao, kuona kama wataweza kumsaidia baba yake. Akiwa anajaribu kwenye ofisi nyingine, sekretari wake alimpigia simu kumwambia yupo mtu amesema anataka kuongea na yeye mwenyewe. Tunda alichukua ile namba akapiga.

Walimuomba huduma yake ya upambaji na kumtaka afike kwenye moja ya kikao chao cha ijumaa ili kuongea na wanakamati.  “Mlishaona kazi zangu lakini? Maana mnaweza kupitia kwenye website yangu, mkachagua muundo mnaoupenda, kisha unapiga simu ofisini onatoa oda yako. Sio lazima mimi nikawepo kwenye kikao.” “Tungependa kukuuliza maswali kabla ya kuchagua.” Tunda akakubaliana nao muda na eneo atakalokwenda siku hiyo ya ijumaa kukutana na wanakamati wengine.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilikuwa siku hiyo ya ijumaa jioni, Tunda akiwa amejitayarisha vizuri kwenda kuonana na wanakamati hao. Alikuwa na kazi moja tu siku hiyo. Alishakamilisha tokea asubuhi. Akarudi nyumbani, akapumzika na kujiandaa tayari kwa kikao cha jioni. Kama kawaida yake, hakuwa akifanya makosa kwenye mwili wake. Alipendeza sana, akachukua picha zote alizojua angehitaji kuvutia wateja wake, akaelekea kwenye kikao.

Eneo tu walilokuwa wakikutania hao wanakamati, Tunda alijua watakuwa na pesa. Aliingia kwenye hoteli hiyo iliyokuwa Masaki, akasalimia pale mapokezi, kisha akampigia simu mtu aliyekuwa ameongea naye kwenye simu, akafika pale mapokezi kumchukua.

Tunda alimuona yule kaka jinsi alivyobabaika baada yakumuona. Akaongeza ujasiri. Wakaongozana mpaka upande wa chakula walipokuwepo wale wanakamati wenzake. Walikaa ndani, kwenye eneo kubwa kidogo. Waliunganishiwa meza mbili ili waweze kuonana. Tunda aliwasalimia bila kuwaangalia huku akijaribu kuvuta kiti alichoonyeshwa na mwenyeji wake.

Ana kwa Ana na Net tena!

“Tunda!” Tunda alishtuka kidogo baada yakusikia jina lake likitajwa pale mezani. Akanyanyua uso kutafuta aliyemwita na kukutana na Net. Tunda akatoa tabasamu kubwa sana la mshtuko. “Net! Habari za siku!?” Net alikuwa kwenye mshangao mkubwa sana, uliowafanya wanakamati wote wabaki wakiwakodolea wao macho. Tunda alikaa chini, na kumwangalia tena Net, pembeni ya Net, alikuwepo Gabriel. Tunda akashtuka sana, akaamua kutokuwaangalia tena. Akabaki akimtizama mwenyeji wake tu.

“Naona tumeshatambulishwa jina, tumeshajua unaitwa Tunda.” Yule mwenyeji akavunja ukimya. “Ndiyo. Ninaitwa Tunda, ndiye ninayehusika na mambo ya upambaji. Uliniambia mlishapitia kwenye website yangu. Si ndiyo?” Tunda akauliza huku akimtizama yule mwenyeji. “Ndiyo.” “Sio wote bwana.” Mwingine akakanusha. “Basi haina shida. Nimewaletea baadhi ya picha, ili muone baadhi ya kazi zangu kisha mchague.” Tunda akatoa zile picha alizokuwa amezipanga vizuri kwenye albamu.

          “Bei zako zikoje?” Mmoja wao akauliza wakati akiendelea kuangalia. “Inategemea na nini unataka ukumbini. Ukichagua moja ya picha hapo naweza kukutajia bei. Na pia kama hakuna muundo hata mmoja mtakao kuwa mmependa hapo, naweza kuwapambia kutokana na mtakavyo nyinyi. Mnaniambia nini mnataka, ukubwa wa ukumbi, meza na idadi ya wageni mnao tarajia, nitaandika na kwenda kuwapigia mahesabu kisha nitawajulisha. Mara nyingi najitahidi kwenda kutokana na bajeti ya mteja.” Tunda akajieleza vizuri sana na sauti yake tulivu bila pupa, nakubaki akiwasikiliza, ila macho yake yakiwa kwa mwenyeji wake tu.

Zile picha zilizunguka pale mezani watu wote wakiangalia kwa kurudia rudia. “Kazi yako nzuri dada Tunda.” Mmoja wa wanakamati akasifia. Tunda akatabasamu na kufanya azidi kuvutia kumtizama. “Asante.”

“Umeolewa?” Mwanakamati mwingine akauliza. “Acha hizo Tino, bwana! Wewe mtafute kwa wakati wako. Acha sisi tuongee mambo ya maana.” Wote walianza kucheka mpaka Tunda akatabasamu na kuinamia kwenye picha alizokuwa ameshika mkononi mwake. “Tatizo lako wewe Mgeekwa, unapenda kupania mambo sana. Si watu bado wanaangalia picha? Sasa kuna tatizo gani mimi nikaendelea  kuongea na Tunda?” “Utamchanganya bwana.” “Tunda mwenyewe haonekani kama ni mtu wakuchanganyikiwa hovyo. Halafu jibu lilikuwa fupi tu, ‘ndiyo au hapana’ ili nipate nguvu ya kuendelea kumtafuta baada ya hapa. Au hamtaki kikao kingine?” “Wewe si muoaji Tino. Acha fujo.” “Sasa ningemuoa nani wakati Tunda ndio amekuja leo? Eti jamani?” “Mgeekwa anakubania tu.”

“Mmeona eeh? Tuendelee Tunda. Sasa vipi?” Tino akaendelea kumchokoza Tunda. “Kwa kuwa wengi wenu hamkuwa mmeona kazi zangu, nashauri mtembelee website yangu ili muweze kuona kazi zangu nyingine ili mmfanye maamuzi sahihi. Kisha mnaweza kupiga simu ofisini ili kutoa maamuzi yenu na kujua gharama zinakuaje.” “Bwana Tunda yupo kikazi! Na mimi nimesoma Tunda. Nimeelewa kuwa hunitaki.” Kila mtu akacheka.

“Achana naye huyo Tunda. Tuendelee na kazi.” Mgeekwa ambaye alionekana ndio muongoza kikao, aliingilia.

“Jamani nyinyi mnamjua bibi harusi mwenyewe. Mimi naomba nikubaliane na Tunda. Nikamuonyeshe, achague. Kisha tutakuja kuongea na Tunda.” “Au kwa nini msitukutanishe naye, yeye mwenyewe huyo bibiharusi? Tuone kitu gani anataka. Na kama atataka ushauri pia tunaweza kumshauri.  Anaweza kufika ofisini kwetu, ninao wataalamu pale watamshauri vizuri au watamsikiliza anachotaka.” “Sisi tunakutaka wewe Tunda. Usitutupie kwa watu wengine.” Yule mwenyeji wake akamkatisha.

“Msiwe na wasiwasi kabisa. Hakuna kitakachoharibika. Naomba niwaache, tuwasiliane mtakapo kuwa tayari.” Tunda akasimama. Net hakuwa ameongea kitu chochote alibaki akimtizama tu Tunda. “Naomba nikusalimie pembeni kidogo, Net.” Tunda aliongea kwa sauti tulivu huku akimtizama Net. “Mimi hutaki kunisalimia pembeni kidogo?” “Acha Tino, nini lakini?” “Tatizo lako Mgeekwa, hutaki nioe kaka!” Tunda akacheka akiwa bado amesimama. “Tundaaa!” Tino akarudia. Net akavuta kiti na kuondoka pale. Tunda akamfuata nyuma. Net alikuwa akiongoza njia huku Tunda akimfuata nyuma.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mbona huonekani kama una furaha, Net? Mzima?” Tunda akauliza mara baada ya Net kusimama nje ya ile hoteli na kumgeukia Tunda. “Kila kitu kipo sawa?” Tunda akarudia kwa upole akionyesha kujali. “Kwa nini hukunitafuta tena Tunda?” “Mama alichukua simu kwa ghafla, Net! Sikuweza kuchukua namba zako za simu. Nilishindwa jinsi ya kukupata. Hata nilipokwenda nyumbani kwako kufuata baadhi ya vitu vyangu, Emma hakuwa anajua lini unarudi nchini na hakuwa akijua njia ya kuwasiliana na wewe. Babu anaendeleaje?” “Alifariki. Unasema mama alikupokonya simu!?” Tunda akatulia kidogo.

“Tunda?” “Kwani yeye amekwambia nini?” Tunda akauliza. “Kwa nini unauliza swali juu ya swali Tunda? Nani anamjibu mwenzake?” “Samahani Net. Hakunipokonya, bali alichukua.” “Ilikuaje?” “Net please!” Tunda akamsihi kwa upole. Akimtaka ayaache tu. “What?” “Naomba tusiongelee mambo ya nyuma.” “Kwa kuwa wewe ushapita huko?” “Hapana Net. Kwa nini tusiongelee mambo ya sasa?” “Ya sasa yapi?” Tunda akanyamaza.

“Kama unashindwa kunijibu basi naona nikuache tu.” “Sishindwi Net. Lakini sijui ni nini mama alichokwambia juu yangu?” “Kwa kuwa wewe huna haja yakujua alichoniambia, mimi ninataka kujua nini kilitokea. Maana tuliagana vizuri siku ile ya jumamosi, ukaniambia tutawasiliana kesho yake. Ndio nakuona leo! Nakuuliza kulikoni, naona unashidwa kunijibu.” Tunda akaona ajieleze tu. Net alikuwa amekasirika.

“Siku ile tulipoagana, mimi niliendelea kukaa pale ofisini nikimalizia oda ya Nchawa. Si unakumbuka nilikwambia alipiga simu akitaka tumpelekee mzigo wake wote kwa pamoja siku ya jumanne?” “Ndiyo.” Net akajibu. “Sasa kumbuka nilikuwa sina lori kubwa. Yote mawili yalikuwa yamepeleka mizigo mikoani. Wazo lilinijia kuazima kwa kina Masai, ili nihakikishe napeleka mzigo wote siku ya jumanne ili kuhakikisha simpotezi Nchawa. Maana alisema nikimfanikishia, atakuwa anatupa kazi kila week hata kama mara mbili kwa week itategemea na sisi wenyewe na uwezo wetu. Sasa ikabidi kupambana ili nisiharibu, nimfurahishe.” Tunda akaendelea.

“Niliongea na Masai mwenyewe akasema lori analo lakini hana dereva anayemuamini. Dereva wake ambaye anatumia hilo lori amepatwa na matatizo, hayupo kazini. Akawa amenipa namba za simu za watu kadhaa, akaniambia huwa anawatumia mara moja moja. Nilikaa pale mpaka usiku nikijaribu kutafuta dereva wakupeleka mzigo wa Nchawa Moshi, siku hiyo ya jumanne asubuhi. Nilitaka kufikia jumatatu niwe nina uhakika na kila kitu. Dereva na usafiri wenyewe. Nilikuja kukamilisha kila kitu usiku kama kwenye saa mbili.” Net alikuwa akisikiliza tu.

“Niliporudi nyumbani baada ya kukamilisha kila kitu, nikamkuta mama na Safia.” Tunda akatulia kidogo. “Nini kilitokea?”  Kama kawaida ya Net, akataka amalizie. “Mama alionekana amenikasirikia sana na zaidi hakupenda kabisa kitendo cha mimi kuwa nikiishi pale bila yeye kuwa na taarifa. Alilaumu ni kwa nini uliweza kuruhusu mtu mwenye tabia kama zangu kuishi mle ndani na Maya, na mambo mengine mengi ambayo siwezi kurudia, itakuwa ni kama najitusi tena mwenyewe.”

“Lakini aliniambia Safia ndiye atakuwa bosi wangu, anahitaji nimkabidhi kila kitu ikiwemo simu ile ya mkononi na usiku uleule nimpishe Safia kwenye chumba kile nilichokuwa nikilala pale nyumbani kwake. Na usiku uleule niondoe mizigo yangu pale. Nilimkabidhi kila kitu, tena nilimuomba kwa kuwa ilikuwa usiku, na nilikuwa na mizigo, aniruhusu kuondoka na gari yako kisha niirudishe kesho yake, lakini mama alikataa. Nilijaribu kumuuliza kulikuwa na shida gani kwa nini amekuwa vile! Lakini mama alikuwa mkali sana, Net. Alinitaka niondoke pale usiku uleule. Ikabidi niondoke na mizigo yangu mpaka barabarani ndipo nikapata taksii.”

“Siku ya jumatatu asubuhi niliwakuta walishafika ofisini, Safia alikuwa kwenye meza yangu. Nikaamua kwenda kumsalimia mama ofisini kwako.” Tunda akanyamaza akageukia pembeni. Net akamuona Tunda akianza kufuta machozi. Alilia sana Tunda. Net akamshika mkono akamvuta nyuma ya gari.

“Nini kilitokea Tunda?” Tunda alishindwa kuongea kwa muda. Akajaribu kutulia ndipo akaendelea huku akilia. “Mama Cote alitumia maisha yangu ya nyuma kunidhalilisha Net. Alinitukana mbele ya Safia na yule kijana. Akinitaka nirudi kwanza shule niache umalaya, nikipata vyeti ndio nirudi pale kazini. Akanilipa na kunitaka niondoke.”

“Kweli sijui ni baya gani niliwatendea! Nilijitahidi kufanya ile kazi kwa kadiri ya uwezo wangu, na nilikusudia kuacha yale maisha machafu Net. Niliacha umalaya. Niliumia sana kuona mama Cote anatumia maneno niliyoongea kanisani tena mbele ya wazee, Mchungaji akinisihi niseme tu, pale ni sehemu salama, na wewe ukasema nisiwe na wasiwasi, lakini baadaye tena baada ya kutubu, na Mungu kunisamehe, bado nakumbushwa tena kwa kutukanwa! Bila kosa! Niliumia sana Net. Sana.” Tunda akajifuta machozi.

“Historia yangu yakufukuzwa ikajirudia, Net. Alinifukuza mama yako usiku nikiwa na mizigo, na pale ofisini akinitukana. Lakini nimesamehe. Sikutaka kurudia kuzungumzia na wewe yaliyotokea kwa kuwa yananikumbusha mambo ambayo hayanijengi bali kunibomoa. Isingekuwa Mungu, nisingeweza kurudi tena kanisani Net. Nisingeamini watu wa kanisani, na nisingekuwa kanisani mpaka sasa.”

“Lakini Mungu ameniponya Net. Amenipa familia ya kanisani. Nzuri sana. Nina mama na baba wa Kiroho wanao nifuatilia vizuri sana. Tena wao ndio wamenisaidia kufikia hapa. Na wala sikurudi tena shule. Kwa elimu ileile ndogo niliyonayo ninaweza kuishi.” Net alibaki kama amemwagiwa maji. “Pole Tunda na samahani sana.” “Yameshakwisha Net. Mungu amenisaidi ninaishi vizuri na nina amani.” 

Simu ya Tunda ikaanza kuita. Akasogea pembeni kidogo na kuanza kuongea. Alisikiliza kwa muda, akiwa kimya “Naomba subiri kidogo.”  Net akamsikia Tunda akiongea kwenye simu, akimwambia anayezungumza naye asubiri, kisha akamgeukia tena Net. “Net! Naomba nikuage, Mungu akipenda tutaonana tena.”  Tunda alikuwa bado ameshikilia simu yake kama kuna mtu anayemsubiri upande wa pili. Net alibaki akimwangalia. “Bye!” Tunda akamuaga, kisha akaondoka pale akilifuata gari lake. “Samahani kuna mtu nilikuwa nikizungumza naye hapa. Ehe! Kwa hiyo umesema inawezekana?” Net akamsikia Tunda akiongea huku akiishia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku inayofuata, Tunda akiwa ukumbini anapamba, mida ya saa mbili asubuhi, mmoja wa wafanyakazi wake, Jazi, alimpigia simu kumwambia ametoka kuzungumza na simu ya wateja wake wa siku iliyopita, wakina Mgeekwa, wanamuomba wakutane tena jioni yake, walishafikia uamuzi. Jazi alikuwa ameandika kila kitu chini, muda na mahali. Tunda akamtaka huyo huyo Jazi ndio aende kumuwakilisha muda huo utakapofika. Siku za jumamosi usingeweza kumuweka Tunda kwenye kikao chochote. Anakuwa busy kupita kiasi.

Ilipofika jioni Jazi alitoka kwenda kumuwakilisha Tunda kule kwa wale wanakamati alipokuwepo Net na Gabriel. Jazi alitoka pale akiwa amejiandaa kwenda kukamilisha oda, lakini alipofika pale walimkataa kabisa. “Tunda yupo na majukumu mengine. Chochote mtakachoniambia mimi, kitamfikia na yeye.” “Hapana. Kamwambie Tunda aje yeye mwenyewe. Na sisi pia ni wateja. Tunataka huduma yake. Kwani ni bure? Na sisi tutamlipa.” “Siku za jumamosi inakuwa ngumu sana kumpata Tunda jamani! Naomba mniamini kuwa, mkiniona mimi, ndio mmemuona Tunda.” “Bwana wee! Sisi tunamtaka Tunda. Wewe nenda zako.” Wote wakamshambulia Jazi kwa maneno wakimtaka Tunda, mwishowe Jazi akaondoka.

Alimpigia simu Tunda akiwa analia kuwa amedhalilika sana. “Usichukie Jazi, ndio changamoto za kazi hizo.” “Wamenifukuza, kama..” “Kwanza ujue wengi wao pale ni walevi. Wala usiumie. Umenielewa Jazi? Nitawapigia simu baadaye kuzungumza nao. Wewe rudi nyumbani ukapumzike. Pole sana.” Siku ya jumamosi ilikuwa siku ambayo Tunda anakuwa na kazi mbili au tatu. Sasa jumamosi hiyo alikuwa akipamba kumbi tatu, tena zote kubwa. Tangia saa 9 usiku au alfajiri, Tunda alishafika kazini kwenye ukumbi wa kwanza.

Alichokuwa akifanya ili kumaliza kwa wakati, kila ukumbi alitanguliza vijana wake waanze kupamba kisha yeye alipita kumalizia. Hakuwa akipokea simu ya mtu yeyote isipokuwa wafanyakazi wake na mama Penny, basi. Ile simu ambayo namba alikuwa akiwapa wateja, alikuwa hata hagusi siku hizo za jumamosi. Kwanza hakuwa akitoa kwenye pochi mpaka akimaliza kazi, ndipo ataitoa tena kwa ajili ya kumpigia simu muhusika, afike hapo, amkabidhi huo ukumbi, basi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo alishinda kwenye kazi mpaka ilipofika usiku ndipo aliporudi nyumbani kwake. Siku hiyo hakuwa hata na hamu ya chakula. Aliingia kuoga akatoka na kujitupia kitandani kwake. Ni kweli alikuwa akitengeneza pesa, lakini alihitajika nidhamu ya hali ya juu kwenye kazi hiyo. Kwa kuwa alikuwa akichukua kazi nyingi, ilibidi kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha hakuna anapokosea, na hakuna anayemuudhi. Iwe wanaolipia pesa nyingi au wale wenye kutaka kupambiwa kwa kawaida tu, kote alihakikisha anaridhisha wateja wake. Na mara nyingi siku za jumamosi ndio alikuwa na kazi nyingi sana kuliko siku nyingine zote.

Akiwa anakaribia kupitiwa na usingizi, akasikia mlio wa sauti wa simu yake kuashiria ujumbe umeingia. Alijichukia kwa kutokuzima ile simu kabisa. Bila kutaka kuwasha taa, alinyoosha mkono kwenye meza ndogo pembeni ya kitanda chake, ili kuivuta simu yake na kuizima kabisa, ili apumzike.

Wakati anataka kuizima kabisa ile simu, akaonelea aone ule ujumbe ambao kwanza umeingia muda ule, ukawa umemtoa kwenye usingizi. Alitaka kusoma kesho yake lakini akaona amjue huyo msumbufu wake. “Anataka nini usiku huu jamani!” Tunda akajiuliza kwa hasira. Akasoma. ‘Najua una mambo mengi Tunda, lakini naomba utafute muda tuzungumze. Net.’ Tunda aliruka pale kitandani, akakaa. Akaamua kujibu. ‘Tunaweza kuongea wakati wowote.’ ‘Lakini leo hukupokea simu zangu kabisa, Tunda!’ ‘Samahani Net, sikujua kama ni wewe. Siku za jumamosi nakuwa na kazi nyingi sana. Kama simu siifahamu huwa sipokei. Sasa hivi ndio narudi nyumbani. Nimechoka kweli, hapa nipo kitandani.’ ‘Pole.’ ‘Asante.’ Tunda akajibu, kisha akatulia.

‘Lini sasa unaweza kuwa na nafasi?’ Net akatuma ujumbe mwingine. ‘Naweza kukupigia sasa hivi?’ Tunda akauliza. Mara akaona simu yake ikiita. “Net!” “Vipi?” “Safi tu. Nimeona ni heri tuongee tu kwa simu.” “Hutaki kuniona tena!?” “Hapana. Sio hivyo Net.” “Hivi unakumbuka uliniacha sehemu ya kuegesha magari?” Tunda akafunga macho na kuvuta kumbukumbu.

“Lakini nilikuaga Net.” “Unakumbuka mimi kukuaga?” “Hapana. Naomba unisamehe. Nimekuwa na mambo mengi kweli! Yananivuruga akili.” “Nini tena?” “Nahangaika kumtoa baba jela, anaumwa. Natamani atoke mapema ili akatibiwe.” “Umepata wakili mzuri?” Net akauliza kuonyesha kujali.

“Nafikiri hivyo. Sijui. Ndiyo yupo anahangaikia kufufa hiyo kesi. Ila baba amedhoofu sana, Net. Anatakiwa kutoka jela mapema ili awahi matibabu. Kesho nataka niende nikamuone tena.” “Pole sana. Tunaweza kwenda wote kumtizama?” “Twende wote jela!?” Tunda akauliza kwa mshangao.

“Si ndipo alipo?” Net akauliza kiustarabu tu. “Ndiyo. Bado yupo jela.” Akajibu kwa upole. “Basi tutaenda wote.” “Asante Net.” “Unaabudu kanisa gani?” Tunda akamuelekeza na kumwambia ni muda gani wanaanza ibada. “Basi nitakuja kanisani kwenu kukutembelea.” “Nitafurahi kukuona Net. Karibu.” “Asante. Basi ngoja nikuache upumzike, nitakuona kesho.” “Asante, usiku mwema.” “Na wewe pia.”  Waliagana, Tunda akabaki akijiuliza maswali mawili matatu, mwishowe akaonelea alale tu.

Jumapili. Net Kanisani kwa Kina Tunda.

Siku hiyo ya jumapili, alimkuta Net ameshafika kanisani akimsubiri nje ya gari yake. Tunda akaegesha gari yake pembeni ya alipokuwa amegesha Net gari yake. Kama kawaida yake hakujikosea. Alikuwa amependeza haswa. Alishuka akiwa ameshikilia pochi yake na bibilia yake mkononi. Akamsalimia Net huku akijaribu kuweka vitu vingine kama simu yake ya mkononi na funguo za gari ndani ya pochi yake.

“Karibu sana, hapa ndipo Mungu alinipa familia nyingine. Ni watu wazuri sana. Utamfurahia Mchungaji wetu na mkewe. Wamefanya hapa kanisani kukawa kimbilio la wengi. Wanahimiza sana vijana kufanya kazi kwa bidii. Mkewe ndiye mwenye kipaji cha kugundua vipaji vya watu na kuviendeleza. Yeye ndiye amenisukuma kwenye hii kazi ninayofanya, tena nikiwa na hofu nyingi kweli.” “Auntie Tunda!” Watoto wa Mchungaji walimkimbilia Tunda. Penny na mdogo wake Pendo.

“Dady ametufukuza ofisini kwake.” Tunda akacheka. “Huu ni muda wenu wa Sunday School. Muwahi msichelewe.” “Huyo ni mzungu?” Mmoja wao ambaye Tunda alimlaumu sana mama yake kuwa alimuharibu mwanae kwa vituko, Penny alimnong’oneza hilo swali Tunda lakini aliweza kusikika. “Na anasikia Kiswahili.” Tunda akamjibu, wote wakacheka.

“Umekamatwa leo na maswali yako yasiyoisha we Penny!” Mdogo wake alimwambia ndugu yake huku akimcheka. “Shikamoo. Naitwa Penny, kipenzi cha dady.” Penny akamwambia Net. Net alikuwa akicheka tu. “Muongo, mimi ndiye kipenzi cha dad and by the way, dady yetu ndiye bosi hapa.” Net akazidi kucheka.

“Nilikwambia hili kanisa lina vituko! Sasa bado hujakutana na wazazi wao. Ndio utachoka zaidi. Haya naomba muende Sunday school.” Tunda aliwashika vichwa na kuwageuza, kama kuwaelekezea upande lilipokuwepo darasa lao kwa kuwasukuma kidogo.

“Hata hatujamjua mgeni wakizungu sababu yako!” Walimsikia mdogo wake Penny akimlaumu Penny. “Ni mchumba wa auntie Tunda?” Pendo akamuuliza Penny, “Wewe! Akikusikia anko Juli, atakupiga makwenzi. Anko Juli ndio mchumba wa auntie Tunda.” “Muongo.” “Kweli.” “Muongo.” “Kweli tena. Nilimsikia mama akimwambia dady.” Waliwasikia wale watoto wakibishana huku wakielekea darasani kwao. Walijawa fujo na kelele kupita kiasi. Tunda alibaki akitingisha kichwa huku akicheka.

“Shalom!” Tunda na Net walishtuliwa na sauti iliyokuwa ikiwasalimia, maana akili zao zilikuwa zimezama kwenye mazungumzo ya wale watoto. Wote wakageuka. “Amina Juli. Shalom!” Tunda akajibu. Juli akamsogelea na kumkumbatia Tunda huku akimtizama kwa tabasamu. “Umependeza sana Tunda.” Tunda akacheka kidogo. “Usingenisifia ningeshangaa!” Wote wawili wakacheka.

“Ni kweli bwana. Au hutaki nikupe sifa zako?” “Hapana, nashukuru. Juli! Huyu anaitwa Net, Net huyu anaitwa Julius au Juli kama wengi tulivyozoea kumwita.” Walipeana mikono. “Net ndiye mtu aliyenitoa duniani nakunileta kanisani.” Tunda akaongeza huo utambulisho mfupi tu. “Tunashukuru bwana kwa kutuletea kondoo. Maana kuna vifaa vingine muhimu sana kanisani, ndio kina Tunda.” Juli aliongeza huku akicheka. Juli na Tunda walitaniana kidogo mbele ya Net, waliposikia nyimbo zimeanza kusikika kanisani, Tunda akamwambia Net waingie kanisani, ibada imeanza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda alikaa na Net mpaka mwisho wa ibada, ndipo walipotoka na kwenda kusalimiana na Mchungaji na mkewe ofisini. “Wote nilisha waambia juu ya Net. Nafikiri mnakumbuka.” Tunda akaongea kwa hakika akijua lazima Mchungaji na mkewe watakuwa wakimkumbuka tu Net. Wakabaki wametoa macho. “Jamani nyinyi! Net!? Pale kanisani alijitambulisha kama Nathaniel Cote, lakini kwa kifupi ni Net. Net yule niliyewaambia habari zake!” Tunda akashangaa wanawezaje kumsahau Net!

“Tunakumbuka sana. Lakini sikumbuki kama ulituambia kama ni mzungu!” Mama Penny akajibu na kumgeukia mumewe. “Au wewe baba Paroko unataarifa hizo?” “Hata kidogo.” Tunda na Net wakaanza kucheka.

“Unaposimulia jambo, usiwe unaondoa mambo ya muhimu.” “Sasa swala la uzungu wa Net ungeongeza nini kwenye ushuhuda wangu?” “Usitutanie kabisa wewe Tunda! Kuna uzito wake mkubwa sana. Wewe kutolewa jalalani na Mzungu na kuketishwa na wakubwa kama sisi, sio kitu kidogo!” “Mama Penny wewe! ” Tunda alibaki akimshangaa.

“Kabisa!” Kama kawaida ya mumewe kuunga mkono kila kitu anachoongea mkewe. Net alikuwa akicheka tu. “Kwanza ujue Net anasikia na kuongea Kiswahili fasaha kama mtu aliyezaliwa Tanzania. Yaani hata hapa anawasikia kila kitu.” Wakatulia kidogo. “Eti ni kweli?” Mama Penny akauliza huku akimwangalia Net ambaye yeye alikuwa akicheka muda wote. “Sasa unafikiri ile salamu ya pale kanisani alikariri?” Mama Penny akamtizama Net na mumewe. “Tunajua sana kama anajua kiswahili.” Mumewe akasaidia, wote wakacheka.

“Jamani nimefurahi kuona Tunda yupo na watu wanao mjali.” Ikabidi Net azungumze tu. “Sisi tumefurahi kukufahamu na kuja kututembelea Net. Hatujawahi kupata rafiki wa kizungu tangia tuanze hii huduma.” “Jamani Mama Penny wewe!” Tunda akazidi kushangaa. “Naongea moyo wangu. Kwa nini nisiseme ukweli?” “Mimi ndio kabisaaa, sijawahi kuwa na rafiki mzungu tokea nizaliwe.” Mchungaji akaongeza. Wote wakacheka.

“Net, tuondoke zetu.” Tunda akasimama. “Lazima twende naye nyumbani akale.” “Nina haraka mama Penny!” Tunda alitaka kukataa. “Haituhusu sisi. Ulimleta mwenyewe. Kama unaharaka ndio mtangulie nyumbani, sisi tutawakuta huko huko. Huwezi kumleta mgeni halafu ukaishia naye ofisini.” Mama Mchungaji akajibu.

“Atakuja nyumbani siku nyingine.” “Mbona hilo tunalifahamu? Na tutahakikisha lazima aje nyumbani siku nyingine. Leo haiwezi ikawa mwisho wake wakufika nyumbani kwetu” Tunda akatingisha kichwa, huku akiguna. Alijua jinsi mama Penny alivyo king’ang’anizi. “Twende Net mwaya.” “Ukajisikie nyumbani Net. Sisi tuko nyuma yenu tunakuja. Ngoja nikusanye vifaranga vyangu vyote. Tunakuja sasa hivi.” “Asante sana.” Net akashukuru wakatoka.

 

Tunda na Net kwenye gari.

Wote wakajikuta wakianza kucheka tena mara ya kutoka hapo ofisini. “Huwa wanakuwa serious hawa?” Net akauliza. “Heri Mchungaji kidogo huwa anajitahidi, lakini huyo mkewe!  Sijawahi kumuona. Lakini anaupendo sana. Hana roho ya wivu hata kidogo, anapenda kila mtu afanikiwe.” Waliongozana mpaka kwenye magari yao.

          “Unataka tuendeshe magari mawili kama tupo kwenye msafara bwana! Njoo upande kwenye gari yangu, tutakuja kuchukua gari yako baadaye.” Tunda akacheka, akaona ni wazo zuri. Akaingia kwenye gari ya Net. Alipokaa tu, Net akamvuta mkono wake wakushoto akaangalia vidole vyake. “Mbona Juli hajaweka pete bado!?” Tunda akatulia kidogo kama anayefikiria.

“Hatujafika huko.” Tunda akajibu baada yakumuona Net akimtizama. “Mmefikia wapi? Maana naona mpaka mnakumbatiana.” “Nisalamu tu, Net jamani!” “Salamu yenu nyinyi wawili tu!? Mnasalimiana kwa kukumbatiana?” Tunda akatulia tena kama anayefikiria kwa kuvuta kumbukumbu. “Eti Tunda?” Net akauliza tena na kuwasha gari kisha akaondoa gari pale kanisani.

“Watu wengi huwa wanasalimiana pale kanisani kwa kukumbatiana.” “Oooh! Basi inabidi nirudi tena. Maana leo sikubahatika kukumbatiwa kabisa, na wala sikubahatika kuona watu wengine walio kumbatiana. Hata Juli mwenyewe hakunikumbatia na mimi ila wewe tu wakati tulikuwa tumesimama wote.” Tunda akanyamaza.

“Kwa hiyo sasa hivi mpo kwenye hatua gani ya mahusiano?” “Hatujafika popote.” “Anatambulika mpaka kwa viongozi wako kama ni mchumba wako, bado hamjafika popote!?” “Alinigusia tu nia yake yakutaka kunioa.” Tunda akaongea tu hivyo na kunyamaza, Net akamgeukia kama kumwambia aendelee, anamsikiliza.

“Ndio na mimi nikamwambia mama Mchungaji, au tuseme mama Penny. Yeye ndio kama rafiki yangu au mshauri wangu, nafikiri watoto walimsikia wakati akimwambia mumewe. Lakini hamna mwendelezo wowote.” “Unamaanisha nini?” “Tuliishia hapo hapo tu, Net!” “Mbona sikuelewi Tunda? Mtu alikufuata kukueleza nia ya kutaka kukuoa. Halafu unaniambia mliishia hapo hapo! Inamaana mmeishia hapo hapo kama wachumba,  au kama mke na mume au?” “Net jamani! Nilishindwa kitu chakumjibu.” Net akamgeukia huku amekunja uso.

“Huyu kaka anamtaka Tunda asiyemfahamu hata kidogo. Nilijua anataka kujiingiza kwa mtu asiyemfahamu kabisa. Anamuona Tunda aliyesimama pale, lakini hamjui Tunda wa kweli na maisha niliyoishi nyuma. Najua wazi Mungu amenisamehe, lakini hapa duniani mambo yote niliyofanya bado yapo kwenye akili na miayo ya watu, Net.”

“Mama yangu mpaka leo sina mahusiano naye kwa kosa la kutembea na mumewe na wanawake wengine wengi ambao nimevunja ndoa zao au nimeathiri ndoa zao kwa namna moja au nyingine. Ndugu zangu wenyewe hawaniamini hata na marafiki zao wakiume! Hebu niambie Net, huyu Julius siku moja akitaka kuja kukutana na familia yangu nampeleka wapi?” Tunda akauliza kwa upole.

“Wewe ulikaa na ndugu zangu kwa muda mfupi sana, lakini waliweza kukwambia mabaya yangu yote. Japo mengine ni ya uongo, lakini yanasababishwa na chuki waliyonayo juu yangu kwa yale niliyo watendea. Naogopa hata kufikiria swala la mahusiano na mtu yeyote yule, kuhofia kuja kunilazimu kueleza historia yangu ya aibu au chafu kama vile! Sitaki nije nianze kupenda, halafu nikaumizwa kwa maisha niliyoishi zamani.”

“Ni ngumu kuja kuishi na mwanaume halafu akaja kukuamini kwa asilimia zote kama ambavyo angemuheshimu mwanamke aliyeanza naye mahusiano ya kimapenzi. Namaanisha labda msichana aliyemkuta bikra. Kwangu itakuwa ngumu Net. Nilishaharibu sana maisha yangu.”

“Nikichelewa kurudi nyumbani, atahisi nimetoka kwa mwanaume mwingine. Nikichelewa kupokea simu yake, au niongea na simu na mwanaume yeyote asiye mfahamu yeye, au hata nikiwa na mahusiano ya kawaida tu na mwanaume mwingine, huyo mume au mchumba wangu atahisi vinginevyo. Kuja kuwa na mahusiano kwa upande wangu ni kukubali kuingia kwenye maisha yatakayoninyima uhuru, furaha, na naona nitakuwa najiingiza kwenye matatizo tu.”

“Nimeamua niishi hivihivi, hata hivyo nimeshakinahiwa, halafu ninahofu yakuja kuingia kwenye ndoa nikashindwa kuzaa. Nitateseka sana.” “Kwa nini?” Net akauliza.

“Mama aliponitoa ile mimba, sijui walinitoaje! Sijui kama haikuathiri kizazi changu au la. Sitaki kuingia kwenye ndoa, nikiwa na wasiwasi huu.” “Kwani hukuwahi kushika mimba tena?” Net akauliza huku akimtizama Tunda. Tunda akainama.

“Ni Baba Tom tu, ndiye mwanaume pekee niliye lala naye bila kondom. Alikuwa hataki hata kusikia neno kondom. Ila baada yakutoka pale, au baada ya pale kila mwanaume niliyewahi kulala naye, hata Sadiki nilihakikisha natumia kondom kila wakati. Sikuwahi au sikurudi tena kutotumia kondom. Hata hivyo wengi nilihakikisha nawamaliza nguvu zakutoweza kuniingilia. Niliishia kuwa..” Tunda akanyamaza. Akageukia dirishani, nakuanza kufuta machozi.

“Nisikilize Tunda. Hayo nimaisha uliyoishi zamani. Ulishakiri, Mungu amekusamehe. Hutakiwi kuendelea kuumia kwa ajili ya hayo. Huko umeshatoka, na umeamua kutokurudi tena. Naomba utafute jinsi yakutumia hayo maisha kuwa msaada kwa wengine. Nilazima ubadilishe kutoka kuwa aibu na kuwa msaada kwa mtu mwingine. Ukikubali kuwa ni kwa ajili yako tu, na ukakubali ikutese, kweli itakuwa shida ulizopitia ni bure kabisa. Umenisikia?”  Tunda alikuwa akiendelea kulia.

Net akamvuta mkono wake aliokuwa akijifuta machozi akaubusu kiganjani. Ilikuwa ni mara ya kwanza Net kumbusu Tunda. Mwili mzima wa Tunda ulisisimka. Hakuwahi kujisikia vile tokea anazaliwa. Eti mtu kumbembeleza akiwa mkosaji! Kwanza huo mwili wengi waliugusa ili kujinufaisha nao. Wakike kwa wakiume. Sasa leo anapokea busu la faraja! Ilikuwa faraja ya pekee kwake. Tunda hakuamini kupata busu kutoka kwa Net anayemfahamu akiwa mchafu vile! Hata hivyo ni Net jamani!

“Huna haja yakulia kabisa Tunda. Lazima tugeuze yale maisha yako kuwa msaada kwa wengine.” “Nitafanyaje?” Tunda akauliza huku akifuta machozi, hata yeye hakuwa anaelewa alipitaje kule kote. Aliwezaje!? Hapo alipotulia ndipo picha ya kila kitu alichofanya nyuma ikaanza kumjia. Wakati mwingine aliweza kuhudumia wanaume hata watatu kwa siku moja!

Kinyaa, shida na mateso yote aliweza kuyapuuza akawa akifanya kama mchezo mwepesi sana. ‘Niliwezaje!?’ Ni swali alilokuwa akijiuliza kila wakati Tunda bila kupata jibu. Achilia mbali kujidhalilisha alikopitia bila kufanikiwa. Ilikuwa ni kama chombo cha thamani sana, kinachostahili kutumiwa kuwekea chakula hata cha wafalme, halafu chombo hicho hicho umpe mtoto mdogo, asiyejua thamani yake, achee nje kwenye matope.

“Kwa kuwa habari mbaya zinazagaa kwa haraka,” Net akaendelea. “lazima wewe mwenyewe uwe msemaji wa habari zako. Geuza kuwa msaada kwa mabinti na vijana. Huwezi kujua hata wazazi wengine wanaweza kupona.” “Kweli Net!?” “Kabisa. Acha watu wakufahamu kwa yale maisha ya zamani, na waone kazi kubwa Mungu aliyofanya ndani yako. Hakuna mwanadamu ambaye angeweza kukutoa ulipokuwa Tunda, isipokuwa Yesu mwenyewe. Ulikuwa umefungwa na nguvu za giza tokea mtoto unaishi na baba Tom. Ufahamu wako ulitekwa, ulikuwa ukitumikia falme nyingine kabisa. Kwa nini usitumie kile ulichofanyiwa na Mungu kufungua wengine?” Net akaendelea taratibu.

“Wapo wengi wanapitia ulipopita wewe, lakini wanakosa msaada. Ona jinsi ulivyofanikiwa kwenye maisha kwa kukubali kutumia kipaji Mungu alichokupa tena bila shule ya maana. Lazima kutumia maisha yako yaliyopita kwa ushindi. Yale shetani aliyokuwa amekusudia kuwa mabaya kwako, Mungu amekugeuzia kuwa mema. Sasa kwa nini unalia tena? Lazima ufurahie kama mshindi na si uliyeshindwa. Eti Tunda?” Machozi ya Tunda yalikauka gafla, akajawa tabasamu kubwa usoni mwake.

“Nilimiss hayo macho na hilo tabasamu!” Tunda akajifunika uso wake na kucheka kwa sauti. Net akaendelea kumfariji, huku akiendesha mpaka Tunda akafunguka kabisa. “Unajua Net, Mungu anakutumia sana katika maisha yangu? Kila wakati huwa unanitoa sehemu moja na kunipeleka sehemu ya juu! Isingekuwa wewe unajua sasa hivi nisingekuwa hapa?” “Ndio nakushangaa sasa unavyokuwa unanikimbia kila wakati!” Tunda akacheka.

“Sijakukimbia bwana!” “Unanipuuza sana Tunda! Hunichukulii maanani hata kidogo.” “Jamani Net!” “Kweli Tunda. Hebu niambie ni juhudi gani umefanya kunitafuta tokea ulipoondoka Arusha?” Tunda akabaki kimya.

“Inawezekana Arusha ni mbali sana. Lakini tulikutana majuzi pale hotelini, ukaniacha sehemu yakuegesha magari! Niambie ukweli Tunda, hivi ulikuwa hata na mpango wakuja kunitafuta tena?” Tunda alijisikia vibaya sana. “Nilijua tungeonana tu.” “Kwa njia gani, Tunda? Maana hata simu yangu hukuomba na kikao kilichofuata ulimtuma mfanyakazi wako aje kwenye kikao sio wewe mwenyewe. Mimi ndio nahangaika kulazimisha mahusiano ambayo hata sijui niite mahusiano au sijui niitaje.” “Ni mahusiano Net.” “Ni mahusiano gani haya Tunda!? Mimi ndiye wakukutafuta kila wakati, lakini mwenzangu ni kama nakusumbua tu.”

“Hunisumbui hata kidogo Net.” “Unauhakika Tunda?” Tunda akatulia kidogo. “Nikwambie ukweli Net?” “Niambie tu.” “Naomba nielewe kabisa. Nakosa ujasiri kwako.” “Kwangu tena!?” “Kabisa Net. Sijui nikujishtukia au vipi? Najiona nakuchosha na kukugharimu sana. Kwa hiyo wakati mwingine najiambia kukaa mbali na mimi ni kama unapumzika. Naona kama kazi yako uliyoifanya kwenye maisha yangu ni kama imetosha, sasa hivi nalazimika mimi mwenyewe kusimama, sio kukuchosha zaidi. Sijui umenielewa?” Walifika nyumbani kwa Mchungaji.

“Tutazungumza vizuri baadaye.”  Net aliongea hivyo wakati anaegesha gari. “Lakini naomba uniamini kuwa hunichoshi Net. Nisamehe pale unapoona ni kama nakupuuza. Sasa hivi nipo kwenye wakati wa hekaheka. Siwezi kusema mgumu, ila ni kama mtoto ambaye yupo kwenye kutambaa, lakini mazingira yanamtaka akimbie. Nina majukumu ambayo yote yananiangalia mimi na lazima niyatimize.”

“Siku kama ya leo ndio huwa napumzika. Ila siku nyingine, akili inabidi kufanya kazi kwa haraka ili kuweza kuchukua hatua na nisiharibu.” “Am so proud of you Tunda. Najivunia sana. Nilifurahi sana kukuona juzi ukiongea kwa kujiamini. Tena ukijinadi kipaji chako!” “Yote hiyo ni wewe Net.” Net akacheka.

“Na wewe Tunda. Ulikubali na kuchukua hatua. Nilijua jinsi wanaume walivyokuwa wakikusumbua tulivyokuwa pamoja kule Arusha. Wenye pesa na wafanyabiashara wakubwa. Lakini ulitulia. Umenifurahisha.” “Asante.” Tunda akacheka taratibu na kumwangalia Net. “Umenisamehe sasa?” Tunda akauliza kwa kujali akibembeleza. “Tutaongea zaidi baadaye. Twende ili tusichelewe kila mahali. Si uliniambia kule jela wana muda maalum?” “Ndiyo.” “Basi tusalimie hapa, halafu tuwahi.” Wakachuka garini.

Kwa Mara ya Kwanza Net Nyumbani, kwa Mchungaji.

Wakamkuta Mama Penny alishafika. “Mlipitia wapi!?” “Net alitaka tupitie dukani angalau tusije mikono mitupu.”  “Ndio faida yakuwa na mahusiano na wazungu! Maana wageni wengine wakija humu ndani, utasikia naomba nikanunuliwe Fanta, mimi sipendi Coca, au sijui Sprite! Lakini watu walio staarabika wanakuja na zawadi mkononi.” Mama Penny aliongea akimsuta Tunda. Net akacheka tu.

“Yaani mama Penny! Mwenzio nakuwa nimechoka, na Fanta pekee ndiyo inaniburudisha.” Tunda akajibu. “Sasa uwe unanunua kreti nzima unaliacha hapa ndani, sio kusumbua watu.” “Huwa naacha, ila wanao wanamaliza.” “Ni Penny huyo, anti.” Pendo akadakia. “Hata dady anapenda Fanta.” Penny naye akaongeza na kufanya watu wote wacheke.

“Watoto hawana siri hawa! Kwanza mpenzi wangu huwa hanywi soda nyingi kwa siku, tatu mwisho.” “Sasa kama anakunywa tatu, na wanao mbilimbili, hiyo kreti inakaa siku ngapi?” “Na dada naye anapenda Fanta.” Penny akaongeza tena. “Haya umesikia wanao?” Tunda akadakia.  “Naombeni muondoke nyinyi watoto!” Mama yao akawafukuza. Wote walikuwa wakicheka. 

“Karibu Net. Hapa ndipo nyumbani kwetu wote. Tukupokee mzigo, ila huna haja ya kuja hapa na vitu bwana. Uwepo wako ni zawadi tosha.” “Asante Mama Penny.” Ulikuwa ni wakati Net alioufurahia sana. Alikula na kucheka tokea anaingia mpaka wanatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Sijawahi kuona Mchungaji na Mama Mchungaji wa namna hiyo!” “Nilikwambia mimi. Yaani mimi nilikuja na uchungu moyoni, hata sijui viliishia wapi, na lini! Wana jinsi ya kukuonyesha maisha sio magumu ki vileee!!” “Si umemsikia hata huyo mama mwenyewe anavyosema?” “Basi ndio usemi wake kila wakati. Eti, ‘acha kuwa serious wewe, maisha sio magumu hivyo!’ au utamsikia, ‘Usituharibie hali ya hewa hapa kwa kuwaza kama unataka kuumba dunia wakati Mungu mwenyewe alishasema imekwisha, kazi yetu sisi tutawale.’ Wakati wote husema watu tunashindwa hutawala sababu ya ujinga tu.”

“Usimuone maneno mengi vile, anapesa sana yule mama. Karibu kila siku anayo kazi inayomuingizia sio chini ya milioni. Kama sio kupamba, basi anabiashara zake nyingine. Jina lake linafahamika sana hapa mjini, ndiye aliyenisaidia kuniuza kwa watu mpaka sasa na mimi nafahamika au napata kazi kwa jina langu. Mkarimu na hana tamaa. Ukifanikiwa ndiyo furaha yake.” Tunda na Net waliendelea kuongea wakiwa wanaelekea kumuona baba yake Tunda jela.

“Nimefurahi Tunda. Nimepata wakati mzuri sana. Nilihitaji mapumziko ya akili baada ya mawazo mengi.” “Unawaza nini tena Net!?” “Nitakwambia tukitoka kumuona baba, kama bado utakuwa na muda wakunisikiliza.” “Hata kama ni saa sita usiku, nitakusikiliza Net. Unajua ni wewe pekee ambaye sina haja yakujificha kwako? Sina sababu ya kujifanya Tunda huyu wasasa tu. Nakuwa huru, najua nipo na mtu anayenifahamu vizuri, na bado amenikubali.” Net akamtizama Tunda na kutabasamu.

“Nini sasa? Si kweli?” “Ni kweli Tunda. Na sio kukukubali tu, najipendekeza pia.” “Jamani Net! Hujipendekezi bwana.” “Unauhakika Tunda?” “Kweli Net. Nakuwa nakosa tu ujasiri. Nilikwambia. Lakini nafurahia tukiwa wote. Unaniheshimu japo unanijua kuliko yeyote yule hapa duniani.” Walifika gerezani, hapakuwa mbali na nyumbani kwa mchungaji. Ni eneo hilohilo la Tabata. “Twende kwanza tukamuone baba, kisha tutaongea.” Wakashuka.

Net akiwa na Tunda gerezani.

Waliingia ndani japo muda ulikuwa unakaribia kuisha wa kuwaona wafungwa, lakini baba yake Tunda alifurahi sana kumuona Tunda. Waliongea kidogo, Tunda akamuahidi, kufanya kila awezalo kumtoa humo. “Tunda aliniambia jinsi ulivyomsaidia kumtoa kwenye matatizo. Nakushukuru sana. Nilimuacha mwanangu hospitalini bila msaada, tena nikijua kila mtu hamtaki!” Baba yake akaendelea.

“Nilipo hukumiwa pale mahakamani nililia kama mtoto wa kike nikimfikiria mwanangu pale kitandani hospitalini. Nilimlaani Mungu kwa kukubali mimba ya huyu mtoto itungwe siku nilipolala na mama yake. Na pesa yenyewe niliyompa ilikuwa ndogo kweli, sikujua kama nitakuja kumuona tena Tunda!” Tunda alikuwa ameinama tu kama anayefikiria wakati baba yake akisimulia. Akili zilimrudisha mbali, akabaki akimsikiliza Net na baba yake huku akifikiria hili na kukumbuka lile.

“Nakushukuru sana.” “Hata mimi namshukuru Mungu kunikutanisha na Tunda. Nampenda sana Tunda.” Tunda akashtuka sana. Hakutegemea kusikia Net anasema vile, tena akiwa na baba yake! ‘Upendo huu ni wa namna gani!?’ Tunda akajiuliza kwa mshangao akanyanyua kichwa na kumgeukia Net palepale walipokuwa wamekaa upande mmoja wakimwangalia baba yake. “Nisije kujichanganya. Nisifurahie mengine. Net ni mzungu. Neno upendo ni kitu cha kawaida kutamka kwa wenzetu.” Akajirudi Tunda, akiogopa kufurahia zaidi.

          “Ni kweli ni upendo pekee, ndio uliokuwa ukihitajika kumpokea Tunda. Nakushukuru sana.” “Asante baba. Tunaweza kuomba pamoja?” Net akauliza kiuungwana. “Mimi sijui kuomba Net, wewe omba tu kama utataka.” Baba yake Tunda akajibu. Na hapo ndipo Net alipomfundisha yule mzee kuomba, na kumuhubiria. “Hata Tunda amekuwa akinihubiria, lakini…” Yule Mzee akasita.

“Haina haraka baba. Pata muda wakufikiria, kisha utaamua.” “Nina dini yangu nzuri tu. Sitaki kubadili dini.” “Kuokoka si kubadili dini baba. Nikupatanishwa na Mungu. Bibilia inasema watu wote tumekosa na kupungukiwa na utukufu wa Mungu. Kwa kutubu na kumkaribisha Yesu maishani mwako, nikukubali yale Mungu aliyokusudia kwa maisha yako. Kama ukiokoka, na ukaona dini uliyonayo inakusaidia kukusogeza karibu na Mungu, ujue upo katika njia sahihi.”

“Lengo la dini nikukupatanisha na Mungu, au iwe msaada kwa roho yako, basi.  Lakini kama itakuzuia kuwa na mahusiano na Mungu, basi itabidi ufikirie mara mbili, juu ya hiyo dini. Maana itakufaa nini kuwa na dini halafu ikakukosesha mbingu? Au itakusaidia nini kuiacha dini yako ukahamia kwenye kanisa, na pia ukakosa mbingu?” Net akaendelea.

“Lengo si kuhama kanisa moja kwenda jingine, lengo ni kuhama kutoka falme ya giza na kuhamia kwenye ufalme wa Mungu, na kukaa huko. Sio unahamia kwenye kanisa jingine, wenye jina fulani, ukajulikana na wewe upo kwenye kanisa hilo kumbe maisha yako ni chukizo mbele za Mungu. Ukibaki wewe peke yako na Mungu, hamna mahusiano yeyote, huo sio mpango wa Mungu.”

“Mungu anataka mahusiano na mtu mmoja mmoja si kanisa, wala dini. Ukifa leo mzee, hutaulizwa dini yako. Mungu atataka mahesabu ya jinsi ulivyotumia maisha yako hapa duniani.” “Maisha yenyewe yameisha haya kijana wangu. Nishatupwa huku.” “Nilikwambia usikate tamaa baba. Nahangaika kukutoa.” Tunda akaingilia.

“Hata hivyo, hata hapa ulipo pia utakuja kuulizwa na Mungu ulifanya nini?” “Ananiuliza nini huyo Mungu wakati yeye ndiye amenileta hapa, tena bila kosa!?” “Ewaa! Umezungumza sahihi kabisa. Kuwa Mungu alikuleta hapa kwa kusudi. Basi ujue lipo kusudi. Kwa nini iwe wewe na sio mwingine? Inawezekana kuna kazi anakupa humu gerezani uifanye au umeletwa humu kwa ajili yako mwenyewe. Unasema unayo dini. Huwa unasoma bibilia?” “Hapana, lakini nafahamu vihabari vyake.” Akajibu baba yake Tunda akiwa kama anavuta kumbukumbu.

“Unakumbuka historia ya Yusuph?” Yule mzee akatulia. “Kwa utizamaji huo, naamini unaijua habari nzima. Unakumbuka mwisho wake? Unakumbuka jinsi alivyotoka gerezani kitu Mungu alimfanyia?” “Si ndiye alikuja kusaidia ndugu zake?” Net akatabasamu kwa kuridhika.

“Si ndugu zake tu, watu wengi walipata msaada kupitia kukaa kwa Yusuph gerezani. Kama angelia na kubaki kulalamika, inamaana kuonewa kwake kule gerezani ingekuwa bure kabisa. Tunda amekupa ushuhuda wake?” “Upi tena?” Net akamtizama Tunda kama anayemuomba ruhusa, yakusema. Kwa vile Tunda anavyomfahamu Net, akajua hawezi kumdhalilisha kwa baba yake. Akamruhusu asimulie chochote na yeye akiwa na hamu yakusikia jinsi Net anavyoanza kutumia maisha yake kuwa msaada kwa wengine.

“Nilimwajiri Tunda kwenye kampuni ya mama yangu. Nikasafiri nikamwacha Tunda pale ofisini. Huku nyuma mama yangu alimfukuza Tunda vibaya sana. Aliondoka Arusha akiwa hajui chakufanya, akilia njiani akimlaumu Mungu. Lakini Mungu alimfundisha kwa mfano wa kupitia watoto, huku akimuonya kulia hakutamsaidia, mpaka atakapoangalia mazingira yanayomzunguka, akasimama na kuchukua hatua.”

 

“Tunda alitii, ndio maana yupo leo kama alivyo. Kama Tunda angeendelea kulalamika mpaka leo asingekuwa hapo. Na yale ambayo shetani ameyakusudia kuwa mabaya kwake, yangeendelea kumkandamiza na kumwangamiza kabisa.”

“Usikubali maisha yako yakawa hayana maana. Kila kinachotokea katika maisha yako baba yangu, kitumie kutengeneza hesabu ya kumpa Mungu siku ukisimama mbele zake. Maana ni kweli wote atatudai tu siku moja. Lakini uzuri, kila utakapochukua hatua, yeye anakuwa na wewe, anakuinua, atakutia nguvu na kukubariki.” Tunda alikuwa akimwangalia Net bila kummaliza. Kijana mzuri wakuvutia kwenye kila jicho la mtu anayemtizama, mpaka watoto! Aliyesoma vizuri, anayejua maisha vizuri, na pesa nzuri yakueleweka na bado anasimama na Mungu wake!

“Kwa mfano mwingine tu. Najua unajua maisha ya Tunda kwa sehemu. Tena ni maisha yasiyofaa kutamkika mbele za watu. Lakini tutahakikisha, maisha hayo hayo aliyoishi Tunda, yanasikika, tena vizuri, mpaka watu wakombolewe. Tutafundisha vijana kwa wazee, wakina baba na mama, tutamfikia kila mtu kwa maisha aliyoishi Tunda mpaka watu wapate msaada. Nje na ndani ya nchi. Wazi wazi bila kificho mpaka shetani ataogopa kushika ndoa za watu, maisha ya vijana, watoto wa watu, kila baya lililotendeka kwa Tunda, tena sirini, tutatumia mwangani kufikia jamii nzima, mwenye sikio atasikia na kubadilika.” Tunda hakuwa akiamini. “Inamaana na yeye anajiweka!” Bado Tunda hakuwa ameelewa.

Ilimgusa sana baba yake Tunda. Hata yeye hakuwahi kuona mtu aliyempokea Tunda kwa kiasi hicho. “Asante sana kijana wangu. Asante baba. Na mimi Mungu akinipa uzima, na akanitoa humu ndani, nitaungana na nyinyi.” Net akacheka. “Si umeona Tunda? Tunazidi kuwa wengi? Sasa wewe Mzee tunaomba uanzie humo ndani. Kwa kuwa mimi na Tunda hatuwezi kufikia wafungwa wenzako, wewe ndio uwe nao.”

“Naanzaje wakati hata kuomba siwezi!?” “Tutakuwa na wewe kwa maombi. Na wewe kazana kusoma bibilia ili uwe unaongea habari unazozifahamu. Tutakuombea ili ujazwe na nguvu za Mungu, halafu mruhusu Mungu akutumie kwa jinsi apendavyo na alivyokusudia. Kama alikuleta huku, lazima ujue lipo kusudi, na yeye atakusaidia kufikia lengo.” Yule mzee alifurahi sana. Net alimuongoza sala ya toba, akamuombea na kumuachia bibilia yake.

 

Baada yakutoka gerezani kumuona baba yake Tunda, Tunda & Net.

Tunda hakuwa akiamini. Alishindwa hata kuongea kwa muda. Net aliongea mambo kadhaa, yaliyomgusa na kumuogopesha Tunda. Hakuwa akiamini na aliogopa asije akafurahia kama alivyofurahia kwa Waziri Mbawala, ikawa tofauti. Ikaja kuwa ni Net aliongea yale yote sababu yakufikia roho ya baba yake. “Net anapenda watu watubu na wamrudie Mungu. Ingekuwa kunipenda mimi, angeniambia mwenyewe.” Tunda akaona ajitulize.

Net akaendelea kuendesha na yeye kimya, wakirudi kanisani kufuata gari ya Tunda. Alikaa kimya, baadaye ndipo akaweza kushukuru. “Nashukuru sana kwa kumsadia baba yangu. Umemuona jinsi alivyobadilika? Hata uso wake umechangamka. Asante sana. Mimi nimekuwa nikimuhubiria kwa muda mrefu sana bila Mafanikio.” “Ndio maana bibilia inasema katika kitabu cha {muhubiri 4:9 Two people are better off than one, for they can help each other succeed.} Au kwa Tafsiri ya Kiswahili ni {Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja, maana wapata ijara njema katika kazi au unaweza sema wanasaidiana kufanikiwa katika kazi}. Si umeona jinsi mimi na wewe tunavyoweza kufanya jambo likafanikiwa?”

“Mbona mimi pale sikusema kitu?” “Si kweli. Ulishapanda mbegu kwenye moyo wake, ukawa ukimwagilizia mimi nilienda kumalizia tu kuvuna.” Tunda akatabasamu kama anayefikiria. Wakawa wameshafika kanisani.

“Karibu nyumbani kwangu.” “Nilivyokuwa nasubiri kwa hamu huo ukaribisho!” “Bwana Net! Kwangu usisubiri kukaribishwa.” “Lazima nisubiri, na hivi kuna kina Julius tena!” Tunda akacheka na kushuka kwenye gari. “Unifuate nyuma, ndio itakuwa rahisi kufika nyumbani.” Tunda akafunga mlango na kuingia kwenye gari yake, kisha akaondoa gari yake, Net akawa akimfuata nyuma.

 

 

Net apasua jipu kwa Tunda.

Bado Tunda alikuwa akiishi pale pale maeneo ya Kimara, karibu sana na Ubungo. Alimkaribisha Net ndani, wakakaa kwenye makochi. “Hapa kwangu hakuna soda, nina maji tu. Ila naweza kwenda kukununulia kama utapenda. Mimi sio mpenzi sana wa Soda. Labda niwe nimechoka sana na kazi, ndio nitakunywa soda. Lakini sio hapa kwangu. Najitahidi zisiwepo.” “Hapana. Mimi nipo sawa tu. Bado nimeshiba.” Tunda akaweka vitu vyake ndani, akarudi kukaa hapo hapo kwenye kochi kubwa alilokuwa amekaa Net.

“Hongera. Naona nyumba imekamilika.” “Asante Net. Ndio moja ya vitu vilivyokuwa vikiniliza mwenzio! Sina ndugu wala ukoo wakusema nakwenda kutembea. Sasa hata nishindwe kuwa na kwangu! Ilikuwa ikiniuma sana. Nilianza kutafuta pakuishi hata kabla ya gari. Nilijiambia lazima nipate kwanza kwangu. Angalau nipate kimbilio.” “Hongera sana Tunda. Hakika umenifurahisha.” “Asante Net. Napambana kweli!” “Na juhudi zako zinakulipa. Nimepitia kwenye website yako, upo vizuri sana.” Hilo lilimfurahisha sana Tunda, kujua Net alimfuatilia zaidi.

“Nikuulize kitu Net? Nahofia nisiwe nimekuelewa vibaya.” “Karibu.” Net akajiweka sawa na kumgeukia. “Ulisema ‘utakuwa’ na mimi kunisaidia kutumia maisha yangu kufikia jamii?” Net akacheka pale Tunda alipoweka msisitizo kwenye ‘utakuwa’.

“Unajua umenipa hamasa sana? Ni kama umenitoa kwenye kona na kunivuta mwangani! Sasa hivi sioni haya tena. Lakini sijui ndio ninafanyaje! Umesema utanisaidia?” “Sio kukusaidia Tunda. Tutakuwa wote.” Tunda akawa bado kama hajampata vizuri. Net akaendelea.

“Nahisi ndio kazi Mungu anataka niifanye, labda mpaka kufa kwangu. Nimejaribu kukwepa, nikimpa Mungu sababu za msingi ili niweze kukwepa, lakini Mungu ananirudisha tu. Hata nifanye nini, bado najikuta nimerudi hapa hapa.” Hapo ndio akawa amempoteza kabisa Tunda. Akapandisha miguu yake kwenye kochi akaikunja vizuri nakumgeukia Net.

“Sikuelewi Net.” “Wewe kwa nini hushangai kila unavyozidi kunikwepa, ndivyo tunavyozidi kukutana?” “Net Jamani! Mimi mbona sikukwepi?” Net akacheka.

“Siku ya kwanza nafika nyumbani kwa shangazi yako, unakumbuka ulinifungulia mlango?” Tunda akatingisha kichwa kukubali. “Huwezi amini, naweza kukwambia mpaka aina ya gauni ulilokuwa umevaa siku ile, jinsi ile picha ilivyo niganda mawazoni. Hayo macho yako ya kusinzia, siku ile ndio yalikuwa yamezubaa yakinitizama.” Tunda alicheka na kufunika uso wake.

“Nikaanza kujifariji ili niepukane na mawazo yako. Nikasema kule kupigwa na butwaa na kunishangaa ni kitu ambacho nishazoea kwa watu wengi hasa wadada. Huwa wananiangalia kwa namna yao, ambayo huwa hainisumbui hata kidogo, lakini wewe ikawa tofauti.” “Mimi nilikuwa nakushangaa ulivyo mzuri zaidi ya nilivyosikia sifa zako! Mzungu unayeongea kiswahili chenye heshima.” Net akacheka.

“Sasa nikaanza kupuuza. Lakini bado nikawa nasumbuka. Ndio maana nikawa nahangaika kuja pale nikuone ili nijue ulichonacho wewe cha tofauti na kinadada wengine ni kipi! Nikawa nakuja mchana na usiku, ili nikuone, lakini sikufanikiwa. Nikawa namuomba Mungu angalau uje basi hata kufungua mlango tena, lakini wapi.”

“Baadaye nikajiambia niachane na wewe, usinisumbue. Tena hapo ndipo nilipokuwa nikipata na habari zako mbaya kabisa. Nikawa nikijiambia nina sababu zote za kuwa mbali na wewe. Lakini nikawa najikuta nataka kukuona tu. Mwishowe nikajiambia siwezi kujitesa kwa namna hii ni afadhali nitafute hata sababu nikae na wewe, ili hata nitafute sababu moja utakayonikera, nikuchukie, niondoke zangu nirudi shuleni kwa amani niwe nimekutoa mawazoni.” Tunda alikuwa haamini.

“Unakumbuka niliwakaribisha kwenye maombi nyumbani? Hukufanikiwa kuja, na nia ya kuwakaribisha nyinyi wote mpaka Nyangeta ilikuwa nikupata muda na wewe, nyumbani kwetu. Maana pale kwa shangazi yako ilishindikana kabisa kwa kuwa kila nilipokuwa nikijaribu kukusogelea ndivyo Sera na mdogo wake walivyozidi kunifuata, na kuishia kukutukana mbele yangu kitu kilichokuwa kikiniumiza sana.”

          “Uliposhindwa kuja nyumbani siku ile, na mimi nikaona muda wangu wakurudi chuoni umefika, lazima niondoke, na mimi ni mtu ambaye nikianza jambo lazima nimalize, ndipo nikajitosa kumuomba shangazi yako nirudi kesho yake nije kuongea na wewe kabla sijaondoka. Kumbe ndio naharibu zaidi.”

“Nilirudi Canada chuoni, lakini sikuwa na furaha, nikafikiria kitu chakufanya, nikaamua kutafuta msichana wa kanisani ili tuwe na mahusiano kuepuka msongamano wa mawazo. Nilipata binti mzuri tu wa kanisa ambalo nilikuwa nikiabudu na bibi na babu. Wazazi wake walikuwa wakifahamiana na kina babu. Kwa kipindi hicho wakati mimi nipo chuoni na yeye pia alikuwepo chuoni, lakini ndio alikuwa akianza, mambo yalienda vizuri sana.”

“Hapakuwa na shaka kuwa siye mwanamke Mungu aliyenipa. Tulielewana kwa mambo mengi tu, mengine yalikuwa madogo madogo yakurekebishana kama wanadamu au tuseme yakuchukuliana.”

“Siku moja nikiwa na yule dada nikajikuta nikijiambia afadhali nimeweza kuachana na mawazo ya Tunda. Hapo ndipo ikawa ni kama nimerudisha kumbukumbu zote. Na ndio ilikuwa nakaribia kumaliza chuo, na kwa muda wote huo hata sikuwa nimekufikiria, tulikuwa na amani na furaha na Chloe. Nilijuta sana kuleta zile kumbukumbu zilizokuwa zikinitesa bila sababu. Sikuwa nakufahamu, halafu nilikuwa na sifa mbaya tu za kwako. Nikawa nikimwambia Mungu na kumkumbusha mabaya yako niliyokuwa nimesikia.” Tunda akainama nakujifuta machozi.

“Shule yangu ilipoisha, mama akaniomba nirudi nimsaidie kazi zake kwa muda. Kama nitavutiwa kuishi naye sawa, nikitaka kurudi kuishi Canada pia ni sawa. Nikakumbuka wosia aliokuwa ameniachia baba, juu ya mkewe. Baba alimpenda sana mama. Wakati wote alikuwa akiniambia hata kama akiondoka kesho, I should watch over Maya na mama, yaani nimtunze mkewe na Maya. Ukumbuke aliniacha bado nikiwa mdogo tu, lakini sikuwahi kusahau hilo. Alinilea kuwa mwanaume wa familia tokea mtoto na babu hivyo hivyo. Japokuwa mambo yangu yalikuwa yakienda vizuri kule, ilinibidi nirudi Tanzania kumsaidia kazi mama.”

“Nilimuomba Chloe aihirishe angalau mwaka mmoja ili tuje naye huku, nikishaweka sawa mambo ya mama, tungerudi. Lakini Chloe alikataa. Nikamwambia hata kama itatulazimu kufunga ndoa kwanza, naweza kumuoa kisha tukaja naye Tanzania, na babu alimwambia endapo ataacha chuo kwa ajili yangu, akapoteza udhamini, babu alimuahidi angemsomesha kwa gharama zozote zile mpaka amalize. Lakini alisema, anaweza kunisubiri kwa huo muda wa mwaka mmoja, lakini hakuwahi kufikiria kuishi maisha mengine nje ya nchini kwao na amejiwekea malengo ya kumaliza shule ndani ya huo muda, hawezi kusogeza. Nikamkubalia, nikaja huku.”

“Baada ya mwaka, nikarudi na kumwambia inabidi niongeze muda, maana mama alianza kupata tenda za ujenzi wa barabara zilizokuwa zikimuingiza pesa nyingi sana lakini zilihitaji mtu kama mimi kuwepo na kusimamia. Nikamuomba tuondoke naye, bado akakataa. Akasema atanisubiri tu. Nikaamua kumvalisha kabisa pete ya uchumba ili asije kubadili mawazo. Nikarudi huku nikawa nikifanya kazi kwa bidii sana ili nimwache mama kwenye mazingira mazuri, na wafanyakazi wazuri ili nirudi kwenye maisha yangu. Safari za Canada zikawa nyingi kumfuata Chloe kwa kuwa alianza kulalamika anachoshwa na mahusiano ya mbali.” Net akatabasamu.

“Mambo yalianza kunichanganya pale nilipokuona tena. Katikati ya kazi nyingi, na mahusiano ya lawama, kati yangu na Chloe, kwa nini sipigi simu, kwa nini siendi kumuona, na mambo kama hayo. Unakumbuka mazingira tuliyokutana tena? Ulikuwa na mwanaume na wazi alionekana ni mume wa mtu. Niliumia mpaka nilijichukia. Nilijaribu kujiliwaza kwa kukuunganishia na maneno ya kina Sera, na kusema sina haja yakuumiza akili zangu, kwa msichana ambaye hukuwa na maadili, mimi ni mchumba wa mtu. Unajua tena, ili kujipa aghueni moyoni. Lakini nilishindwa Tunda. Nilikuwa nikiumia sana. Na Mungu naye alikuwa akinikutanisha na wewe kwenye mazingira yaliyokuwa yakizidi kunitesa sana.”

“Nilikuwa nikiumia nakujiuliza chakufanya, sikuwa najua pakukupata wala sikujua chakufanya. Ukweli niliteseka Tunda. Kila nilipokuwa najaribu kukupuuza, ndivyo nilivyozidi kukufumania. Hasira juu ya kila mwanaume niliyekukuta naye ilinifanyanya nichukie hata kazi ya mama. Kwa kuwa wanaume wote niliokuwa nikikukuta nao, ni watu muhimu sana kwenye biashara za mama.”

“Nilishindwa kabisa kuendelea na ile kazi, nilijawa hasira, nikashindwa kuwa mvumilivu kwenye kila kitu. Mama alidhani nimechoka kuwepo hapa Tanzania, akanishauri nirudi tu kwa bibi na babu, lakini nikajikuta siwezi tena kuondoka kukuacha kwenye mikono ya wanaume wanaotaka kukuchezea.” Net alicheka kidogo kama anayefikiria.

“Huwezi kuamini kutoka kwenye kukuchukia sana kwa kunisababishia maumivu ya uchafu unaofanya, nikageuza hisia nikaanza kuona uthamani ulio nao. Na kuzidi kuchukia kila mwanaume anayekuchezea. Nilikuwa nikijiambia wanakuchezea kwa kuwa hawajui thamani yako. Unakumbuka yule Mzee tulikutana wote Mwanza pale baa akiwa amelewa, akikuelezea jinsi ulivyo mzuri, na kueleza mambo kwa undani kabisa?” Tunda alishinda hata kumtizama Net, akabaki ameinama.

Net akaendelea. “Ukweli nilikuwa nikiteseka sana. Mwishowe nikaamua kujisalimisha kwa Mungu. Nilikuwa sijui chakufanya Tunda. Kila ninapoenda nakutana na wewe ukiwa na wanaume tofauti tofauti, huku Chloe naye ananitaka nirudi tufunge ndoa, huku najiambia siwezi kukuacha. Nikamwambia Mungu akinisaidia nikakupata, ukakubali kubadilika, nitaondoka haraka sana kurudi kwa mchumba wangu.”

“Siku iliyoniuma zaidi ni pale nilipokukuta na Gabriel. Niliumia sana. Gabriel alikuwa rafiki yangu tokea Canada. Baba yake alikuja kusoma kule, akawa chuo kimoja na mama, kwa hiyo Gab alikuja Canada akiwa mtoto sana, nilizaliwa yeye akiwa na miaka kama mitatu hivi. Tuliishi nao Canada, wao wakarudi huku nchini, Gabriel akiwa na miaka 18. Na ndio watanzania pekee tuliokuwa nao karibu kule. Hatukuacha kuwasiliana na Gab mpaka sasa. Na hata anapokuwa akija Canada, yeye na mkewe au wazazi wake, wanafikia nyumbani kwetu. Kwa hiyo ni kama ndugu.”

“Kuja kujua ulikuwa na mahusiano naye, nikaamua kuondoka kabisa nchini. Lakini Gab aliniomba sana radhi, nikamwambia akuache kabisa na asirudie kukutafuta tena. Maana alikuwa yupo tayari kumuacha mkewe kwa ajili yako. Nilimwambia endapo atamuacha mkewe, kwa ajili yako ndio itakuwa hata mwisho wangu na yeye pamoja na familia yake yote. Yaani mpaka wazazi. Ndio Gab akakubali kukuacha kabisa. Na kuniahidi hatakutafuta tena.”

“Lakini aliniudhi sana siku ile ulipomfuata hotelini unamlilia shida halafu anakwambia atakupiga! Iliniuma toka moyoni. Unakumbuka nilikukuta umejificha kwenye kona ukilia?” Tunda alitingisha kichwa kukubali akiwa anafuta machozi.

“Pale nilikuwa nimeshazunguka sana. Na gari na kwa miguu huku nikikimbia kukutafuta. Nilijua ndio wakati pekee Mungu alionipa kukupata. Kwa upande mwingine nilifurahi kuona umefika mwisho, watu wote wamekukimbia. Nikajiambia nakaribia kumaliza kazi yangu. Nikupatanishe na Mungu, kisha niondoke niende kwa mchumba wangu.”

“Kule kuishi na wewe Arusha ikawa msaada kwangu mimi mwenyewe. Hukuwa umefikia hata maamuzi ya kubadili maisha, lakini nilikuwa nikifurahia sana tukiwa pamoja. Nikaona jinsi ile ofisi inavyokuwa, nikajiambia wewe ni mtu utakayenifaa kwenye mambo mengi. Kwamba ukikubali kumpa Yesu maisha, nitakuwa nimeua ndege wawili kwa jiwe moja. Nitakuwa nimemalizana na wewe kwa amani, na ofisi nitaiacha kwenye mikono salama. Sasa unakumbuka siku tumeenda kwa mama akakwambia nitasafiri?” Tunda akatingisha kichwa kukubali.

“Alikuwa akijua muda wangu wakuondoka moja kwa moja kwenda kwa mchumba wangu umeshakaribia. Maana nilishakuwa nimekupa muda, nikasema ninakuachia muda fulani, uje ufikie maamuzi ya kubadilika bila mimi kukulazimisha. Nikajiambia muda huo ukifika hujafikia maamuzi, nitaongea na wewe, ukubali au ukatae, nikajiambia nitaondoka. Ndio nikawa nimemwambia mama kuwa ikifika mwezi wa kumi na moja nitaondoka moja kwa moja. Kumbe ule muda niliokuwa nimekupa wewe kukuangalia, ndio kipindi hicho na mimi nilianza kukuzoea. Huwezi amini jinsi ilivyokuwa ngumu kukuacha usiku. Nilikuwa nikitamani niwe na wewe wakati wote.” Tunda akamtizama huku amekunja uso, haamini.

“Siku zikazidi kwenda, wewe ukaokoka, lakini nikawa nashindwa kabisa kuondoka. Chloe naye akawa amenipa muda, kuwa ikifika mwezi wa kumi na moja sijarudi kule, hataweza kuendelea kunisubiri tena. Nilikuwa tayari kwa hilo. Kila mama alipokuwa akiniuliza naondoka lini, sikuwa na jibu tena.”

“Ndipo babu akaugua sana, ikabidi niende tu lakini hapo nilishakuwa nimeahirisha sana. Kila Nana alipokuwa akinipigia simu akiniambia hali ya Papa, nilikuwa nikimwambia nitakwenda, lakini nashindwa kukuacha. Huo mchezo ukaendelea, ndipo nikaambiwa majibu ya hospitalini yameonyesha Papa hawezi kupona. Nana akaniambia Papa anataka kuzungumza na mimi. Lazima niende haraka.”

“Ndio nikaondoka ule mwezi wa 11 mwanzoni. Kwa hiyo ikawa nimefika kabla ya kipindi alichokuwa amenipa Chloe kuisha. Tukaanzisha mahusiano kwa uhakika, huku nikimuahidi kutokuondoka tena Canada. Hapo nikajihesabia nimemaliza kazi yangu. Umeokoka, na ofisi ipo kwenye mikono salama.”

“Ila sasa mahusiano yakawa mazito sana kwangu, kwani Chloe hakuwa Tunda. Sikuwa nikiona maisha yangu na yule binti hata kidogo. Babu alinishauri labda nimchukue nimpeleke sehemu mbali mbali ili kupata naye muda, labda zile hisia za mwanzoni zingerudi. Aliniambia ni kwa kuwa tuliishi mbali mbali kwa muda mrefu sana. Nikamuacha babu akiwa bado anaumwa nikaanza kuzunguka na Chloe.”

“Hata Papa alijua angekufa, kwa hiyo alitaka kuniona nimeoa kabla hajafariki. Madaktari walitupa muda uliobaki wa papa au babu uliobaki kuishi. Nikakusudia babu awepo kwenye harusi yangu, angalau anione tu nikioa kwa kuwa ni kitu alichokuwa akikitamani kuondoka akiwa ameniacha nimeanzisha familia yangu. Nilizunguka na yule dada, lakini hakuwahi kuwa Tunda. Alikuwa na sifa zote za kuwa mke wa mtu, lakini sio mke wa Net.”

“Nakumbuka tulitoka safari tulitua uwanja wa ndege na Chloe nikaenda moja kwa moja hospitalini kwa babu. Nilimkuta na bibi yuko pale, nikajikuta machozi yakinitoka, nikimuhurumia babu yangu, kuwa yale aliyotamani nimeshindwa kumpa.”

“Nakumbuka babu alinitazama kwa huruma, nikajikuta namwambia, ‘She is not Tunda.’ Alitabasamu na kuniambia kwa kifupi tu, ‘then go and tell her, NOW’. Nikachukua ushauri wa babu pale pale, sikutaka hata kusubiri. Nilitoka pale hospitalini nikamfuata Chloe nyumbani kwao. Nikamwambia sitaweza kumuoa tena, nampenda mtu mwingine. Ilikuwa ngumu sana, lakini niliona ni heri yale maumivu ya wakati ule kuliko aje aumie akiwa mke wangu.” Mwili mzima wa Tunda ulikuwa ukitetemeka.

“Basi, nilirudi hospitalini nikamwambia babu, babu alitabasamu na kuniambia hata baba yangu angekuwepo angenisifu kwa kufanya maamuzi magumu na muhimu kama yale. Kwa hukumu yakuona nimemshindwa kumpa babu yangu kile alichokitamani, kwa kutokuoa akiwepo, nilimuuguza bila kuondoka pembeni yake mpaka alipofariki. Zilikuwa zimebaki siku chache afariki, kwa hiyo mimi ndiye niliyekuwa naye pale hospitalini muda wote.” Tunda alikuwa ameinama huku ameficha uso wake akilia. Net akacheka tena.

“Ungenihurumia pale mama alipokuja kwa mazishi, halafu ananiambia uliondoka Arusha, hajui ulipo. Nilitamani wawe wamenizika mimi sio babu yangu. Nilikasirika sana. Nikahisi Mungu anataka kunichanganya akili tu. Nilikaa Canada sijui nirudi tena huku au niendelee na maisha yangu tu moja kwa moja hukohuko. Mama alipopata matatizo kwenye ile ofisi ya Arusha ilinibidi nirudi kuja kumsaidia.” Tunda akashtuka.

“Alipata matatizo gani tena!?” Tunda akajifuta machozi na kuuliza. “Safia alimtapeli. Kwa kifupi aliiba wateja wote wa mama, kwa kuwaambia hatuna uwezo wa kuwasafirishia tena mizigo yao. Kwa sababu tofauti tofauti. Mara awaambie malori yameharibika, au yote yamesafirisha mzigo sehemu nyingine, kumbe akawa ameingia ubia na mtu mwingine. Anamlipa kwa asilimia 40, kwa kila mteja anayempelekea. Kwa hiyo tukawa tunatumia pesa nyingi kujitangaza, wakipiga kuomba huduma, Safia anawapeleka kwenye kampuni ingine.”

          “Safia alipoona amenogewa, akaja kufungua kampuni kama ileile. Akawa anatumia magari yaleyale ya mama, lakini aliajiri madereva wake. Wale niliokuwa nimeajiri mimi aliwatafutia sababu, mama mwenyewe akawafukuza. Tena aliwafukuza vibaya tu. Basi, Safia akajinufaisha kwa gharama ya mama. Mama kuja kushtuka, akakuta alishafilisiwa kabisa na anadaiwa sana. Alimtia hasara kubwa tu.”

“Tuliuza ile nyumba ya Arusha na yale malori yakiwa kwenye hali mbaya sana, tukalipa madeni yote tukabakia na biashara za huku Dar tu.” “Pole Net.” “Mama amejifunza sana. Aliogopa kuniambia ukweli kama alikufukuza, alijua ningemlaumu sana. Lakini juzi tulipokutana pale hotelini, ulipokuja kwenye kikao,  ukanisimulia kila kitu, nikatamani kujua kwa nini alikubadilikia.” “Ulijua ni kwa nini?” Tunda akauliza kwa upole, lakini Net alionekana kusita kidogo.

“Nimbie tu Net. Nataka kujua nini nilifanya kiasi chakubadilisha moyo wa mama Cote. Alinipokea vizuri sana nilipofika Dar, na alinipenda hata kabla hajaniona akawa haishi kunisifia na kunishukuru kwa kazi nzuri niliyokuwa nikimfanyia. Lakini akaja kubadilika ghafla!” Net akavuta pumzi kwa nguvu huku amefunga macho kama anayejishauri.

“Net?” Tunda akaita tena taratibu akijua kuna kitu Net anataka kumficha. “Unawakumbuka wale wazee wa pale kanisani, ambao uliwahudumia?” Tunda alianza kuogopa. Alihisi kitu. “Mmoja wao alikuwa kwenye mahusiano na mama, walitaka kuja kuniambia, kisha wafunge ndoa.” “Mungu wangu Net!” Tunda aliweka mikono kichwani nakuanza kulia.

“Kwa hiyo aliumia sana, ndio maana alikuchukia.” “Naomba uniombee msamaha kwa mama, Net. Uwii jamani! Balaa gani hili!?” “Tunda! Nimekwambia lazima ukubali kubadilisha historia ya maisha yako.” “Siwezi tena Net.” “Unaweza. Mama ni mmoja ya watu wengi walioumizwa na shetani kupitia wewe. Hujapata fulsa ya kusikia wengine wanasemaje. Huwezi jua ulivunja ndoa za wangapi. Inawezekana ni wengi sana, ndio maana unajukumu la kusimama sasa na kusaidia ndoa nyingine.” Net aliendelea taratibu. Hakuonekana na hasira hata kidogo.

“Ukikubali kushindwa, ujue wapo wengine wanaotumiwa na shetani kama vile ilivyokuwa kwako. Na ujue ndoa au mahusiano mengi yapo hatarini. Wewe sio wa kwanza Tunda, na wala hutakuwa wa mwisho. Wapo waliokubali na kutubu, na wapo wanaokataa na kuendeleza huo uchafu mpaka sasa. Wewe umechagua jambo jema, lazima usaidie wengine. Hata hivyo binafsi nakushukuru, maana bila wewe mama yangu angeolewa na mwanaume anayejua ni mcha Mungu, kumbe ni tapeli tu.” Tunda aliendelea kulia.

“Nakupenda sana Tunda.” “Naomba unisamehe Net. Nisamehe. Nimekuumiza sana. Naomba unisamehe.” Tunda akapiga magoti. “Yamepita hayo Tunda. Nitafurahi kama utaishi na mimi bila hukumu. Mungu amekusamehe, na ni kweli anakupenda. Aliniweka kwenye maisha yako makusudi kunifundisha upendo wake kwa watu tunao wahukumu. Tokea unaishi dhambini, wanadamu wakiwa wanakuchukia na kukuhukumu, Mungu alikuwa akinionyesha mimi upendo wake kwako wewe Tunda.”

“Alinitoa kwenye nafasi ya kukuchukia na kukupenda kupita ninavyoweza kukwambia. Aliuweka uthamani wako bayana kwangu. Na amekuonyesha hata wewe kwa vile alivyo kufanikisha. Amekusamehe, amekupokea na elimu uliyo nayo, na ameonyesha wasomi kuwa anaweza kubariki yeyote ampendaye. Unamaisha mazuri kuliko wasomi wengi hapa nchini! Zaidi amekupa furaha na amani.” “Amenipa na wewe.” Net akacheka. “Ndiyo, na mimi ambaye nitakuwa na wewe kwenye maisha yangu yote.” Tunda hakuwa akiamini.

          Alifunga macho yake tena na kuendelea kulia. Alianza kufikiria maisha yake kama mke wa Net, aliyekuwa anamezewa mate na warembo wengi, wasomi wa kila namna. Waliojitunza na kulelewa kwenye familia nzuri, lakini alishangaa vile Mungu alivyomtunza Net, kwa ajili yake yeye aliyekuwa akihangaika na wanaume wa watu! Tunda alishindwa kunyamaza. Net akamnyanyua pale chini, akakaa naye pale kwenye kochi na kubaki amemkumbatia.

“Nakupenda sana Tunda. Sana.” “Asante Net. Nashindwa niseme nini!” Net akacheka. “Kweli. Mpaka naogopa.” “Unaogopa nini sasa?” Tunda akanyanyua uso wake, akamwangalia. “Nagopa isije kuwa nipo usingizini halafu nikaamka nikakuta kila kitu ni ndoto tu.” “Nini unachohofia zaidi?” “Kukupoteza tena.” “Hata nikiamua kukutoroka, ujue Mungu wako atanirudisha tu.” Wote wakacheka.

Net akambusu Tunda kwenye kipanda uso. Hiyo ni mara ya pili Tunda kupata busu la Net. Kwanza ilikuwa kwenye mkono na hapo ni mara ya pili, na mara zote zilimsisimua. Hata kule kukumbatiwa ilikuwa ni mara yake ya kwanza. Tunda alijivuta karibu sana na Net na kumkumbatia huku akilia tena. Kwa mara ya kwanza alihisi ulinzi mkubwa sana. Alimkumbatia Net kwa kumng’ania huku akilia na kushukuru Mungu kwa kumthamini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda aliyepitia kwa wanaume wengi, hakuwahi kukumbatiwa maishani mwake kwa namna ile ya upendo. Hata tu mtu kutoa muda wake na kumtaka atulie mikononi mwake. Si mama yake mzazi hata wanaume aliokuwa akiwahudumia ilikuwa ni yeye kuwahudumia kwa juhudi zote waridhike, basi, labda kidogo waziri Mbawala tena yeye mwenyewe Tunda alikuwa akiomba kukumbatiwa. Hakuwahi kupendwa na kuthaminiwa vile.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa amejificha hapo kwa Net, wazo la kumtia hofu likamji. “Lakini Net! Umeshafikiria tutakuwa na mahusiano ya namna gani? Kila ninapopita yupo mtu anayenifahamu. Nimemuumiza mpaka mama yako mzazi, Gab naye ndio hivyo, itakuaje? Si itakuwa kama nakudhalilisha tu kila wakati?” “Wao walikuwa wezi tu, mimi ndio nimekabidhiwa na Mungu. Wanatakiwa waniogope mimi sio mimi kuwaogopa. Halafu Tunda, kila mtu anamapito yake, tumetofautiana tu matukio. Unakumbuka ule mfano wa Yesu walipomletea yule mwanamke kahaba?” Tunda akatingisha kichwa kukubali.

“Walikuwa na sababu zote za kumpiga mawe yule mwanamke. Lakini unakumbuka jibu la Yesu?” “Nakumbuka.” “Basi huna haja yakuwa na wasiwasi, na kama nilivyokwambia, hatutasubiri watu watumie maisha uliyoishi zamani kukunyanyasa. Sisi wenyewe tutayatumia kusaidia watu. Itasaidia kama utakuwa jasiri, hata kama watakushtukiza kwa nia ya kukudhalilisha, unatakiwa ujue jinsi ya kutulia wala usikubali hata mara moja mtu akakuumiza.”

“Itakuwaje kuhusu sisi wenyewe Net? Unaweza ukaniamini kama ambavyo ungemuamini mwanamke ambaye hakupita mapito kama yangu? Sitaki kuja kuumia tena. Sitaki uje unionyeshe upande wa pili wa maisha ambao sijawahi ishi, halafu ukanikimbia.” Tunda alianza kutokwa na machozi tena.

“Sijawahi kupendwa na kuthaminiwa tokea mtoto. Wala sijawahi kuishi kwenye familia na mimi nikahusishwa na kuthaminiwa mawazo yangu. Naogopa usije kunionjesha hayo maisha halafu baadaye ukaja kuniacha, Net au tukashindwa kuishi kwa amani sababu yakutokuniamini kila ninapokuwa na mtu mwingine au nimechelewa kurudi nyumbani.”

“Naomba Mungu anisaidie Tunda. Sitakuumiza hata kidogo. Nimeamua kuwa na wewe nikiwa nakufahamu vizuri sana. Sijakurupuka. Ni kitu ambacho nishajiuliza maswali yote ambayo wewe unaniuliza sasa hivi na Mungu amenisaidia kupata majibu yake. Hakuna kipya kitakachobadilika.”

“Nakupenda, na nimekusudia uwe mke wangu. Nakuahidi kukupenda Tunda. Nitakupenda kwa dhati na kukuheshimu, kama Tunda huyu niliyenaye sasa hivi hapa mkononi. Tunda aliyeoshwa na kutakaswa na damu ya Yesu. Sitaishi na Tunda yule wazamani.” “Asante Net. Nakushukuru kunipokea.” Tunda alijirudisha kujiegemeza kwa Net na kukunja miguu juu ya kochi. Wakatulia kila mtu akiwaza lake kama wasio amini.

Tunda alijituliza pale akiogopa hata kusogea. Kichwa pembeni ya shingo ya Net aliyekuwa amepitisha mikono yote miwili juu yake, akimpapasa taratibu kwa mkono mmoja mgongoni. Wakatulia. Kama ambaye haamini, akanyanyua uso kumtizama Net kuhakikisha kama ni yeye. Macho yakagongana. “Nimefurahi sana Net. Siamini!” “Hata mimi nimefurahi.” Tunda akajiweka sawa.

“Sasa ndio tunafanyaje?” “Hatuna sababu yakusubiri tena. Nataka kukuoa Tunda. Nataka uwe mke wangu. Nitaenda kuongea na mama, na wewe kamwambie Mchungaji wako. Taratibu za harusi zianze.”  Tunda akacheka. “Siamini kama na mimi nimepata mtu wa kunioa! Nilijikatia tamaa.”

“Naomba salamu za kukumbatiana na Julius ziwe mwisho.” Tunda alicheka kwa mshangao. “Husahau!?” “Nisahau wakati pale nilikuwa nammezea mate jamaa? Yeye amekumbatiwa wakati mimi sijawahi kukumbatiwa hata mara moja!” Tunda alizidi kucheka. “Eti na mimi nitaanza kuvaa pete za ndoa!” Net akacheka lakini Tunda alipooza ghafla na kujitoa mikononi mwa Net.

“Nini tena?” “Nisipo zaa je? Kama waliharibu kizazi changu wakati wananitoa ile mimba, nikapoteza uwezo wa kuzaa?” “Sijui Tunda. Ila nakuomba usiniingizie hofu nyingii. Naomba unipe nafasi nifurahie hii hatua niliyofikia leo. Hujui nilivyoteseka.” “Samahani Net. Nataka tusiharakishe, tupate muda wakutafakari kwanza tusije tukakosa raha baadaye na kulaumiana.” Hofu ilishamwingia Tunda, akamkumbuka Tunda halisia.

“Naomba unielewe Tunda. Haya mahusino yetu kwako nimageni, lakini si mimi. Mwenzio nimekuwa nayo kwa muda mrefu sana. Nakwambia hayo maswali yote nimeshajiuliza na Mungu amenipa jibu. Nikwambie swali jingine ambalo nimeshajiuliza?” “Swali gani tena!?” Tunda akauliza, akisikika kuishiwa nguvu.

“Itakuwaje kama tukienda kupima, nikakukuta umeathirika? Umeshafikiria hivyo?” Tunda alibaki kama amemwagiwa maji yabaridi. Akajivuta pembeni kabisa. “Sasa hata kabla hatujafika hospitalini mimi na wewe tukapewa majibu yako, mimi nilishachanganyikiwa, nilishakuuguza, tena nilishajiona jinsi nitakavyo kuuguza peke yangu kwa kuwa watu wamekususa, nimeshalia na kuomboleza na Mungu wangu, mwishoni nikaamua kumuachia Mungu, nitembee kwa hatua. Sitaki kuleta matatizo ya siku ya kesho, leo, Tunda. Ndio maana nakuomba uache angalau nifurahie hii hatua ya leo. Naomba tutembee hatua kwa hatua, ili tusije pitwa na chochote.” Tunda alijirudisha vizuri pembeni ya Net, akanyamaza asiamini kama Net ni mtu wa kubaki naye maishani. Sio muondokaji! Amekusudia kuwa naye.

“Sasa hivi kinachofuata nitaenda kumwambia mama. Halafu nianze maisha ya kuwa mchumba wa Tunda. Niwe namtoa mchumba wangu sehemu tofauti tofauti za starehe, nifanye yote ninayotakiwa kufanya kwa mchumba wangu, kabla sijawa mume. Sitaki kupitwa na hatua hata moja kwenye maisha yako Tunda. Hata kama tutaoana mwezi ujao, nataka hizo siku zilizobaki kabla sijakuoa, nikutunze kama mchumba wangu.”

“Nataka nifurahie hatua yangu ya uchumba na wewe, bila kuazima matatizo ya kesho. Leo nataka nikufurahie, msichana niliyekusubiri, na kukutamani kwa muda mrefu sana.” Tunda alikuwa akilia asiamini. Alijutia mapenzi aliyokuwa akiyagawa kwa kujidhalilisha. Hakujua kama yupo mtu mahali fulani anampenda nakumsubiri kwa kiasi kile.

“Nilikuwa nikimuuliza Mungu kwa nini anachelewa kukukabidhisha kwangu! Nilimuhakikishia kila kitu. Nilimwapia nitakupenda mpaka kifo. Nikamwapia sitakusaliti wala kukunyanyasa. Yote hayo niliyafanya kama mwehu ili tu anipunguzie siku za kunikutanisha na wewe.” Akajiegemeza kwenye kichwa cha Tunda, aliyekuwa amemkumbatia, na Tunda alikuwa bado amekaa ubavuni kwa Net, huku amekilaza kichwa chake hapo shingoni.

“Sina cha kusema Net. Sikuwahi hata kuwaza kama unamawazo na mimi! Nilijua utakuwa ukinichukia kwa kunifumania zaidi ya mara nne, tena na wanaume tofauti tofauti! Yaani hata sikuwahi kukuwazia hata sekunde moja. Ila nilikuwa nikikuogopa sana. Kila ulipokuwa ukinifumania nilikuwa nashindwa kulala kwa hofu.” Tunda akakaa vizuri.

“Nilijaribu kujipa moyo kuwa hunihusu, sikujui wala hunijui kwa hiyo haijalishi lakini nilishindwa hujiliwaza. Nikaanza kupunguza wanaume, nikabakia na wachache watakaonisaidia kuniweka mjini, lakini pia bado niliteseka. Haya, mama Cote aliponifukuza Arusha, sikujua hata kama utajali. Nikajua utashukuru Mungu kutuliwa mzigo. Sikuwahi hata kukuwazia kama unaweza kuja kunitafuta tena, Net!”

          “Nilipokuona pale juzi, nilifurahi kukuona kama mtu muhimu ambaye umehusika kwenye maisha yangu. Lakini sikujua hata kama nina maana yeyote kwako. Sikuwa hata nikijua kama uwepo wangu kama una maana yeyote ile au unafanya kutimiza tu wajibu kama mkristo tu wakawaida. Hakika wala sikudhani kama unaweza kuniwazia hivi. Nakushukuru kwa kutokunikatia tamaa.” Net alikuwa akimsikiliza huku akitabasamu. Alimvuta mkono mmoja, akambusu na kubaki wakiangaliana.

“Sasa inabidi nirudi nyumbani tu. Nikiendelea kukaa hapa, naweza kushindwa kuondoka kabisa.” Tunda akatabasamu. “Nitakuona tena lini?” Tunda akauliza, Net akacheka. “Kila siku nitajitahidi tuwe tunaonana. Ila kesho itakuwa mchana, kuna tenda naifuatilia. Nikipata hiyo, najua itamsaidia sana mama. Mambo yake yameenda pabaya sana. Biashara zake haziendi vizuri.” “Mungu atakusaidia Net. Nitakuombea.” Net akatabasamu. “Afadhali nimepata na mke muombaji.” “Umesahau wewe ndio ulikuwa ukinifundisha?” “Siwezi kusahau. Lala. Kesho tutapata muda mzuri wakuongea zaidi.” Net akaaga na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usingizi haukuja kwa Tunda. Alivaa haraka haraka akapanda kwenye gari yake mpaka, Tabata, nyumbani kwa Mchungaji wake. Mlinzi alipoona gari ya Tunda akafungua geti. Shida ikawa kufunguliwa mlango kuingia ndani. “Bwana Mama Penny fungua!” “Hatukusikii, tumelala.” “Sasa mbona unajibu?” “Unataka nini Tunda kwenye dirisha la chumbani kwangu?” “Kuna kitu nataka kukwambia. Siwezi kulala mpaka tuongee.” “Kuna msiba?” “Hapana.” Tunda akajibu.

“Umefukuzwa kwenye nyumba?” “Hapana.” “Basi naomba utuache mimi na mume wangu, tumelala. Washirika wote tumewafundisha kuomba. Hakuna haja yakutugongea milango usiku au simu za usiku usiku hatutaki. Kama mtu anashida, unapiga magoti unaomba, halafu Mchungaji unaonana naye asubuhi.” Tunda akaanza kucheka.

“Sasa muda wote huo unaongea hapo kitandani, mama Penny, dada yangu, si ungeshakuwa umenifungulia mlango, tumeonge, na mimi nimeondoka?” “Sitaki kutoka kitandani bwana! Wengine nyumba zetu zina AC. Usiku tunawasha baridi. Nishajifunika, sitaki kutoka kitandani. Wewe niambie ukiwa hapo hapo dirishani.” Tunda akatulia kwa muda.

“We Tunda?” Mama Penny akamwita. “Nimepata mchumba.” Akaruka kitandani nakuanza kupiga vigelegele. Akawasha taa ya chumbani kwake huku akipiga vigelegele. “Acha kelele mama Penny bwana! Watoto wamelala.” Tunda aliongea kwa sauti ya chini kidogo, kama kumtuliza. “Siamini kama nimepata harusi yakusimamia!” Tunda na Mchungaji wote walicheka kwa sauti.

“Hebu amka baba Penny, tukapange mipango ya harusi.” “Hata mchumba mwenyewe hujaonyeshwa, unataka kuanza mipango!?” “Hebu amka bwana na wewe! Yeyote tutakayeletewa huyohuyo tutampokea ilimradi na mimi nisimamie harusi.” Alimsha watoto wote kwa vigelegele.

“Ingia ndani bibi harusi wangu.” Tunda alifunguliwa mlango. “Kuna nini mama?” Penny akauliza akiwa na usingizi. “Anti Tunda anaolewa?” Pendo naye akauliza baada yakusikia vigelegele vikiendelea bila jibu kutoka kwa mama yao. “Na yule Mzungu?” Penny akauliza tena. Tunda akacheka sana. “Penny wewe! Upo kama mama yako!”

“Hebu niambie Tunda. Mchumba ni nani?” Mchungaji alitoka na yeye akakaa kwenye kochi, mkewe alikuwa akiendelea kushangilia hata mchumba hajauliza. “Acha kelele bwana na wewe mama Penny. Mchumba mwenyewe hata hujamjua!” “Atakuwa ni yule mzungu tu. Wewe hukuwaona hapa walivyokuwa wakiangaliana? Yule mzungu alimpakulia chakula Tunda. Wewe hukuona? Atakuwa ni yeye tu. Eti Tunda mdogo wangu?” “Ni yeye.” Yule mama akaendelea kushangilia.

“Afadhali tutapakata vitoto vya kizungu.” Tunda akacheka sana. “Sasa wewe Penny mwanangu utakuwa msimamizi wa nyuma. Kazi yako kuangalia shela ikae vizuri.” “Sasa nikikaa nyuma, kwenye picha si sitatokea!?” “Utatokea kwenye harusi yako.” Mama yake akamjibu na kufanya wote wacheke.

“Mama Penny naomba ukae chini bwana tuongee.” “Tunaongea nini? Hapa ni mipango ya harusi tu.” “Si ndio hivyo sasa! Mimi nilijua wewe ndiye utakuwa mpambaji wa ukumbi na Mchungaji ndiye atatufungisha harusi.” “Aka! He! Wewe Tunda ukoje? Mimi na mume wangu ndio wasimamizi. Akitaka mwenyewe atafungisha hiyo ndoa, halafu atachukua nafasi yake ya kumsimamia bwana harusi tukitoka kanisani. Lakini mimi nasimamia kila mahali.” Tunda alitingisha kichwa huku akicheka.

“Sasa nani atapamba ukumbi!?” “Mimi na wewe haituhusu, kwani sisi wanakamati bwana? Hebu tuongee mambo ya msingi.” “Haya Penny na mdogo wako, mkalale.” Baba yao akaingilia. “Lakini mimi sitaki kusimamia nyuma, dady!” Penny akalalamika. “Mama yako ameshakwambia, utulie mpaka utakapokuwa mkubwa, ukileta mchumba wako, siku yako ya harusi utasimama mbele. Sasa hivi unakwenda kulala, kesho shule. Haya simama haraka kabla sijakubadilikia.” Tunda akabaki akicheka, Penny na mdogo wake wakasimama kuelekea chumbani kwao kulala huku Penny akilalamika “Na mimi nataka kutokea kwenye picha! Sitaki kusimama nyuma.” Akapotelea chumbani kwao huku akilalamika.

“Kweli hawa watoto wamepata wazazi!” Tunda aliendelea kucheka. Waliongea kwa muda mrefu sana, Tunda akitoa historia yake na Net, tena na tena huku machozi yakimtoka. “Ulikuwa unamzungusha Julius wa watu, kumbe unaye mwanaume wako!” “Mungu wangu nishahidi mama Penny. Sikuwahi kumfikiria Net kuja kuwa naye kwenye mahusiano hata kidogo!  Hata dunia yote tungebaki mimi na yeye tu, pia nisingefikiria kama yule kaka angekuja hata kutamani niwe mpenzi wake! Sikuwahi hata kumuhisi. Net anamaadili na msimamo wakupita kiasi. Kwanza nilikuwa nikimuogopa ile yakutetemeka.” Waliongea mpaka usiku sana, ndipo Tunda aliporudi kwake.

Kwa Net!

Huku kwa Net nako, alirudi mpaka nyumbani kwao. Alimkuta mama yake sebuleni akisoma kitabu. Alipomuona tu Net akaweka kitabu chini. “Sijawahi kukuona ukiwa na furaha hivyo! Kuna nini?” “Tunda amenikubali mama.” “Hebu tulia kwanza. Tunda amekukubali!?” “Yaani ni hivi, Tunda amekubali nije kuwa mume wake.” Yule mama alishtuka sana, akavua miwani. Net alimuona jinsi mama yake alivyobadilika.

“Tunda, Tunda!?” “Ndiyo mama. Tunda.” “Sijaelewa. Tunda huyu unayemzungumzia ndiye Tunda huyu Malaya! Aliyekwisha shika mimba ya baba yake. Aliyevunja uchumba wangu na kuvunja ndoa ya Mzee Mati baada ya mkewe kujua alikuwa akihudumiwa na huyo Tunda na kumpeleka na mwenzie Meto! Aliyetembea mpaka na Gabriel, ambaye ni kama kaka yako!? Achilia mbali msururu wa wanaume za watu ambao alishakuwa na mahusiano nao kimapenzi!?”

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Itakuaje? Tunda akiwa na furaha yakupitiliza, maisha ya nyuma yanapambana kumtoa Tonge mdomoni


0 comments: